https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Sunday, March 31, 2013

Tunawatakia Pasaka Njema, ila Amani itawale


LEO Jumapili, Wakristo wote Tanzania wanaungana wenzao duniani kote kuadhimisha Sikukuu ya Pasaka, ikiwa ni kufufuka kwa Yesu Kristo.

Siku ya leo ni muhimu kwa Wakristo wote, huku ikianzia tangu juzi Ijumaa Kuu, hivyo ni wakati wa waumini wote na wale wasiokuwa waumini wa dini hiyo kuadhimisha kwa Amani na upendo.
Mara kadhaa, wapo baadhi ya watu ambao hutumia siku za Sikukuu
kufanya uhalifu, hivyo jeshi la Polisi linapaswa kuwa makini katika siku hizi kwa ajili ya kuhakikisha watu wanaishi kwa amani katika Taifa lao.

Tunajua kuwa wapo watu ambao siku kama hizi hutumia kwa kutembelea mahala popote, hasa kwenye kumbi za starehe, lakini kwasababu hayo ni maamuzi yao, muhimu ni wao kuona wanakuwa walinzi wa amani kwa kila mmoja wao.

Itakuwa ni picha mbaya kama kila mmoja atakuwa akifanya fujo, kama vile kumwaga vileo au kuendesha magari wakiwa wamelewa, jambo ambalo pia si la kiungwana.

Mitaa mingi ya jiji la Dar es Salaam na maeneo mengine ya mijini, wapo madereva ambao hupita wakiwa kwenye mwendo wa kasi pamoja na kutia mbwembwe, kuendesha magari yao bila kufuata sheria za usalama barabarani, jambo ambalo hakika husababisha ajali na kuzua balaa kubwa.

Hatupo tayari kuona watu wanaofanya vitendo hivyo wanazidi kupewa nafasi, hivyo ulinzi kila mmoja wetu anapaswa kuulinda kwa namna moja ama nyingine.

Amani ndio silaha kwa kila mmoja wetu. Hata zile pombe za kupitiliza, zinapaswa kuangaliwa, maana ndio chanzo cha mitafaruku katika maeneo mengi.

Tunajua hatuwezi kuwakataza watu hao, ukizingatia kuwa wanatumia gharama zao wenyewe, lakini si vibaya tukiwashauri hasa kwa kuwa watulivu, kutumia kwa ustarabu, pamoja na kurudi makwao kistaraabu pia.

Kwenye fukwe za Bahari ya Hindi na maeneo mengine yanayoshirikisha watu wengi kwa wakati mmoja, pia wazazi wanatakiwa wadumishe ulinzi kwa watoto wao.

Kuna watu ambao huenda kwenye fukwe na watoto wao, lakini hushindwa kuwalinda kiasi cha kuwaachia wakienda na maji na kusababisha mauti kwao.

Tunaamini haya tukiyafanyia kazi, Sikukuu zote, ikiwapo hii ya Pasaka inayofanyika kesho Jumapili na nyinginezo zote zitakuja kwa amani na kuondoka kwa amani pia.

Tunamaliza kwa kuwatakia tena watu wote afya njema katika Sikukuu hii ya Pasaka. Mungu Ibariki Tanzania



No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...