https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Saturday, February 28, 2015

John Komba afariki Dunia TMJ leo Dar es Salaam

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
KIFO. Mbunge wa Mbinga Magharibi, Kapteni Mstaafu, John Komba, pichani, amefariki Dunia leo jioni katika Hospitali ya TMJ, sasa mwili wake umehifadhiwa katika Hospitali ya jeshi la Lugalo. Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, alithibitisha kutokea kwa kifo hicho.
Marehemu Komba ambaye pia ni Mkurugenzi wa bendi ya TOT inayomilikiwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM), amerafiki huku akiwa anategemewa kwa kiasi kikubwa katika suala zima la Uchaguzi Mkuu mwaka 2015.

Tayari Komba aliachia wimbo wake mpya uliokwenda kwa jina la CCM mbele kwa mbele, aliyouimba rasmi katika sherehe za kuzaliwa kwa CCM, zilizofanyika Songea mjini. Habari za kufariki kwa Komba zimepokewa kwa shingo upande na wadau wa CCM na Watanzania kwa ujumla.

Komba atakumbukwa kwa mchango wake mkubwa kwenye chama hicho cha CCM kutokana na uwezo wake wa kutunga nyimbo za kampeni mara kwa mara ambapo nyimbo zake zimekuwa tegemeo kwa watu wote wanaofuatilia na wasiofuatilia siasa za Tanzania.

Bayport yasononeshwa na mauaji ya albino, yaungana na mbunge Shaimar Kweigyir kutoa pole Mwanza

Meneja Mauzo wa Taasisi ya Kifedha ya Bayport Financial Services Kanda ya Ziwa, Lugaano Kasambala, akimpa pole Ester Jonas, mama wa Yohana Bahati, mtoto mwenye ulemavu wa ngozi albino, aliuawa mkoani Mwanza, hivi karibuni. Mama huyo anatibiwa katika Hospitali ya Bugando baada ya kupata mareraha katika tukio la kuvamiwa na kuporwa mtoto wake. Kulia kwa Kasambala ni Mbunge wa Viti Maalum, Al Shaimar Kweigyir mwenye miwani waliyeambatana katika safari hiyo kwa ajili ya kuwapa pole na kuwafariji.

Na Mwandishi Wetu, Mwanza
MBUNGE wa Viti Maalum, Al Shaimar Kweigyir kwa ushirikiano na Taasisi ya Kifedha, inayojihusisha na mikopo ya Bayport Financial Services yenye Makao yake Makuu jijini Dar es Salaam, Tanzania, walifanya ziara ya siku mbili jijini Mwanza kwa ajili ya kutembelea familia mbili zilizopoteza watoto wao wawili ambao ni walemavu wa ngozi.

Familia hizo ni ya Ester Jonas, mama wa marehemu Yohana Bahati na ile ya Sofia Juma mama wa mtoto Pendo Emmanuel, wote wakiwa ni watu wenye ulemavu wa ngozi, huku familia zote mbili zikipewa Sh Milioni 2 kila moja.
Mbunge wa Viti Maalum, Al Shaimar Kweigyir mwenye miwani akimfariji mama wa Yohana Bahati (Ester Jonas) aliyelazwa Hospitali ya Bugando, Mwanza, pamoja na kumpaa mafuta ya kupaka kwa ajili ya watoto wake wawili ambao nao ni albino,. Kushoto kwa Mh Shaimar ni Meneja Mauzo wa Bayport Financial Services Kanda ya Ziwa, Lugano Kasambala na wafanyakazi wengine wa Bayport waliombatana pamoja kwenye msafara huo wa kutoa pole.

Akizungumza katika safari hiyo, Mbunge Shaimar alisema ameendelea kusikitishwa na mauaji hayo ya albino yanayotoa haki ya kuishi ya watu wote wenye ulemavu wa ngozi, huku akiitaka jamii kuacha kufavya vitendo hivyo visivyokuwa vya kiungwana kutokana na kudhulumu haki za kuishi za binadamu wenzao.
 
“Naumia juu ya vitendo hivi kwasababu na mimi nipo kwenye kundi hili lawatu wenye ulemavu wa ngozi wanaoendelea kupukutika siku hadi siku, hivyo tupambane na majangili haya, maana najua Mheshimiwa Rais, Dr Jakaya Kikwete na Waziri Mkuu Mizengo Pinda wamekuwa wakiguswaa mno na matukio haya yanayoichafua nchi yetu,' alisema Shaimar, ambapo pia aliishukuru Bayport Financial Services kuingia katika harakati za kupambana na mauaji ya albino nchini Tanzania.

Friday, February 27, 2015

Uandikishaji wa wapiga kura Biometrick Voters Registration (BVR) Makambako wapongezwa

Kazi ya kuandikisha wananchi katika Daftari la Kudumu la Wapigakura kupitia mfumo wa Biometrick Voters Registration (BVR), ambao huhusisha uchukuaji wa alama za vidole na picha, jana iliingia siku ya tatu, huku baadhi yao wakipongeza utendaji wake.
Kwa mujibu wa ripoti iliyokusanywa na mwandishi wetu inasema kuwa tokea siku ya kwanza lilipoanza zoezi hilo lilionyesha matumaini maana wananchi wetu walijitokeza kwa wingi.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti wananchi katika vituo vya uandikishaji, wananchi hao walisema kuna mabadiliko ukilinganisha na siku zilizopita, hivi sasa kazi zinafanywa haraka.
“Watu wanaokwenda kwenye vituo kujiandikisha idadi yao ni kubwa kuliko hata makadirio ya tume, kama hawataongeza muda au vifaa, siku saba walizopanga, hazitatosha na wengi wataachwa bila ya kujiandikisha,” alisema.
Baadhi ya waandikishaji na wasimamizi wa mashine wameiomba Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) kuongeza muda ili kazi hiyo ifanyike kwa ufanisi zaidi.

Mbunge wa kuteuliwa Shaimar Kweigyir amtembelea majeruhi wa Albino Hospitali ya Bugando Mwanza

Na Mwandishi Wetu, Mwanza
Mbunge wa kuteuliwa, Al Shaimar Kweigyir, amtembelea majeruhi wa tukio la uporwaji wa mtoto mwenye ulemavu wa ngozi albino,Yohana Bahati, aliyetekwa nyara na kukutwa akiwa amekufa.

Katika ziaraa hiyo kwenye Hospitali ya Bugando jijini Mwanza, Mh Shaimar aliongozana pia na Katibu Tawala Msaidizi wa Ofisi ya Mkoa wa Mwanza, Crencencia Joseph na August Tesha, ambaye ni Meneja wa Bayport Financial Services mkoani Mwanza.
Wakiwa Hospitali ya Bugando, Mbunge Shaimar na alioambatana nao alipata fursa ya kuzungumza na wahudumu katika wodi aliyolazwa Ersther ambaye ni wa Yohana na kumfariji katika kipindi kigumu cha kuuguza majeraha yake pamoja na kulia msiba wa mwanae.

Tukio la utekaji na uporwaji wa watu wenye ulemavu wa ngozi limezidi kushika kasi, ambapo kumekuwa na malalamiko mengi kutoka kwa wadau, hususan wale wenye ulemavu wa ngozi wakiamini kuwa serikali imeshindwa kuwapatia ulinzi wa kutosha.

Akiwa jijini Mwanza, Mbunge Shaimar na taasisi ya kifedha ya Bayport Financial Services watakuwa kwenye safari ya kuelekea wilayani Kwimba kwa ajili ya kwenda eneo alilokuwa akiishi Ester na watoto wake, hususan wawili kati ya watano waliobaki wakiwa ni albino.
Mbunge wa kuteuliwa Shaimar Kweigyir katikati akiwa na bibi wa Yohana Bahati (Tabu Maganiko) kulia ambaye ni mlemavu wa ngozi aliyeuawa hivi karibuni mkoani Mwanza, huku mama yake akiachwa na majeraha makubwa wakati wanagombania mtoto katika tukio hilo la kusikitisha. Kushoto kwake ni Mweka Hazina wa Chama Cha Albino Tanzania Abdullah Omari.
Katibu wa Mheshimiwa mbunge, Semeni Kingalu, kulia akipiga picha wakati walipomtembelea majeruhi Ester Maganiko, ambaye mtoto wake Yohana Bahati mwenye ulemavu wa ngozi aliuliwa katika tukio hilo la kusikitisha. Anayefuata ni Muuguzi wa zamu wa Hospitali ya Bugando na Clencencia Joseph, Katibu Tawala Msaidizi Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Mwanza.

Sunday, February 22, 2015

Mchezaji wa zamani wa Simba, Christopher Alex afariki Dunia mjini Dodoma

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
MCHEZAJI wa zamani wa Simba SC, Christopher Alex, amefariki Dunia mkoani Dodoma, baada ya kuugua kwa muda mrefu. Mchezaji huyo anayekumbukwa kutokana na uwezo wake uwanjani, amefariki ikiwa ni baada ya kuteseka kwa muda mrefu.

Marehemu Christopher Alex, enzi za uhai wake.
Mapema mwaka huu Alex alisikika katika kituo cha redip cha Uhuru FM, akilalamika jinsi viongozi wa soka wa Simba walivyoweza kumtupa kiasi cha kushindwa hata kumjulia hali, licha ya kuichezea timu hiyo kwa moyo wote.

Katika malalamiko yake hayo, alitumia muda mwingi kumuomba pia nahodha wake wa zamani, Selemani Matola, akiamini kuwa alikuwa na uwezo wa kufuatilia suala hilo kwa viongozi wake hao wa zamani wa klabu ya Simba.

Alex ni moja ya wachezaji mahiri wa klabu ya Simba walioitumikia klabu hiyo kwa moyo na mafanikio makubwa. Akiwa uwanjani mwaka 2002, Alexa na wenzake walaifanikiwa kufuzu robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika kwa kuwaondosha vigogo wa Afrika, tmu ya Zamalek na kuzua  shangwe Tanzania na kwa nchi zote za Afrika Mashariki na Kati.

Friday, February 20, 2015

Mradi wa NewsRadar wa ukusanyaji wa taarifa za kibiashara wazinduliwa jijini Dar es Salaam

Mshauri mkuu wa mradi wa NewsRadar, Romana Gersuni kutoka Ujerumani akielezea jinsi teknolojia hiyo mpya na ya kisasa ya ukusanyaji taarifa mbalimbali ya Push Observer inavyofanyakazi zake.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
Sekta zote Nchini sasa zinaweza kupata taarifa mbali mbali zilizorushwa kwene vyombo vya habari kupitia teknolojia mpya ya usambazaji taarifa ijulikanayo kwa jina la NewsRadar ya kampuni ya Push Observer.

Push Observer Limited ni kampuni ya Tanzania inayomiliki vyombo vya kiinteligencia na teknolojia ya sanaa ya kufuatilia, kukamata na kuchuja vyombo vya habari - magazeti, matangazo (radio & televisheni), Internet na uchambuzi, ripoti ya ushindani kwa ajili ya biashara, serikali na wateja wengineo wa mashirika yasiyo ya kiserikali.

Mkuu wa mikakati wa kampuni ya Six Telecoms ambayo ni kampuni mama ya Push Observer, Rashid Shamte akielezea faida ambazo watazipata kampuni mbalimbali nchini, husasani za kibiashara kwa kujiunga na huduma ya NewsRadar waliyoianzisha nchii.

Msanii Mez B afariki Dunia mjini Dodoma alipokuwa akiugua

HABARI ambazo hazijathibitishwa rasmi na familia, zinasema kuwa mwimbaji wa muziki wa kizazi kipya, Mez B, amefariki Dunia mjini Morogoro baada ya kusumbuliwa na maradhi. Taarifa za kifo cha msanii zimetufikia hivi punde baada ya kufariki. Kifo cha msanii huyo ni pigo katika tasnia ya muziki wa kizazi kipya.
 
Mwimbaji wa Bongo Fleva, Mez B, enzi za uhai wake.
Mez aliwahi kutamba na nyimbo kadhaa kama ule wa Nimekubali, ambao alipoutoa ulifanya vizuri, bila kusahau nyimbo yake ya kwanza iliyokwenda kwa jina la Kikuku, ambao uliweza kumtambulisha katika tasnia hiyo.

Taarifa zaidi za msiba huo zitaendelea kukujia baada ya kuzungumza na wadau mbalimbali, bila kusahau familia yake na kuelezea pia taratibu zote za msiba huo.

Joseph Kusaga: Habari za kuuzwa Clouds Media Group ni uzushi wa kupuuzwa

Mkurugenzi Mtendaji wa Clouds Media Group, inayomiliki redio ya Clouds Fm, Clouds Tv na Choice FM, Joseph Kusaga, pichani katika moja ya matukio ya kikazi. Leo Kusaga alizungumzia habari za kuuzwa kwa kampuni yao na kusema si kweli.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
TAHARUKI iliyosambaa jana kwenye mitandao kijamii juu ya kuuzwa kwa Clouds Media Group, inayomiliki Clouds FM, Clouds Tv na Choice FM, zimepata majibu baada ya Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni hiyo, Joseph Kusaga, kuibuka na kukataa habari hizo na kuziita ni uzushi wa kupuuzwa.


Habari za kuuzwa kwa kampuni hiyo dhidi ya mfanyabiashara maarufu na kada wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Rostam Aziz, zilishika nafasi katika mitandao ya kijamii na hatimae kuzua usumbufu mkubwa kwa wafanyakazi, viongozi wa Clouds na Watanzania kwa ujumla.

Akizungumza leo asubuhi moja kwa moja katika kituo cha Radio cha Clouds FM, Kusaga alisema habari hiyo imetengenezwa na watu walioamua kupoteza muda wao katika mitandao ya kijamii, hali ya kuwa wapo wanaovuna fedha nyingi kwa kupitia njia hiyo ya mawasiliano (social media).

Alisema mara baada ya kuenea kwa habari hiyo, usumbufu mkubwa uliibuka kutokana na watu wenye mapenzi mema na kampuni hiyo kuanza kuhoji juu ya taarifa hizo kama zina ukweli, huku akisisitiza pia si kosa kuuza kwa kuwa ni jambo la kawaida katika mambo ya kibiashara.

“Clouds Media Group ni kampuni iliyoanzia chini kwa ushirikiano wa watu wengi, hivyo kuamua kuiuza kiholela ni jambo la kushangaza, ingawa pia si dhambi kufanya hivyo kwa mtu yoyote kwa sababu ni biashara kama zilivyokuwa biashara nyinginge.

Wednesday, February 18, 2015

Fahamu majina ya vijiji vyote 112 vya wilaya ya Handeni, mkoani Tanga

Na Kambi Mbwana, Aliyekuwa Handeni
HANDENI ni wilaya kongwe inayounganisha Mkoa wa Tanga. Uwepo wa wilaya hii umesababisha kuzaliwa kwa wilaya nyingine ya Kilindi. Licha ya kugawanywa na serikali bado Handeni inaendelea kuwa wilaya kongwe na kubwa.
Mkuu wa wilaya Handeni, Muhingo Rweyemamu, pichani
Handeni ni kati ya wilaya saba za Mkoa wa Tanga katika Tanzania. Imepakana na Wilaya ya Kilindi upande wa magharibi, Wilaya ya Korogwe na Mkoa wa Kilimanjaro upande wa kaskazini, Wilaya ya Pangani upande wa mashariki na Mkoa wa Pwani kwa kusini.

Kulingana na sensa ya watu na makazi ya Mwaka 2002 Wilaya ilikuwa na watu 248,633 kwa kiwango cha ukuaji wa asilimia 3.3% katika kaya 52,240 ambayo ni sawa na wastani wa watu 4.66 kwa kaya. Wastani wa msongamano wa watu ni watu 30 kwa kilometa ya mraba.

Msongamano mkubwa upo kando kando ya barabara kuu na mijini. Idadi ya watu huongezeka kwa wastani wa asilimia 3.3% kwa mwaka, kwahiyo idadi ya watu mwaka 2010 ilikadiriwa kuwa 322,375 na mwaka 2013 ilikadiriwa kuwa na watu 355,355.

Juhudi nyingine zinafanyika kuigawa tena wilaya hii sambamba na kufanikisha kuifanya kuwa mkoa mpya, ukitoa wilaya za Kilindi, Korogwe na ile Halmashauri ya Kabuku ambapo juhudi na maarifa zinaelekezwa huko.

Ni vyema sasa mkakati huo ukawa kijiji kwa kijiji, kata kwa kata, tarafa kwa tarafa na wilaya yote ya Handeni, ili kuleta dira mpya kimaendeleo. Tarafa hizo ni pamoja na Kwamsisi, Mkumburu, Mzundu, Sindeni, Mazingara, Magamba na Chanika, wakati kata ni pamoja na Vibaoni, Kideleko, Chanika, Kwankonje, Kwachaga, Kwaluguru, Kang'ata, Mkata, Mazingara, Kiva, Kwamatuku, Misima, Sindeni, Kabuku, Kabuku ndani, Komkonga, Ndolwa, Mgambo, Segera, Kwedizinga, Kwamgwe, Kwamsisi na Kwasunga.

Vijiji vinavyopatikana katika wilaya ya Handeni ni pamoja na
Kwabaya, Konje , Konje, Kwamasaka na Vibaoni, Msasa, Kideleko, Bangu, Kwamngumi, Kwakivesa, Mdoe, Malezi, Kwenjugo, Mashariki, Kilimilang'ombe,

Kwenjugo magharibi, Kwediyamba, Kwedizando, Kwenkambala, Nkumba, Kwamsundi, Kwamsangazi, Kwankonje, Kwamkunga, Kwachaga, Mkomba, Tuliani, Mpalagwe,
Magamba, Kibindu, Muungano B, Kwamagome, Msaje, Kwaluwala, Madebe, Nyasa, Gole, Kang'ata, Kilimamzinga, Manga.

Vingine ni Kwenkwale, Kwang'ahu, Kitumbi, Mkata Mashariki, Mkata Magharibi,  Suwa, Amani, Mazingara, Kweditilibe, Kwedibangala, Zavuza,  Kweingoma, Komsala, Nkale, Kwamatuku, Mzeri, Misima, Kibaya, Mbagwi, Msomela, Sindeni, Kweisasu, Kwamkono, Komfungo, Mbuyuni, Bongi, Kabuku Kaskazini, Kabuku Nje, Kwedibago.

Vijiji vingine ni pamoja na Msilwa, Kwedikwazu Mashariki, Kwedikwazu Magharibi,  Kabuku Ndani, Majani Mapana, Kabuku Mjini, Chogo, Komkonga, Kwamachalima, Hoza, Mumbwi, Tuliani/Kabuku,  Kwamnele, Chanika Kofi, Komkole 'B", Luiye, Kwamwenda, Komdudu Mzundu, Seza Kofi, Gendagenda, Kwedihwahwala, Komsanga, Kwabojo,  Jitengeni, Mandera, Masatu, Mailikumi, Segera, Chang'ombe, Michungwani,  Taula,  Kwedizinga, Ugweno, Bondo,  Kwamgwe, Kwadoya, Ngojoro, Mkalamo, Pozo, Kwedikabu, Kwamsisi,  Kwandugwa, Kwasunga, Kwanyanje na vinginevyo,

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...