https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Thursday, November 10, 2011

Mwanamke aliyeacha Jeshi kwa ajili ya sanaa


KELVINA JOHN

Mwanamke aliyeacha Jeshi kwa ajili ya sanaa

WAHENGA walikuwa na semi zao ambazo zilikuwa na maana sana. Kati ya hizo, upo ule wa ‘Umdhaniaye ndiye kumbe siye’, huu unastahili kabisa kupigiwa mfano kwa Kelvina John.

Je, unajua kwa nini mwandishi wa makala haya anatolea mfano wa usemi huo kwa Kelvina? Hiyo ni kutokana na kuamua kuvua gwanda za Jeshi la Wananchi Tanzania  (JWTZ) kwa ajili ya kujikita katika kucheza filamu, fani ambayo anaendeshea maisha yake kwa sasa.

Katika mahojiano, Kelvina alisema uamuzi wake huo ulitokana na uthubutu wake kwa sababu kazi hiyo ya kuwa muigizaji na mtengeneza (Prodyuza) filamu alikuwa akiipenda tangu utoto.

“Maisha ni kujaribu, inakupasa mtu kujaribu na hasa kwa kile unachokipenda na hakika utafanikiwa kwa sababu utakifanya kwa ufanisi wa hali ya juu, ndivyo ilivyojitokeza kwangu na kufikia uamuzi wa kuachana na kazi ya Jeshi na kujikita katika filamu.

“Ingawa nilipata wakati mgumu kuanzia katika Jeshi, lakini namshukuru Mungu hivi sasa nafanya kile ambacho nafsi yangu inapenda na naweza kuendesha maisha yangu kutokana na kazi hii ya kuandaa na kucheza filamu,” ndivyo alivyoanza kuzungumza Kelvina.

Kwa wasiomfahamu vema, Kelvina John ni muandaaji wa filamu (Prodyuza) ambaye alianza kujikita katika fani hiyo mwaka 2000 kwa kuandaa filamu yake ya kwanza kabisa ambayo aliamua kuiita Mtazamo.

Ingawa pia na yeye ni muigizaji, lakini anapenda zaidi kufanya kazi ya uandaaji, kazi ambayo hapa nchini imekuwa ikifanywa zaidi na wanaume  na ndiyo maana upo uwezekano mkubwa kabisa akawa ni mwanamke pekee aliyeamua kujiiingiza katika fani hiyo ya uandaaji.

Pengine ujasiri huo umetokana na kuwa mwajiriwa wa Jeshi la Wananchi (JWTZ) ambaye alihitimu mafunzo na kupewa namba ya kazi 2712MTM na kupangiwa kazi katika kikosi namba 312 KJ Lugalo, kabla ya kuamua kuvua gwanda na kujikita katika filamu.

Katika mahojiano yake na Mtanzania, Kelvina alisema aliamua kuachana na kazi hiyo ya jeshi aliyoifanya kwa uadilifu ili akafanye kazi ya kuandaa na kuigiza filamu kwa sababu ni kitu kilichokuwa moyoni mwake tangu utoto.

“Ki ukweli katika maisha kila mmoja ana jambo ambalo anapenda, kwa sababu siku zote mimi nilikuwa naipenda fani hii, hata nilipokuwa jeshini nilihisi kama bado moyoni mwangu kuna jambo napungukiwa.

“Kwa sababu sikutaka kuidhulumu nafsi, niliamua ‘kusarender’ kazi ya jeshi na kuamua kujikita zaidi katika kuandaa filamu sambamba na kuigiza, kazi ninayoifanya hadi leo inayoniingizia kipato na kufanya nitatue matatizo yangu,” alisema.

Alisema aliamua kujitoa Jeshini mwaka 2003 baada ya kuona kazi yake ya kwanza aliyoandaa mwenyewe ambayo aliiita Mtazamo ikifanya vizuri, hivyo kuona ipo haja kutumia muda zaidi katika fani hiyo.

Kwa sababu inafahamika kazi hiyo ya Jeshi ni ‘bize’ sana kama angeendelea kuifanya, basi asingekuwa na muda wa kutosha kuandaa filamu zake, ndipo alipoamua kujivua gamba.

Mpaka sasa amefanikiwa kuandaa filamu tano, ikiwamo ambayo iko katika mchakato wa mwisho wa maandalizi ambayo inaitwa Leave or Die. Ni filamu ya action iliyowashirikisha mastaa kibao wa fani hiyo na kati yao mbali ya yeye mwenyewe, yupo Anti Fifi, Winter, Shilole na wengine.

Nyingine ambazo Kelvina amekwishatoa ni ile ya Penzi la Baba, Machozi na The Dadaz, ambayo aliitoa mwaka juzi. Aliwataka wanawake kuwa na uthubutu wa maamuzi ya mambo yao ili kufikia ndoto wanazohitaji, kwani hakuna lisiloshindikana endapo utakuwa na nia.

“Naomba wanawake wenzangu waache kubweteka, mimi unavyoniona dada yangu, naendesha maisha yangu kwa kazi hii, kwani imeniwezesha kuwapeleka watoto wangu wawili shule ambao Mungu amenijaalia.

“Na sasa nimeanza ujenzi wa kibanda cha kuishi huko jijini Mwanza, ambako ndiko ninapotokea, hivyo wale wenye mtazamo hasi juu ya kazi hii waachane nao kabisa,”  alisema.

Akizungumzia maisha binafsi nje ya shughuli hizo za uandaaji wa filamu pamoja na kuvua kwake gwanda za Jeshi, Kelvina anasema yeye ni mama wa watoto wa kike wawili aliobahatika kuwapata kati ya miaka minane iliyopita.

Hata hivyo, ilimlazimu kuachana na mumewe ambaye naye alitaka kumtia kiwingu kutokana na kutokubaliana naye kujihusisha na kazi hizo za uandaaji filamu, jambo ambalo hakukubaliana nalo ingawa awali alifanya hivyo.

“Kwa kweli hii ni sehemu ya changamoto katika maisha, namshukuru sana Mungu kuendelea kunipa ujasiri, hasa baada ya kupitia wakati mgumu na kufikia uamuzi wa kuachana na mume wangu ambaye hakuridhia nifanye kazi hii,” alisema.

Kwa sasa anaishi Mbezi jijini Dar es Salaam na ni mtoto wa kwanza katika familia yao ya watoto wanne, huku akiwa ndiye mtoto wa kike pekee. Akizungumzia ushirikiano anaoupata katika familia, alisema hakuna, kwa sababu hawafurahii fani aliyojikita.

“Baba yangu hataki hata kidogo nifanye kazi hii, yeye alitamani sana niwe ‘Air Hostess’ kwani ndiyo fani aliyonipeleka kusoma kabla ya mimi kuikacha na kujiingiza katika Jeshi, ingawa hakuvutiwa nayo sana, lakini aliipenda baada ya kusikia nimehitimu mafunzo na kuajiriwa.

“Nilikuja kumtibua tena nilipoamua kuvua gwanda na kujikita katika filamu. Simlaumu sana kwa sababu najua yeye, familia, ndugu na jamaa bado wana mtazamo hasi wa kazi ninayoifanya, lakini nataka niwaonyeshe kwamba sivyo wanavyofikiria.

“Ndio maana nahitaji kufanya mambo makubwa katika fani hii yatakayonifanya niwe msanii mkubwa ninayetambulika ndani na nje ya nchi na hapo nafikiri wataelewa nini nafanya na sasa nimeishaanza kuwaonyesha, hasa nilipofanikisha kumiliki kampuni yangu ya ‘Production’ ya kazi za filamu inayoitwa KJ Production,” alisema.

Kila kazi inakabiliwa na changamoto mbalimbali. Je, unajua fani hii ya filamu inakabiliwa na changamoto gani?

“Changamoto kubwa tunazokabiliana nazo katika fani hii hapa kwetu ni kama tatu hivi: Sehemu za kuigizia, wasanii wengi ni wasumbufu, hasa baada ya kulewa sifa, hivyo kitu unachotakiwa kufanya siku mbili inaweza kuchukua hata wiki, soko la kazi zetu na tatizo la wizi wa kazi ni kubwa mno, tunaomba Chama cha Hakimiliki (COSOTA) kisimame imara, wasanii tunaumizwa sana hatufaidiki vilivyo,” alisema.

Ushauri wake kwa Serikali, watambue vema umoja wao waliounda unaoitwa Tanzania Films Federation (TAFF) na kuupa nguvu uweze kufanya kazi ipasavyo pengine utasaidia kuzuia wimbi la wizi wa kazi zao.

Lakini kwa upande wa wasanii wenzake, aliomba kujenga tabia ya kuheshimiana, kushirikiana na kuifanya kazi hiyo kwa ufanisi kwa maendeleo yao binafsi na Taifa kwa ujumla. Huyo ndiyo Kelvina John.

xxxxxxMWISHO
 

Tuesday, November 01, 2011

Serikali izivunje COSOTA na BASATA

JUMATANO ya wiki hii nilikuwa miongoni mwa wadau wa sanaa waliohudhuria kikao cha Kamati ya Huduma za Kudumu ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania , kilichoongozwa na Mwenyekiti wake Jenista Mhagama.
 
Kikao hicho kilichohuduriwa pia na wasanii wa aina mbalimbali, kilifanyika katika viungwa vya Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA), kikiwa na maana kubwa ya kujadili masuala mbalimbali ya sanaa na wasanii nchini.
 

                                          Waandishi wa habari wakiserebuka.
Kikao hicho kilikuja wakati muafaka. Wakati ambao kwa miaka kadhaa sasa, bado wasanii wamekuwa wakiishi maisha ya kubahatisha huku wengine wakiindelea kuishi maisha mazuri kwa kupitia migongo ya wasanii.
 
Mengi yalisemwa. Wasanii wengi walichangia pamoja na wajumbe ambao ndio wabunge na wageni waarikwa. Inasikitisha sana . Kwani kwa kiasi kikubwa, matatizo mengi yalihjitokeza, huku chanzo chake kikiwa ni BASATA na ndugu zao COSOTA.
 
Hata hao wezi wanaodaiwa kuwapo, ilionekana dhahiri wanabebwa na wakubwa wao, ukizingatia kuwa BASATA ina uwezo wa kuwa wakali kwa ajili ya kuwakomboa watoto wao, yani wasanii ambao kwa Tanzania wanaishi kama omba omba.
 
Licha ya kuwa na vipaji vya hali ya juu, lakini wanachopata ni sifuri. Ni kutokana na hilo , nadiliki kusema kuwa ipo haja ya Serikali, kupitia Wizara yake ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, ili kuokoa maisha ya wasanii.
 
Kuvunjwa huko kunatokana na taasisi hizo kushindwa kufanya kazi zake kama inavyotakiwa, licha ya kupewa memo na wasimamizi wa sanaa kwa ujumla. Ndio, ingawa kwa COSOTA wao wanaweza kuyumba na msimamo wa Serikali, yani kuripoti kwa Wizara tofauti, kama ile ya Viwanda na Biashara pamoja na Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo.
 
Pamoja na hayo, bado hainifanyi niamini kuwa COSOTA na BASATA wanaweza kukomboa maisha ya wasanii wetu. Kwa sasa uwezo huo hawana. Maana kwa miaka kadhaa wamekuwa wakifanya kazi kwa kuleana zaidi badala ya kusimama kwenye ukweli.
 
Angalia, ukweli huu umedhihirika zaidi, maana viongozi hao wa COSOTA waliweza kuingia mitini, japo walijua kuwa walitembelewa na Serikali yao , iliyowekwa madarakani kihalali, huku ikiongozwa na watu makini.
 
Jamani, hakuna haja ya kulumbana. Hapa hakuna haja ya kuogopana. Kwanini BASATA waachwe na ndugu zao COSOTA? Kwa wale waliokwenda katika mjadala huo watakubaliana na mimi. Malalamiko mengi yalielekezwa kwao.
 
Usimamizi wao ni mdogo zaidi. Kuingizwa katika biashara za kujinyoji hiyo ndio kazi yao , hata kama wanajua hazina umuhimu kwa Watanzania. Kwa mfano, BASATA kuingizwa kwenye tuzo za Kilimanjaro Music Award huo ni umbumbumbu.
 
Tuzo hizo zinayumba. Hazina maana. Wasanii bora wanaachwa na wale wabaya wanapata tuzo. Sasa kwanini washiriki? Hawaoni ni kuwayumbisha Watanzania? Haya ni maswali ambayo majibu yake ni rahisi, endapo viongozi watajivua gamba.
 
Hayo yatakwisha kama viongozi hao watakubali kuwajibika. Moja ya sera ya uongozi bora ni kusimama kwenye ukweli kwa ajili ya manufaa ya watu wako. Inapotokea mambo yanakwenda tofauti, huo ni wizi.
 
Tuuseme hadharani, maana vikao kama hivyo havitakuwa na maana kama yanayojadiliwa yanaachwa na wale wezi kiuendelea kula raha. Inasikitisha mno. COSOTA wao kushiriki kwenye kampeni za mtu mmoja kuna nini ndani yake?
 
Wasanii kuendelea kuibiwa wakati wao wapo inaonyesha wameshindwa kazi. Kuyasema haya ni lazima kwa faida ya kizazi cha sanaa. Kuna haja gani msanii kuimba pasi kupata chochote cha maana?
 
Kwanini maisha yake ya sanaa asiyatumie kwenye kilimo? Nadhani hili la kuvunjwa kwa mabaraza hayo na kupewa kazi watu wengi wengine kutachangia kwa kiasi kikubwa kuibua ari ya utendaji kwa wasanii na wasimamizi wao.
 
Ikumbukwe kwamba sanaa ni kazi na inaweza kuleta utajiri mkubwa kwa Taifa. Nchi za wenzetu wao wanafanikiwa kwa kupitia ulingo huo wa sanaa. Ndio, maana nasema katika majumuisho ya kikao hicho, ipo haja ya viongozi waliopo wa BASATA na ndugu zao COSOTA wawekwe pembeni kama wameshindwa wenyewe kuwajibika.
 
Huu sio wakati wa kuoneana haya. Tusimame kwenye ukweli na hapana shaka, Jenista Mhagama, mwenyekiti wa kamati hiyo ya Huduma za Jamii pamoja na Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo watapata dawa hiyo kwa manufaa ya Taifa.
 
Mungu ibariki Tanzania
Mungu wabariki wasanii wetu
 
0712 053949
0753 806087

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...