https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Saturday, March 16, 2013

Yanga yawatia tumbo joto Simba, mkutano wao kufanyika kesho


Kikosi cha Yanga SC
Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
MKUTANO Mkuu wa Dharura unaotarajiwa kufanyika Machi 17 mwaka huu katika Hoteli ya Star Light, Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam, umepangwa kuwa suluhu ya kuiweka Simba imara katika muendelezo wa ligi ya Tanzania Bara, ikiwapo mechi dhidi ya Yanga.

Mkutano huo umetangazwa tena jana jijini Dar es Salaam na Mratibu wa wanachama zaidi ya 600, Mohamed Wande, akieleza kuwa wamefuata taratibu zote za kisheria, likiwapo jeshi la Polisi wilayani Ilala, Ofisi za Utamaduni Ilala, pamoja na msajili wa vyama vya michezo.


Akizungumza kuhusu maadalizi ya mkutano huo wa kesho, Wande alisema ni dhahiri klabu yao ipo kwenye hali mbaya, kiasi cha kutishia huenda wakapata mvua ya mabao kutoka kwa mtani wao wa jadi Yanga, kama hawatakutana haraka na kujadili mwenendo mbaya wa timu yao.

Alisema kuwa ingawa mwanzo mkutano wao ulizuiwa hatua za mwisho kutokana na hila za mwenyekiti wao, Ismail Aden Rage, lakini wanaamini wanachama wa Simba wataendelea kuipigania klabu yao.

“Tumefuata hatua zote za kufanikisha mkutano huu muhimu wa Simba, huku tukiamini kuwa utarudisha heshima za timu yetu, ikiwamo mechi yetu na Yanga, itakayopigwa baadaye mwezi ujao.

“Sisi wanachama na wapenzi wa Simba, tunaona njia kuu ya kuiwezesha timu kuwa pazuri kwa kufanya mkutano huu wa dharula ambao kwakweli tunaomba watu wote waje bila kuchoka,” alisema.

Wande alisema kuwa katika mkutano huo hakutakuwa na vurugu zozote, huku akiamini kila mwanachama anayestahili kuwapo atahudhuria kwenye mkutano wao wa kuinusuru klabu ya Simba.

Mkutano wa Simba unafanyika huku wanachama wakiwa na kumbukumbu ya viongozi wao wa juu, akiwapo Makamu Mwenyekiti Geoffrey Kaburu na Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili, Zacharia Hans Pope kuachia ngazi na kuundwa pia Kamati ya Ushindi, ikiwa chini ya Malkia wa Nyuki, Rahma Al-Kharoos.

Kwa upande Msemaji wa klabu ya Simba, Ezekiel Kamwaga, alisema kuwa hawautambui mkutano huo, maana umeitishwa na watu wasiokuwa na uwezo wa kufanya hivyo, isipokuwa mwenyemkiti peke yake.


Alisema hakuna mwanachama mwenye uwezo wa kuitisha mkutano, badala yake wangesuburi mwenyekiti wao apone na kurudi Tanzania, ili ashughulikiea masuala ya mkutano huo wa Simba.

“Nashauri wanachama wa Simba wajiepushe na mkutano huo, maana tumetoa taarifa sehemu husika, huku tukiamini kuwa hautafanyika kwasababu haujakidhi vigezo vyote.

“Hata hivyo, Katiba ya Simba SC, Ibara ya 22, inatamka wazi kuwa wanachama wasiopungua 500 wana uwezo wa kuitisha Mkutano wa Dharura, endapo watajiorodhesha kwa Kamati ya Utendaji.

Kutokana na orodha hiyo, wanachama zaidi ya 600 wamejitokeza na kusaini juu ya mkutano huo, hali inayoupa uhalali kwa kiasi kikubwa, hasa katika kipindi hiki ambacho mwenyekiti hayupo, Makamu mwenyekiti amejiuzulu.




No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...