https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Wednesday, March 27, 2013

Serikali yakunjua makucha mgogoro wa Hifadhi za Loliondo

Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
SERIKALI imedhamiria kutenga sehemu ya Pori Tengefu la Loliondo lenye ukubwa wa Kilomita za Mraba 1,500 kutoka kwenye sehemu ya Kilomita za Mraba 4000 za pori hilo ili kutatua migogoro inayoendelea katika hifadhi hiyo.
 Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Khamis Kagasheki, akizungumza na waandishi wa habari.


 Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Khamis Kagasheki.
Waandishi wakimsikiliza Waziri Kagasheki jana.
Hayo yamesemwa jana na Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Khamis Kagasheki, alipokuwa anazungumza na waandishi wa habari juu ya eneo la Loliondo linavyoendelea kutafunwa na migogoro kutokana na muingiliano wa matumizi ya ardhi katika eneo lililotengwa na kutangazwa na serikali kuwa pori tengefu la Loliondo.

Waziri Kagasheki alisema kwamba katika adhma hiyo itakayochukuliwa bila kuingiza hisia zozote za kisiasa, wataokoa hadhi ya Pori hilo na kulinda pia mazalia ya wanyama pori, mapitio na vyanzo vya maji kwa ajili ya ustawi wa hifadhi na manufaa kwa Watanzania wote.

“Serikali itasimamia eneo litakalobaki kuwa Pori Tengefu kwa mujibu wa Sheria za Uhifadhi wa Wanyamapori, huku ardhi itakayobaki baada ya kuondoa eneo hilo likiachwa kwa wananchi, kijiji namba 5 ya mwaka 1999.

Wananchi watawezeshwa kuanzisha eneo la Jumuiya ya Hifadhi za Wanyamapori (WMA), katika ardhi itakayobaki ya kijiji kwa mujibu wa sheria, huku tukijua kuwa huo utakuwa mpango bora wa matumizi ya ardhi katika vijiji vya eneo la Loliondo, yakiambatana na mifugo, ikienda sanjari na majosho, malambo ya maji ya mifugo, minada na mengineyo,” alisema Kagasheki.

Aidha Kagasheki alisema kuwa muhimu ni wananchi hao kufuga kisasa na kuzingatia ukubwa wa eneo lao (Carrying Capacity), ili isilete madhara kwa kwa eneo husika.

Waziri alisema kuwa katika uamuzi wao huo, kamwe hawataangalia wanasiasa wanataka nini, hasa wale wanaopita na kurubuni watu kwa ajili ya kuendelea kukuza mgogoro huo kwa ajili ya kuhitaji kura au kulinda kwa kujipendekeza kwa wapiga kura wao bila kufuata sheria za nchi.

Kwa mujibu wa Kagasheji, serikali itapitia na kuangalia  ukubwa wa maeneo waliyopewa baadhi ya wawekezaji, wakiwamo OBC na ikibidi kupunguzwa na kuwagawa kwa wananchi, huku tukishirikiana kwa karibu na wenzetu, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ili kuona uhalali wa Kampuni zinazomiliki ardhi katika eneo linalohifadhiwa kwa madai kuwa wameuziwa na serikali za vijiji.

 

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...