https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Monday, June 29, 2015

SIWEZI KUVUMILIA: Mashabiki wamekosea, ila Stars imekosea zaidi

Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
NI miongoni mwa wadau wa michezo hususan mpira wa miguu waliohudhunishwa na kitendo cha hivi karibuni cha baadhi ya mashabiki wa soka walioamua kuwazomea wachezaji wa timu ya Taifa (Taifa Stars), hali iliyoibua utata baina yao. Ingawa nilihudhunishwa na suala hilo, lakini pia nilihudhunika zaidi kwa kitendo cha wachezaji kushuka na kufanya fujo kwa mashabiki wao, ambao kimsingi wameguswa na matokeo mabovu ya timu yao ya Taifa, licha ya kuwa na mapenzi nayo. Hapa ndipo nisipoweza kuvumilia. Siwezi kuvumilia kwa sababu inaonyesha wachezaji hawana nidhamu. Na hawajui kuwa kiasi gani matokeo yao mabaya hupelekea wengine kuugua au kujisikia vibaya.

Hii haiwezi kukubalika na haivumiliki pia. Ni wakati sasa wachezaji wa Stars kujua wana deni kubwa. Wanapoingia uwanjani wahakikishe kuwa wanafanya kila wawezalo kupata ushindi. Na inapotokea wanapata matokeo mabaya, lazima wajue pia watawafanya mashabiki wao wahisi presha. Ni kutokana na presha hizo, baadhi ya wadau na mashabiki wanaona hakuna njia nyingine ya kufikisha ujumbe kwa wachezaji wao zaidi ya kuzomea.

Ingawa hii si tabia nzuri dhidi ya mashabiki hao, lakini kwa wachezaji kushuka chini na kufanya vurugu ni kubaya zaidi. Ingekuwaje kama mashabiki hao walipoanza kuzomea gari lingeondoka, mashabiki hao wangelikimbilia hadi linapoishia? Ni wazi wangeliacha ili waendelee na zao. Ni wakati wetu sasa kila mtu kuwa na mapenzi dhidi ya mwenzake. Wachezaji wawe na nidhamu mbele ya mashabiki wao hali kazalka mashabiki nao wawe na nidhamu kwa wachezaji wao.

Kucheza mpira si jambo dogo. Kunahitaji nguvu na akili kubwa katika kusaka ushindi uwanjani, hivyo kuna kila sababu ya kuona namna gani ushindi unapatikana. Huu ndio ukweli wa mambo. Kinyume cha hapo tutaendelea kuona mwenendo mbaya dhidi ya timu yetu, huku wachezaji wetu wakiongeza ukali kwa mashabiki wao. Je, watawatoa roho? Huu ndio ukweli wa mambo. Mashabiki kuwafanyia vurugu wachezaji wao ni kibaya, ila wachezaji nao kushuka chini kufanya fujo ni kubaya zaidi. Ingekuwaje kama wachezaji wangeumizwa kwenye vurugu hizo?

Tubadilike kama kweli tunahitaji maendeleo ya mpira wa miguu.
Tuonane wiki ijayo.
kambimbwana@yahoo.com
+255 712053949

Kongamano la maendeleo endelevu lafanyika kwa mafanikio

IMG_4628
Mkurugenzi Mtendaji mpya wa Taasisi Huru ya Utafiti wa Uchumi na Jamii (ESRF), Dk. Tausi Kida, akitoa maelezo ya kongamano kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi kulifungua kongamano kubwa la siku mbili la kujadili namna taifa linavyojiandaa kutekeleza malengo mapya ya Maendeleo endelevu (SDGs) limefanyika mwishoni mwa wiki mjini Dodoma ambalo liliandaliwa na taasisi yake.

Na Mwandishi wetu, Dodoma
KONGAMANO kubwa la siku mbili la kujadili namna taifa linavyojiandaa kutekeleza malengo mapya ya Maendeleo endelevu (SDGs) limefanyika mwishoni mwa wiki mjini Dodoma. Kongamano hilo lililoandaliwa na Taasisi ya Utafiti ya Masuala ya Uchumi na jamii (ESRF) limelenga kuwakutanisha wataalamu kutoka Tanzania Bara na Visiwani kujadili namna ya kupata fedha za kutekeleza malengo hayo baada ya kumalizika kwa malengo ya maendeleo ya millennia (MDG’s) baadae mwaka huu.

Miongoni mwa mambo yaliyojadiliwa katika kongamano hilo ambapo wataalamu wa Umoja wa Mataifa wa maendeleo walishiriki ni pamoja na namna ya kupata fedha kwa ajili ya maendeleo baada ya Septemba mwaka 2015 kwa kuangalia rasilimali za ndani. Mada hiyo imetokana na ukweli kuwa upatikanaji wa fedha za ndani ndio suluhu ya utekelezaji wa malengo mapya kwa kuwa awali kwenye MDG’s utekelezaji wa malengo ulikwamishwa na kukosekana kwa fedha kutoka kwa wafadhili ambao waliahidi kuchangia maendeleo.

Friday, June 26, 2015

TFF yafungua kozi ya makocha vijana, timu sita zapanda ligi daraja la pili

Na Mwandishi Wwetu, Dar es Salaam
Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini (TFF) leo limefungua kozi ya makocha wa mpira wa miguu kwa watoto na vijana kwa nchi nzima kwa lengo la kuhakikisha vijana wengi wanapata nafasi ya kufundishwa mpira na kuucheza mpira kuanzia katika umri mdogo.

Akifungua kozi hiyo, Katibu Mkuu wa TFF Mwesigwa Selestine amesema ili nchi/Taifa lifanikiwe katika soka ni lazima kuwekeza katika mpira wa watoto na vijana ambao makocha hao ni sehemu ya uwekezaji huo. “Tumekua na mashindano ya Taifa U-13, kikosi cha timu ya Taifa ya U-15 ambayo inashirikisha vijana wadogo, vijana hao wanapaswa kupata malezi na mafunzo yenu waalimu ili wafikiapo kuchezea timu za Taifa wawe wamekua kwenye msingi bora wa kuujua mpira wa miguu” alisema Mwesigwa.


Naye mkufunzi wa FIFA wa kozi hiyo ya makocha kutoka nchini Ujerumani, Eric Muller amesema hata ujerumani imefanikiwa baada ya kuwekeza katika soka la vijana, mwaka 2000 kwenye fainali za Euro nchi yao ilishika nafasi ya mwisho katika msimamo kundi lao kwa kupata poniti moja, lakini uwekezaji walioufanya kwenye soka la watoto na vijana umewapelekea kutwaa Ubingwa wa Dunia mwaka 2014.


Washiriki wa kozi hiyo ni makocha wa timu za vijana za mikoa yoye Tanzania, ambao watashirki na timu zao za mikoa katika michuano ya Copa Coca Cola mwaka huu.
Kozi hiyo ya makocha wa timu za watoto/vijana inayoendeshwa na wakufunzi wa FIFA, Ulric Mathews kutoka shelisheli na Eric Muller kutoka nchini Ujerumani itamalizika jumatatu tarehe 29 Juni, 2015.

Thursday, June 25, 2015

Wana CCM 21,000 wamdhamini Bernard Membe mkoani Pwani katika mbio zake za urais

 Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa na Mbunge wa Jimbo la Mtama, Bernard Membe akilakiwa na umati wa wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na wananchi waliofurika nje ya viwanja vya ofisi ya CCM Wilaya ya Kibaha Mjini mkoani Pwani jana, wakati alipofika kutafuta wadhamini ili aweze kuwania urais katika uchaguzi mkuu ujao kwa tiketi ya chama hicho, ambapo wanaCCM zaidi ya 21,000 walimdhamini. Picha zote na John Badi.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa na Mbunge wa Jimbo la Mtama, Bernard Membe (kushoto) akipokea lundo la bahasha lenye fomu zilizojazwa na wanaCCM wa Mkoa wa Pwani zaidi ya 21,000 kutoka kwa Kada wa CCM, Pili Chande wakati alipofika katika Ofisi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Wilaya ya Kibaha Mjini jana, kwa ajili ya kutafuta wadhamini ili aweze kuwania urais katika uchaguzi mkuu ujao kwa tiketi ya chama hicho. Anayeshuhudia (katikati) ni Mwenyekiti wa CCM Wilaya hiyo, Maulid Bundala.

Mbunge Nassari amaliza mikutano ya kuhamasisha wananchi kujitokeza kujiandikisha kupiga kura

Rubani wa Helkopta akimfunga mkanda Mbunge wa jimbo la Arumeru Mashariki ,Joshua Nassar kabla ya kuanza safari ya kuelekea katika mikutano ya hadhara ya kuhasisha wananchi kujitokeza kujinadikisha katika daftarai la kudumu la wapiga kura.
Wananchi katika kata ya King'ori wakimpokea Mbunge Nassari wakati alipowasili katika mkutano wa hadhara wa uhamasishaji zoezi la uandikishaji .
Kada wa Chadema ,Samwel Nnko akizunumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika kata ya King'ori .

Wednesday, June 24, 2015

Mdau wa masumbwi nchini Tanzania afunga ndoa


Refarii wa mchezo wa masumbwi nchni kushoto akiwa na mke wake Aisha Chilumba  baada ya kuoa hivi karibuni maeneo ya Vingunguti Dar es salaam. Picha kwa hisani ya Rajabu Mhamila

Mamia wamdhamini Bernard Membe Morogoro, wasanii wamiminika kumuunga mkono

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa na Mbunge wa Jimbo la Mtama, Bernard Membe akizungumza na wasanii wa tasnia ya filamu mkoa wa Morogoro jana, wakati alipokuwa mkoani humo kwa ajili ya kutafuta wadhamini ili aweze kuwania urais katika uchaguzi mkuu ujao kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambapo wanaCCM zaidi ya 950 walimdhamini. Picha zote na John Badi.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa na Mbunge wa Jimbo la Mtama, Bernard Membe akiwa katika picha ya pamoja na wasanii wa tasnia ya filamu mkoa wa Morogoro jana, wakati alipokuwa mkoani humo kwa ajili ya kutafuta wadhamini ili aweze kuwania urais katika uchaguzi mkuu ujao kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambapo wanaCCM zaidi ya 950 walimdhamini.

Tuesday, June 23, 2015

Bayport Financial Services yamfuta machozi Latifa Juma kwa kumpa hundi ya Bima ya Sh Milioni 3

Mratibu wa Bima ya Elimu kwa Uwapendao kutoka Taasisi ya Kifedha ya Bayport Financial Services, Ruth Bura, kushoto akimkabidhi hundi Latifa Juma yenye thamani ya Tsh 3,000,000, baada ya mzazi wake Juma Said, aliyekuwa Mchapa Vitabu wa Shule ya Uhuru Mchanganyiko, jijini Dar es Salaam. Kulia ni mume wa Latifa, anayeitwa Bakari Msumi. Picha zote kwa Hisani ya Bayport Financial Services.

Na Mwandishi Wwetu, Dar es Salaam
TAASISI ya Kifedha ya Bayport Financial Services, leo jioni imemkabidhi hundi ya Sh Milioni tatu (3,000,000), mjasiriamali Latifa Juma, ikiwa ni sehemu ya mafao yake baada ya mzazi wake Said Juma, kuwa mteja wa Bayport kwa kupitia huduma yake ya Bima ya Elimu kwa Uwapendao iliyoanzishwa mapema mwaka jana.

Makabidhiano hayo yalifanyika Makao Makuu ya Bayport Financial Services, Morocco, jijini Dar es Salaam, huku akisindikizwa na mumewe Bakari Msumi. Akizungumza katika makabidhiano hayo, Mratibu wa Bima ya Elimu kwa Uwapendao ya Bayport Financial Services, Ruth Bura, alisema kwamba marehemu Said Juma alikuwa mteja wao, huku akijiunga pia katika huduma ya bima, ambayo leo imemnufaisha mtoto wake.

Mratibu wa Bima ya Elimu kwa Uwapendao kutoka Taasisi ya Kifedha ya Bayport Financial Services, Ruth Bura, kushoto, akiwa kwenye makabidhiano ya hundi Latifa Juma yenye thamani ya Tsh 3,000,000, baada ya mzazi wake Juma Said, aliyekuwa Mchapa Vitabu wa Shule ya Uhuru Mchanganyiko, jijini Dar es Salaam. Kulia ni mume wa Latifa, anayeitwa Bakari Msumi. Picha zote kwa Hisani ya Bayport Financial Services.

Alisema mapema mwaka huu mteja wao alifariki Dunia, hivyo baada ya kupata taarifa hizo tuliamua kufuatilia na kukutana na mtoto wake Ratifa, ambaye hapana shaka fao hili linaweza kumuendeleza zaidi na zaidi. “Bayport Financial Services kama kawaida yetu tumekuwa na lengo la kuwakomboa wateja wetu kwa kuwapatia mikopo mbalimbali kama vile mikopo ya fedha, mikopo ya bidhaa ikiwamo huduma yetu mpya ya mikopo ya viwanja vya Vikuruti, wilayani Kibaha, mkoani Pwani, bila kusahau fao la Bima ya Elimu ambalo lina umuhimu mkubwa.

“Naomba Watanzania wote waweke utaratibu wa kujiunga na bima hii ambayo malipo ya kila mwezi kwa fao la Bronze ni Sh 3500 tu, huku mafao yake yakiwa ni Sh 1,800,000, huku Makato ya bima ya Silver yakiwa ni Sh 7,000 na fao lake ni Sh 3,700,000 na Gold akilipwa mteja Sh 7,500,000 wakati makato yake yakiwa ni Sh 12,000 tu kwa mwezi,” alisema Ruth.
Naye Ratifa aliwashukuru Bayport kwa huduma zao nzuri, huku akisema mafao ya baba yake yatachangia kwa kiasi kikubwa kuboresha maisha yake na mama yake, hususan kwa kuendeleza ujenzi wa nyumba yao.

Friday, June 19, 2015

Zambia na Tanzania zaingia makubaliano ya kurahisisha uchukuzi wa mizigo na abiria

Waziri wa Fedha wa Tanzania, Bi Saada Mkuya, na Waziri wa Uchukuzi, Ujenzi na Mawasiliano wa Zambia, Yamfwa Mukanga wakisaini hati ya makubaliano ya kurahisisha uchukuzi wa mizigo na abiria katika nchi hizo mbili, , leo mchana katika ukumbi wa St Gasper mjini Dodoma huku wakishuhudiwa na Naibu Waziri wa Wizara ya Fedha Tanzania, Adam Malima( wa kwanza kulia waliokaa), Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Servacius Likwelile (wa tatu kutoka kulia waliosimama), Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Dkt. Shaaban Mwinjaka (wa pili kutoka kulia waliosimama) na wataalam kutoka Tanzania na Zambia.

Makamu wa Rais, Dkt Bilal aagana na Balozi wa Palestina aliyemaliza muda wake nchini Tanzania

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akisalimiana na Balozi wa Palestina nchini Tanzania, Nasir Abu Jaish, wakati alipofika Ofisini kwake Ikulu jijini Dar es Salaam, leo Juni 19, 2015 kwa ajili ya kumuaga baada ya kumaliza muda wake wa kazi nchini. Picha na OMR

Waandishi wa Tanzania watembelea shamba la mamba nchini Zimbabwe

IMG_2835
Pichani ni Mhudumu wa Mapango ya Chinhoyi Cephas Sithole akitoa maelezo kwa timu ya waandishi wa habari waliombatana na wadau wa utalii kutoka nchini Afrika Kusini kwenye ziara hiyo ya kutembelea vivutio vya utalii nchini Zimbabwe katika mapango Chinhoyi.(Picha zote na Zainul Mzige).
Waandishi wa habari kutoka vyombo 5 vya habari vya magazeti ya Tanzania ikiwemo mtandao wa habari wa modewjiblog ambao ni Justin Damiana (The African), Frank Aman (The Guardian), Zainul Mzige (modewjiblog), Mariam Said (Daily News) pamoja na Timothy Kitundu (East Africa Business Week) walipata mwaliko kutoka Mamlaka ya Utalii ya Zimbabwe (ZTA) kufanya utalii katika mapango ya Chinhoyi, Ziwa Kariba, Shamba la ufagaji wa Mamba, Hifadhi ya Taifa ya Kariba, Bandari ya Zambezi pamoja na ukuta wa bwawa la Kariba unaotengenisha nchi ya Zambia na Zimbabwe.

Thursday, June 18, 2015

Kongamano la upatikanaji wa fedha za ndani za maendeleo lafanyika jijini Arusha

CDF 1
Mratibu Mkazi Mashirika ya Umoja wa Mataifa (UN) na Mwakilishili wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) nchini, Alvaro Rodriguez ambaye alikua mgeni rasmi katika Kongamano la upatikanaji wa fedha za ndani za maendeleo akitoa hotuba yake kwa washiriki kutoka Halmashauri za wilaya nchini lililofanyika jijini Arusha.

Na Mwandishi wetu, Arusha
MFUKO wa Umoja wa Mataifa wa Ukuzaji Mitaji (UNCDF) kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), umeitisha kongamano la siku mbili la upatikanaji wa fedha za ndani kwa maendeleo. Kongamano hilo linahusisha wakurugenzi wa mamlaka za serikali za mitaa nchini Tanzania na linashirikisha watu 110.

Pamoja na wakurugenzi hao, wapo na wawakilishi kutoka Serikali Kuu na wawakilishi walioteuliwa kutoka serikali za mitaa za Uganda, Senegal na Benin.
Kwa mujibu wa taarifa ya UNCDF, nia ya kongamano hilo ni kuonesha mafanikio ya mfumo wa ukusanyaji wa fedha za ndani kuwezesha ujenzi wa miundombinu ya kiuchumi ya kibiashara katika nchi za Tanzania na Uganda. Taarifa hiyo imesema kwamba baada ya kujifunza mafanikio hayo washiriki watajadiliana na kujipanga kwa ajili ya utekelezaji wa mfumo huo katika nchi zao wanaokotoka ili kupiga hatua mbele katika uendelezaji wa miradi bila kutegemea fedha za nje.
CDF 2
Mkuu wa Mfuko wa Umoja wa mataifa wa Ukuzaji Mitaji (UNCDF) nchini na Meneja wa LFI duniani, Peter Malika akizungumza wakati Kongamano hilo.

TANAPA wakabidhi mradi wa ujenzi wa bweni katika shule ya Sekondari Nuru, wilayani Siha

Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro ,Leonidas Gama akisalimiana na wanafunzi wa shule ya sekondari Nuru iliypo wilayani Siha alipowasili kwa ajili ya makabidhiano na ufunguzi wa Bweni la wananfunzi lililojengwa kwa ufadhili wa hifadhi za taifa Tanzania (TANAPA).
Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro,Leonidas Gama akizungumza katika hafla fupi ya makabidhiano hayo.

Stephen Wassira asema hana majina ya washukiwa wa ufisadi Tanzania

Na Mwandishi Wetu, Rukwa
MGOMBEA anayeomba kuteuliwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuwania Urais katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu, Steven Wasira, amesema hana majina ya washukiwa wa ufisadi, ingawa uovu huo umo ndani ya vyama vya siasa ikiwamo CCM.
Stephen Wassira, akizungumza katika mkutano wa kuomba kudhaminiwa kwa ajili ya kupitishwa na CCM kuwania urais, mwezi Oktoba mwaka huu.

Wasira anayeongozwa na kauli mbiu ya Uadilifu na Umoja wa Watanzania; Safari ya Uhakika, alisema hayo wakati akizungumza na wana-CCM waliomdhamini katika mikoa ya Rukwa na Katavi jana.

Alisema CCM na serikali yake ni taasisi zilizo na misingi ya uadilifu, ingawa ndani yake kuna uwezekano wa kuwapo watu wanaotuhumiwa kwa uhalifu huo.
Alisema ufisadi na rushwa na miongoni mwa matatizo makubwa yanayoiathiri jamii na kwamba taifa linamhitaji kiongozi asiyekuwa na kashfa inayomfanya atiliwe shaka katika kukabiliana na kadhia hiyo.

“Hapa sina majina ya mafisadi lakini ninaamini kwamba si ndani ya CCM pekee, bali hata katika vyama vingine vya siasa, rushwa na ufisadi ni miongoni ma matatizo makubwa yanayovikabili,” alisema.

Wasira alisema kutokana na hali hiyo, vita dhidi ya rushwa na ufisadi inapaswa kuwa katika misingi ya hoja na uthubutu wa kuidhibiti badala ya kumlenga mtu binafsi.

Monday, June 15, 2015

SIWEZI KUVUMILIA: Sakata la Singano na hadithi ya fisi akiwa hakimu

Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
INAHITAJI akili za kiuwendawazimu kukubali mwenendo mbovu wa soka la Tanzania, linaloendeshwa kwa mizengwe mizengwe. Leo mtu anaweza kuharibu mkataba wa kisheria kwa makusudi na bado asiburuzwe katika vyombo vya sheria.

Ndio, maana tumeshuhudia Shirikisho la Soka nchini (TFF) kulimaliza sakata la mchezaji wa Simba, Ramadhan Singano ‘Messi’, kitu ambacho wengi walikitarajia. Hii ni aibu kubwa, maana TFF waliamua kulifunika funika.

Mwenyewe Singano anasema anamuachia Mungu. Pengine aliyasema haya kwa sababu alijua kwamba hawezi kuipata haki aliyokusudia. Kama hivi ndivyo, nakumbuka msemo mmoja wa Kiswahili usemao ‘Fisi akiwa hakimu, mbuzi sheria hana’. Ndio, TFF wao wanamtaka Singano na klabu yake warekebishe mapungufu kwenye mkataba wao.

Kurekebishwa kunaashiria kuwa kuna tatizo kubwa. Lipi hilo? Kwanini tatizo hilo lisiwekwe hadharani ili kila mmoja alijuwe? Hii inaonyesha kwamba kuna dalili za kulindana. Ni wazi kati ya Simba au Messi, kuna mmoja anatatizo.

Ila kulifumba fumba si njia ya kusuluhisha mzozo huo. Hata kama leo hili likiisha, vizazi vinavyo vitaendelea kuwa na kasumba hii. Hapa ndipo nisipoweza kuvumilia. Siwezi Kuvumilia kuona soka letu linaendelea kuendeshwa kienyeji na kiubabaishaji.

Wananchi walivyotembelea mradi wa viwanja wa Bayport Vikuruti na kuvutiwa nao

Baadhi ya wananchi wakiangalia ramani katika mradi wa viwanja unaoendeshwa na Taasisi ya Kifedha ya Bayport Financial Services, katika eneo la Vikuruti, wilayani Kibaha, mkoani Pwani mwishoni mwa wiki na kusimamiwa na Meneja Mauzo wa Taasisi hiyo Nasra Sudi. Picha zote na Mpigapicha Wetu.
 Wananchi waliokwenda kuonyeshwa viwanja hivyo wakipata somo la mradi huo wa vianja vya Vikuruti unaoendeshwa na Taasisi ya Bayport Financial Services.
 Wananchi hawa wakiangalia kwa makini ramani ya viwanja vya Vikuruti, vinavyoratibiwa na Taasisi ya Kifedha ya Bayport Financial Services, mwishoni mwa wiki. Zoezi la viwanja hivyo kwa watumishi wa umma, wafanyakazi wa kampuni binafsi na wajasiriamali linaendelea hadi Juni 30 mwaka huu, ambapo kila Mtanzania anaweza kupata kiwanja hicho kwa fedha taslimu au kwa mkopo. Thamani ya viwanja hivyo inaanzia Sh 1,400,000 na kuendelea.
Afisa Mauzo wa Bayport Financial Services, Catherine Tesha, akitoa maelekezo kwa baadhi ya wananchi waliokwenda Vikuruti, wilayani Kibaha, mkoani Pwani kujipatia fursa ya viwanja vinavyoratibiwa na Taasisi ya Kifedha ya Bayport Financial Services, mwishoni mwa wiki. Zoezi la viwanja hivyo kwa watumishi wa umma, wafanyakazi wa kampuni binafsi na wajasiriamali linaendelea hadi Juni 30 mwaka huu, ambapo kila Mtanzania anaweza kupata kiwanja hicho kwa fedha taslimu au kwa mkopo. Thamani ya viwanja hivyo inaanzia Sh 1,400,000 na kuendelea.

Thursday, June 11, 2015

Simba sasa yamkomoa Ramadhan Singano 'Messi'

Taarifa kwa vyombo vya habari.
Kikao cha kamati ya utendaji ya club ya simba kilichokutana jana tarehe 10/06/2015, pamoja na mambo mengine kilijadili suala la mchezaji wa Simba Ramadhan Yahya Singano pichani na kuamua yafuatayo:
Kwakuwa Mchezaji Ramadhan Yahya Singano alivunja makubaliano yaliyoamuliwa katika kikao cha pamoja kati ya club ya Simba, mchezaji mwenyewe, sputanza na secretarieti ya shirikisho la mpira wa miguu nchini(TFF) ya kutozungumzia yaliyojadiliwa na kupendekezwa kwenye kikao kwa kuyazungumza kwenye vyombo vya habari kwa kusema yeye ni mchezaji huru,

Klabu ya simba imeamua kutokufanya mazungumzo na mchezaji huyo kwa sasa kwa kuwa bado ina mkataba naye ambao utaisha 01/07/2016. Hata hivyo Klabu itakuwa tayari kufanya nae mazungumzo pindi muda muafaka utakapofika kwa mujibu wa kanuni na taratibu za mikataba.


Ni matarajio yetu mchezaji Singano ataheshimu maamuzi hayo na mkataba ambao pia upo TFF na kwenye mtandao TMS.
Imetolewa na Evans Aveva
Rais Simba Sports Club

Waziri Membe aibukia Zanzibar kufungua mkutano Mkuu wa nne wa Umoja wa kinamama wa Kikristo

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe akizungumza wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Nne wa Umoja wa Kinamama wa Kikristo (UMAKI) wa Kanisa Anglikana Dayosisi ya Zanzibar mjini Unguja jana. Kulia kwake ni Askofu Mkuu mstaafu wa Kanisa Anglikana.

Bayport yasogeza mbele ofa ya viwanja vya mikopo Vikuruti

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
TAASISI ya Kifedha ya Bayport Financial Services inayojihusisha na mambo ya mikopo imesogeza mbele huduma yao mpya ya mikopo ya viwanja vilivyopo Vikukuruti, wilayani Kibaha, mkoani Pwani kwa ajili ya kutoa fursa zaidi ya Watanzania kupata viwanja hivyo vilivyopimwa.

Meneja Masoko na Mawasiliano wa Taasisi ya Kifedha ya Bayport Financial Services, Ngula Cheyo, kushoto, akizungumza jambo baada ya kutangaza kusogeza mbele huduma ya mikopo ya viwanja vya Vikuruti, wilayani Kibaha, mkoani Pwani, ambapo sasa huduma hiyo imepelekwa mbele hadi Juni 30, mwaka huu. Picha na Mpiga Picha wetu.


Awali ofa ya huduma hiyo ilipangwa kumalizika Juni 10 mwaka huu, lakini sasa imepelekwa mbele hadi Juni 30, ikiwa ni ongezeko la siku 20 zaidi kama njia ya kuhakikisha kwamba wale wenye nia hiyo wanafanikisha ndoto zao za kumiliki viwanja.

Meneja Biashara wa Taasisi ya Kifedha ya Bayport Financial Services, Thabit Mndeme, kulia akizungumza jambo baada ya kutangaza kusogeza mbele huduma ya mikopo ya viwanja vya Vikuruti, wilayani Kibaha, mkoani Pwani, ambapo sasa huduma hiyo imepelekwa mbele hadi Juni 30, mwaka huu. Picha na Mpiga Picha wetu.


Akizungumza leo mchana jijini Dar es Salaam, Meneja Biashara wa Bayport Financial Services, Thabit Mndeme, alisema kwamba wamekuwa wakipokea maombi mengi kutoka kwa Watanzania wenye uhitaji wa viwanja hivyo, jambo lililowafanya wakae na kuona namna gani wataongeza siku chache kwa wananchi na wateja wao. Alisema kama ilivyokuwa mwanzo, wateja wao watalazimika kuchukua fomu za maombi ya mikopo ya viwanja hivyo katika ofisi yoyote ya Bayport, bila kusahau wakala wao ambayo ni tawi lolote la Bank of Africa (BOA), huku akitakiwa kulipa malipo ya awali kuanzia Sh 150,000.

“Kama ilivyokuwa mwanzo, mara baada ya mteja wetu kuchukua fomu na kulipa Sh 150,000 kwa kupitia benki ya BOA, ataleta nyaraka zake kwetu na atapatiwa kiwanja chake, huku gharama za kiwanja cha chini kabisa ni Sh 1,400,000, ambapo Bayport itamlipia gharama zilizosalia, huku akilazimika kulipia Sh 105,181 kwa mwezi kwa kipindi cha miezi 24,” alisema Mndeme.

Naye Meneja Masoko na Mawasiliano wa Bayport Financial Services, Ngula Cheyo, alisema kwamba huduma yao ni muhimu kwa watumishi wa umma, wafanyakazi wa kampuni binafsi na wajasiriamali ambao wote kwa pamoja wanachotakiwa kufanya ni kuchukua fomu na kuchagua viwanja watakavyo, kutoka kwenye mradi huo wenye viwanja 1878, huku pia mteja akiweza kupata kiwanja kwa fedha taslimu ya kuanzia Sh 1,400,000 na kuendelea.

152 kuburuzwa mahakamani kwa kujiandikisha mara mbili kwenye daftari la kudumu la wapiga kura

TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imesema watu 152 watafikishwa mahakamani mkoani Njombe kutokana na kujiandikisha mara mbili katika Daftari la Kudumu la Wapigakura kwa mfumo mpya wa ‘Biometric Voter Registration Kit’ (BVR).
Aidha, imeeleza kuwa kata 130 zimeongezeka kutokana na Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) kufanya mabadiliko ya kiutawala katika kata, vijiji,vitongoji na Mitaa hivyo kulazimu NEC kuhairisha kwa wiki moja uandikishaji wa daftari uliokuwa ukianza jana kwa baadhi ya mikoa. Kaimu Mkurugenzi wa Uchaguzi NEC, Dk Sisti Cariah alisema hayo jana wakati akielezea kuahirishwa kwa wiki moja uandikishaji hadi Juni 16 mwaka huu kwa mikoa ya Kilimanjaro, Arusha, Manyara na Mara.
Akizungumzia suala la watu kujiandikisha mara mbili, alisema katika mkoa wa Njombe ambao Daftari hilo liko tayari na wiki ijayo litawekwa wazi kwa siku tano na kisha kufanyiwa marekebisho kwa siku moja na wamebaini watu 152 waliojiandikisha mara mbili.
Alisema watu hao wametenda kosa la jinai na watashtakiwa, huku akitoa onyo kwa watu kuacha kufanya hivyo kwani mashine za BVR zinagundua wanaojiandikisha zaidi ya mara moja. Alisema wataweka wazi baadhi ya watu waliojiandikisha mara mbili kwenye mikoa yote, ambayo iko tayari.
Alisema mpaka sasa tayari wamepokea madaftari yaliyokamilika ya uandikishaji kwa mikoa ya Lindi, Mtwara na Ruvuma huku uandikishaji huo ukiwa umekamilika kwa asilimia 50 na wanatarajia kukamilisha uandikishaji mwezi Julai. Akizungumzia suala la mipaka ya kiutawala, yaliyofanywa na Tamisemi, Cariah alisema ilifanyika wiki mbili zilizopita katika mikoa mbalimbali, jambo lililosababisha kusitisha uandikishaji katika mikoa hiyo huku mikoa ambayo tayari uandikishaji umefanyika watarekebisha wakati wa kuweka wazi daftari.
“Katika kupiga kura lazima kitambulisho kioneshe kata anayokaa mtu kwa mabadiliko haya yamefanya kata kubadilika na kuongezeka 130 hivyo kufanya madiwani watakaopigiwa kura kuongezeka hivyo kata kuendana na kitambulisho,” alisema.

Wednesday, June 10, 2015

Viongozi wa dini Mtwara wambariki Bernard Membe kuwania urais



Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa na Mbunge wa Jimbo la Mtama, Bernard Membe akizungumza na viongozi wa dini ya kiislam wa Mtwara mjini jana jioni, wakati wa dua maalum iliyoandaliwa na viongozi hao kwa ajili ya kumtakia kheri katika safari yake ya kuwania urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika uchaguzi mkuu ujao kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM). Aliyekaa (kushoto) ni Sheikh wa Mkoa wa Mtwara, Dk. Nurdin Abdallah Mangochi. Picha zote na John Badi


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa na Mbunge wa Jimbo la Mtama, Bernard Membe (mwenye shati la kijani), akiagana na baadhi ya viongozi wa dini ya kiislam wa Mtwara mjini jana jioni, baada ya dua maalum iliyoandaliwa na viongozi hao kwa ajili ya kumtakia kheri katika safari yake ya kuwania urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika uchaguzi mkuu ujao kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Saturday, June 06, 2015

Angalia muonekanano mzuri wa mradi wa viwanja vya Bayport Financial Services, Vikuruti, wilayani Kibaha, mkoani Pwani

Huu ndio muonekano mzuri unavvyoonekana maeneo ya Vikuruti, wilayani Kibaha, mkoani Pwani kunapoendeshwa mradi wa viwanja vya mikopo kwa watumishi wa umma, wafanyakazi wa kampuni binafsi na wajasiriamali. Picha na Mpigapicha wetu.

Uhondo wa katuni, Tanzania mpya tutakula mihogo na viazi kwa hamu sio kwa shida

Kuelekea katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 na uhondo wa katuni zetu.

Kinana na msafara wake watoa kwenye msiba wa Jaji Luangisa

Katibu Mkuu wa CCM, Ndugu Abdulrahman Kinana akitia saini kwenye kitabu cha kumbukumbu ya maombolezo ya Marehemu Jaji Mstaafu Samuel Luangisa nyumbani kwake kwa marehemu Kitendagulo, mjini Bukoba mkoani Kagera. Marehemu Luangisa ni miongoni  mwa Waasisi wa Taifa na katika vipindi tofauti tofauti alikuwa mkuu wa Mkoa wa Ziwa Magharibi (Kagera), Mbunge na Meya wa Manispaa ya Bukoba pamoja na nyadhifa nyingine.
Katibu Mkuu wa CCM,Ndugu Abdulrahman Kinana akiweka shada la maua kwenye kaburi la Marehemu Jaji Mstaafu Samuel Luangisa mapema leo asubuhi nyumbani kwake kwa Kitendagulo, mjini Bukoba mkoani Kagera.

Friday, June 05, 2015

Ziara ya Kinana ya kuelekea Bukoba kwa kutumia basi haijawahi kutokea

KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndugu Abdulrahman Kinana akipokewa na Kamati ya Ulinzi na Usalama usiku wa jana ndani ya wilaya Kahama mkoani Shinyanga tayari kwa mapumziko, ambapo leo ameianza rasmi ziara yake katika kijiji cha Nyakanazi wilaya ya Biharamulo mkoani Kagera, Ndugu Kinana ndani ya Biharamulo atapokea taarifa za chama na Serikali na baadae kuzungumza na Wafugaji wa kanda ya Ziwa (Mikoa ya Geita, Kagera, Mwana na Shinyanga)  na baadae kueleke Bukoba mjini.

Ndugu Kinana amewasili wilayani humo akielekea mkoani Kagera kwa basi maalum katika ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezwaji wa ilani ya uchaguzi ya CCM mwaka 2010 na kuimarisha uhai wa chama,akiwa ameambatana na Katibu wa NEC Itikadi na Uenezi Nape Nnauye na baadhi ya Maofisa wa chama. 
 KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana akipokelewa na Mbunge wa jimbo la Nzega usiku huu Dkt.Hamis Kingwangalla, mara baada ya kuwasili wilayani humo akielekea mkoani Kagera kwa basi maalum katika ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezwaji wa ilani ya uchaguzi ya CCM mwaka 2010 na kuimarisha chama. Ndugu Kinana ameambatana na Katibu wa NEC Itikadi na Uenezi Nape Nnauye na baadhi ya Maofisa wa chama. 
  KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana akipokelewa na baadhi ya viongozi wa chama hicho usiku wa jana wilayani Nzega mkoani Tabora akielekea mkoani Kagera kwa basi maalum katika ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezwaji wa ilani ya uchaguzi ya CCM mwaka 2010 na kuimarisha chama.Ndugu Kinana ameambatana na Katibu wa NEC Itikadi na Uenezi Nape Nnauye na baadhi ya Maofisa wa chama. 

Watanzania wavichangamkia viwanja vya Bayport Vikuruti, wilayani Kibaha, mkoani Pwani


Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
WATANZANIA wameendelea kuvichangamkia viwanja vya mkopo vinavyotolewa na Taasisi ya Kifedha ya Bayport Financial Services, vilivyopo Vikuruti, wilayani Kibaha, mkoani Pwani.
 Hawa ni miongoni mwa Watanzania waliohamasika kutembelea katika viwanja vilivyokuwa kwenye mradi wa Vikuruti kutoka Taasisi ya Kifedha ya Bayport Financial Services, wilayani Kibaha, mkoani Pwani, ambavyo vinatolewa kwa wananchi kwa mkopo. Wakopaji ni watumishi wa umma, kampuni binafsi na wajasiriamali.
Eneo la viwanja vya Vikuruti vinavyoonekana huku barabara ikionekana pichani.
Kuchangamkiwa kwa viwanja hivyo kumekuja siku chache baada ya kuzindua huduma mpya ya mikopo ya viwanja hivyo kutoka Bayport, ikiwa ni ishara nzuri na njia ya kuwapa fursa Watanzania ya kumiliki nyumba.

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, Meneja Masoko na Mawasiliano wa Bayport Financial Services, Ngula Cheyo, alisema watu wengi wamekuwa wakituma maombi ya kuomba kupewa viwanja hivyo, tangu huduma hiyo ilipozinduliwa rasmi.

Alisema kwamba baadhi ya watu walioonyesha nia ya kuvipata viwanja hivyo pamoja na kutuma maombi yao, pia wamekuwa wakitembelea eneo kulipokuwa na viwanja hivyo ili wajiridhishe kwa ajili ya kujipatia viwanja hivyo vinavyokopeshwa kwa minajiri ya kuwakwamua Watanzania, ukizingatia kuwa ardhi inapanda thamani siku hadi siku.

“Jana (juzi) zaidi ya watu 82 wamekwenda Vikuruti, Kibaha kujionea eneo lenyewe na kuchagua viwanja wapendavyo, ikiwa ni mwendelezo mkubwa wa wananchi wanaotuma maombi ya kukopa viwanja vya Bayport, wakichukua fomu bure z  kwa kupitia matawi yetu yaliyoenea nchi nzima, bila kusahau kwenye matawi ya Bank of Afrika (BOA).

“Huduma hii ni murua kwa Watanzania wote, tukiamini kuwa ni sehemu ya kuwapatia wananchi urahisi wa kumiliki vitu vyenye thamani ikiwamo ardhi wanayoweza kuitumia kwa mambo mengi, ikiwa nyumba za kuishi na za biashara, huku thamani ya viwanja vikianzia Sh 1,400,000 na kuendelea kwa viwanja vyenye ukubwa tofauti vya kujenga nyumba za kuishi na biashara kama vile shule, vituo vya afya, nyumba za kulala wageni na hoteli,” alisema Cheyo.

Wednesday, June 03, 2015

Profesa Muhongo: Mwenye uwezo wa kuikwamua Tanzania ni mimi

* Atangaza nia kwa kutoa takwimu za umasikini na utajiri
*Asema viwanda, gesi, umeme utaipaisha Tanzania


Na Mwandishi Wetu, Musoma
WAZIRI wa zamani wa Nishati na Madini Sospeter Muhongo, ametangaza nia rasmi ya kuwaomba Wana CCM kumteua kuwania urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwezi Oktoba, huku akisema ni yeye pekee mwenye uwezo wa kuikwamua nchi katika hali mbaya ya umasikini na ukosefu wa wataalamu, hali inayoifanya nchi ishindwe kupiga hatua.


Profesa Sospeter Muhongo, pichani.
Pamoja na mambo mengine, Muhongo alitumia muda mwingi kutoa takwimu hali ya umasikini na utajiri kwa wananchi wa Tanzania, bila kusahau baadhi ya nchi ambazo zimeweza kupiga hatua kubwa kwa kujikita kwenye kuzalisha wataalamu na watafiti, akiwamo yeye, ambaye si tu ni Profesa, bali pia amebobea kwenye nishati kwa miaka mingi.


Akizungumza kwa kujiamini mbele ya wanachama wa CCM na Watanzania katika Ukumbi wa Chuo Kikuu Huria, Musoma Mjini jana, Profesa Muhongo alisema kwamba anayo tiba ya umasikini wa Watanzania kwa kuhakikisha kwamba anatumia utaalamu wake kwa kusimamia mambo ya gesi, mafuta, umeme, bila kusahau elimu kwa ajili ya kuwakwamua wananchi wake.


“Nchi ina upungufu mkubwa wa takwimu hali inayowafanya viongozi washindwe kujua namna gani wanaweza kuondoa umasikini na kero zinazowakumba wananchi wake, hivyo hata wale wanaosema wanataka uongozi, hawajui wangapi wenye uhitaji.


“Ukiacha takwimu ambayo kwa Dunia ya sasa ni lazima, nchi yetu lazima ijiamini, kuongeza ushindani, kuongeza upendo, bila kusahau rushwa ambayo kwa uhakika inapaswa kupigwa vita kwa vitendo ili nchi yetu isonge mbele,” alisema Muhongo.


Kuhusu uchumi, Profesa Muhongo alisema kwamba ni aibu Tanzania kupitwa kiuchumi na Mataifa waliyokuwa nayo sawa, akitolea mfano wan chi za Brazil, China, India na Kenya ambao wao wamewekeza kwa kiasi kikubwa kwenye elimu na utafiti.

Tuesday, June 02, 2015

SIWEZI KUVUMILIA: Kwa ubabaishaji wetu, hakuna kocha mzuri ndani ya Simba na Yanga

Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
WENYEWE wanaziita Kulwa na Dotto. Eti Yanga ni Kulwa na Simba ni Dotto. Kama majina haya hayaendani nao, basi yanakaribia kabisa na tafsiri ya majina yao haya.


Wanafanana mizengwe na ubabaishaji. Hata migogoro pia hurithishana, ukitoka Simba, utahamia Yanga. Klabu mbili hizi ambazo ni kongwe, hazijawahi kukaa miaka mitatu mfululizo bila migogoro.  Na kwa miaka ya karibuni, wamezidi.


Mbali na migogoro hiyo, klabu hizi zimekuwa na kawaida ya kubadilisha makocha kama nguo za ndani. Labda wanatafuta kocha mwenye mafanikio zaidi ya Sir Alex Ferguson, aliyewahi kuwa kocha wa timu ya Manchester United ya nchini Uingereza.


Kama huo ndio mtazamo wao, basi wanajidanganya. Wanajipotezea muda,  maana ndani ya timu hizi kongwe hakuna kocha mzuri. Hata akiwa mzuri, ataharibiwa na mizengwe yao.
Hadi leo hawaheshimu makocha wao.  Mwenyekiti au kiongozi wa klabu anaingilia upangaji wa timu bila kuona athari zinazoweza kujitokeza kwenye klabu yao.


Na ikitokea timu inafungwa, wanajaribu kuwasumbua wataalamu hao ambao wengi wao wamekuwa wakiishi kwa kubangaiza wasiojua kesho yao itakuwaje.

Profesa Muhongo kutangaza nia ya Urais leo Musoma Mjini, Ukumbi wa Open University Hall


Leo ni zamu ya Profesa Sospeter Muhongo kutangaza nia ya kuombwa kugombea urais wa Jamahuri ya Muungano wa Tanzania, kurithi mikoba ya Rais Jakaya Mrisho Kikwete. Profesa Muhongo anatangaza nia yake leo Mjini Musoma, kwenye Ukumbi wa Open University Hall, kuanzia saa 10 jioni.

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...