https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Tuesday, March 12, 2013

Ruaha Marathon kutangaza utalii wa ndani


Mratibu wa Ruaha Marathon, Albert Sanga

Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
MRATIBU wa mashindano ya riadha ya Ruaha Marathon, Albert Sanga, amesema kwamba wanaamini mbio hizo zitafanikiwa kwa dhati kutangaza utalii wa ndani, kwa kushirikisha wanariadha zaidi ya 2500 kutoka nchi mbalimbali duniani.


Mashindano hayo yamepangwa kufanyika Mei 25 mwaka huu mkoani Iringa, ikiwa ni mara ya pili kufanyika baada ya mwaka jana kufanyika pia kwa mafanikio makubwa.

Akizungumza kwa njia ya simu kutoka mkoani Iringa, Sanga, alisema kwamba lengo ni kuhakikisha kuwa wanaendeleza mchezo huo pamoja na kutangaza utalii wa ndani kwa kuona kuwa watu kutoka nchi mbalimbali wanashiriki.

Alisema kuwa Ruaha Marathon ni kwa ajili ya Watanzania wote, huku lengo lingine ni kukusanya fedha za kuwasaidia watoto walemavu.

“Mamia ya washiriki kutoka Italia, Canada, Marekani, Uingereza, Australia, Kenya, Ethiopia, Afrika Kusini na nchi nyingine wamethibitisha ushiriki wao kwenye mashindano hayo yenye mguso mkubwa mkoani Iringa na Tanzania kwa ujumla.

“Naamini mambo yatakuwa mazuri kwa kuona kuwa tunafanikisha mashindano haya kwa kiwango cha juu na kuendeleza sekta ya michezo pamoja na kutangaza utalii wetu ambao kwa hakika utakuwa na tija kwa namna moja ama nyingine,” alisema.

Kwa mujibu wa Sanga, watu wa kada mbalimbali, wakiwamo mawaziri, wabunge na wengineo nao watakuwapo kwenye mashindano hayo kuangalia kila kitakachojiri kwa siku hiyo maalum ya Ruaha Marathon mkoani Iringa.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...