https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Sunday, March 10, 2013

Simba kuvuna nini kwa Coastal Union leo Taifa?


Mlinda mlango wa Simba, Juma Kaseja.

Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
MABINGWA watetezi, Simba SC, leo wana kibarua kigumu cha kuhakikisha kuwa wanatoka na ushindi wa pointi tatu muhimu katika mechi yao itakayopigwa katika Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam, dhidi ya timu ya Coastal Union, kutoka Tanga kwa Wagosi wa Kaya.


Mechi hiyo inasubiriwa kwa hamu na mashabiki wa soka wa Tanzania, huku upande wa Yanga na Azam FC, wakiombea Simba iendelee kupoteza mechi hiyo ili ipotee katika mbio za kuwania ubingwa huo.

Simba wanaingia uwanjani kumenyana na Coastal Union, huku zote zikiwa na pointi 31, sawa na timu ya Mtibwa Sugar ya Turiani mjini Morogoro, hivyo ina kila sababu ya kushinda ili ijiweke kwenye nafasi nzuri ya kuendelea kuwa na matumaini ya kutetea ubingwa wake.

Timu yoyote itakayoibuka na ushindi leo, itafikisha pointi 34 na kushika nafasi ya tatu, jambo linaloongeza ushindani katika mchezo huo ambao kila moja inataka ishinde na kuwafurahisha mashabiki wake.

Hata hivyo, licha ya timu hizo kudaiwa kuwa na undugu japo kwa kiasi kidogo, lakini zote zimepania kushinda, huku joto kwa upande wa Simba likiwa juu zaidi kutokana na matokeo ya migogoro inayoendelea kuwatafuna.

Juzi jioni, Malkia wa Nyuki, aliyepewa nafasi ya Mwenyekiti wa Kamati ya Ushindi, Rahma Al Kharoos, alitembelea katika tawi la Mpira Pesa, akihitaji ushirikiano na kuvunja makundi ndani ya Simba kwa ajili ya kuiwezesha kushinda katika kila mchezo unaokuja mbele yao.

Hata hivyo, ujio wa mwanamama huyo unakuja huku Makamu Mwenyekiti wa Simba, Geoffrey Kaburu kuachia ngazi, ikiwa ni uamuzi uliochukuliwa pia na Mjumbe wake Zacharia Hans Pope.

Kocha Mkuu wa Simba, Patrick Liewing, yeye ana kila sababu ya kuona timu yake inaibuka na ushindi, ili kulinda kibarua chake, ukizingatia kuwa baadhi ya watu wameanza kuhoji uhalali wa kibarua chake ndani ya Simba.

Mechi hiyo ambayo kwa upande wa Coastal inafundishwa na kocha wake, Ahmed Morocco, itachezeshwa na Martin Saanya akisaidiwa na Jesse Erasmo na Vicent Mlabu wote kutoka mkoani Morogoro.

Timu zote zimepania vilivyo kuibua na ushindi katika mchezo huo, akiwamo kocha msaidizi wa Simba, Jamhuri Kihwelo Julio na bosi wake, Liewing, waliyetangaza hatari kwa Coastal Union, ambayo nayo imejigamba kuwachachafya Wekundu hao wa Msimbazi, mechi itakayokuwa na msisimko wa aina yake katika uwanja huo wa Taifa.

Endapo Simba itashindwa kuifunga Coastal Union leo, basi huenda migogoro ikazidi kushika hatamu katika klabu hiyo ambayo kila mtu ameanza kuiangalia kwa jicho la umakini mno, huku baadhi ya viongozi wake wakiona kuwa wanastahili kukaa kando kwa kushindwa kuiongoza timu yao katika nafasi nzuri ya kutetea ubingwa wao.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...