https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Monday, March 11, 2013

Tujiangalie, tusitwange maji kwenye kinu



SIWEZI KUVUMILIA
Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden Rage
 
Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
SIKU zote ni aghalabu sana mtu anayetangwa maji kwenye kinu akapata faida, kama anavyokusudia, zaidi ya hapo; ataambulia kulowana kwenye kifua chake kwa kazi anayoifanya.

Kwa mtindo huu, kuna wajibu wa kuwazindua wale wenzetu wanaofanya vitendo hivyo kujiangalia upya, maana daima kazi hiyo haina malipo, isipokuwa kujisumbua.


Ndivyo ninavyoweza kusema katika makala haya ya Siwezi Kuvumilia, kwa kuona kuwa wapo wadau wasiokuwa na malengo sahihi ya kuokoa michezo, ukiwamo mpira wa miguu.

Huu ndio ukweli, maana wengi wao wanaangalia faida yao katika sekta husika. Mtu yupo tayari kukanyaga baadhi ya kanuni kwa ajili ya kujiweka katika nafasi ya mafanikio yake.

Angalia, licha ya kuwa na wataalamu wengi kwenye Shirikisho la Soka nchini (TFF), lakini ligi yetu ni mbaya haina mvuto. Hayo yanasababishwa na mbinu zetu kuegemea sana kwenye kipato cha wachache kuliko wengi.

Dunia nzima wanaelewa kuwa mpira wa miguu kazi inayolipa fedha nyingi, hivyo kama sisi Watanzania mipango yetu si endelevu, ni waganga njaa, hakika matamshi yetu ni kama kutwanga maji kwenye kinu.

Huo ndio ukweli wa mambo. Utakuta watu licha ya kujigamba kuwa wana uchungu na michezo hasa mpira wa miguu, lakini ameshindwa kabisa kuwa malengo ya kuendeleza vijana.

Mtu anao mtaji kabisa wa kumuwezesha kufanya hivyo, lakini amefumba macho na kushuhudia nguvu kazi, vipaji vingi vikikimbilia kulima, kukata mkaa na kugombana na maliasili kila siku, hali ya kuwa wangekuwa matajiri wakubwa kama wangesimamiwa kwenye michezo.

Matatizo kama hayo yapo vijijini. Siwezi Kuvumilia imekuwa ikipokea simu nyingi kutoka kwa vijana wadogo, kila mmoja akionyesha shauku ya kutaka kuonyesha uwezo wake, lakini wadau wenyewe wamefumba macho.

Nimekuwa nikilizungumzia hili kila siku kuwa, hata wabunge wetu, wanaweza kuendeleza vijana kwa kuwaanzishia mashindano japo ya mwaka mara mbili, kama njia ya kuwapatia mwanga wapiga kura wao.

Jimbo moja likiwa na msisimko kwenye michezo, ina maana vijana wanajiweka katika nafasi nzuri, ukizingatia kuwa tayari wana nafasi ya kuonyesa cheche zao, hivyo hili haliwezi kufumbiwa macho.

Hakika siwezi kuvumilia, hasa kwa kuona bado sisi ni watu wa kupiga porojo, kuhubiri siasa, kwa namna moja ama nyingine, hali ya kuwa vijana wetu, wanaashia kuwa mashabiki.

Mapema wiki iliyopita nilizungumza na Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka nchini (TFF), Boniface Wambura, ambapo yeye katika malalamiko yake, yaliegemea kwa wachezaji kuwa licha ya kuwa na vipaji lakini hawajitambui.

Haya ni maneno kutoka kwa Wambura, ingawa binafsi naona vipaji vingi vipo vijijini vinazagaa kwenye vibanda vya pombe kali, maana hata hiyo nafasi ya kuonyesha vipaji vyao hawana.

Ndio hapo TFF inapotakiwa kusimama kidete kuwakumbusha vyama vya wilaya, kuanzisha ligi zenye mashiko au mashindano yenye mguso kwa ajili ya kuendeleza vipaji vya vijana.

Kinyume cha hapo, juhudi zetu ni kazi bure. Hatutaweza kuwa na wachezaji wenye nguvu na mtazamo wa kimaendeleo, ukizingatia kuwa ligi zetu, hazina mvuto na tunahubiri uzandiki.

Naamini tukifanya hivyo, hakika mbinu zetu zitakuwa na mashiko, huku tukiwa na wachezaji wazuri na wenye mvuto wa kusaka nafasi ya kushiriki ligi zenye nguvu duniani kwa kusajiliwa huko.

Kinyume cha hapo, Tanzania haitakuwa na mbinu za kujiletea mafanikio Kimataifa, maana kila mtu ni mwanasiasa na hakuna mtendaji kwa kuangalia mfumo mzima ulioozeshwa na viongozi mbalimbali, wakiwamo wa TFF, ambao suala la Uchaguzi tu linawayumbisha kwa kufanya fitina za kuwabana au kuwabeba wachache wao.

Hakika siwezi kuvumilia, maana tunatwanga maji kwenye kinu.
0712 053949
0753 806087

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...