https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Monday, January 28, 2013

Rais Kikwete akiri tatizo la ajira nchi yake ni kubwa



Rais Jakaya Kikwete

Na Mwandishi Wetu, Denmark
RAIS Jakaya Kikwete amekiri kuwa ukosefu wa ajira kwa vijana ni tatizo kubwa na kwamba lisipotafutiwa ufumbuzi wa kudumu linaweza kusababisha vurugu, machafuko na uasi wa umma, hata kwa nchi zinaoongozwa kwa misingi ya kidemokrasia, kama inavyotokea sasa katika nchi za Kiarabu.

Onyo hilo la Rais Kikwete linafanana na lile ambalo limekuwa likitolewa mara kwa mara na Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa, lakini, linapingana na kauli ya Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudensia Kabaka ambaye Machi 21 mwaka huu, alimjibu Lowassa akisema, "Kitendo cha wanasiasa kuendelea kusema tatizo la ajira kwa vijana ni bomu linalosubiri kulipuka, siyo kweli."

Jana akifungua mkutano wa mwaka wa Magavana wa Benki ya Maendeleo Afrika (AfDB) nchini Denmark, Rais Kikwete alisema moja ya sababu kuu ya machafuko yanayoshuhudiwa sasa kwenye ukanda wa nchi za Kiarabu, ni matokeo ya ukosefu wa ajira kwa vijana na watu kukata tamaa.

“Siyo kweli kwamba machafuko yanayoshuhudiwa kwenye nchi za Kiarabu ni matokeo ya Serikali za nchi hizo kukaa madarakani kwa kipindi kirefu kama wengi wanavyodhani. Ukweli ni kwamba hayo ni matokeo ya ukosefu wa ajira na watu kukata tamaa ya maisha,” alisema Rais Kikwete.

Alisema bila kutafutia ufumbuzi wa haraka, tatizo la ukosefu wa ajira kwa vijana ambao wengi hukimbilia mijini kusaka hali bora ya maisha, hata nchi zenye kuongozwa kidemokrasia, zinaweza kukumbwa na machafuko na uasi wa umma.

Rais alitumia fursa hiyo kuishukuru Denmark kwa kutoa fedha za kusaidia Mfuko wa Ajira kwa Vijana barani Afika, akisema ni moja ya mapendekezo kadhaa yaliyotolewa na kamati maalum ya kutafuta ufumbuzi wa matatizo ya kiuchumi barani Afrika ambayo yeye na Rais wa AfDB, Dk Donald Kaberuka, walikuwa wajumbe.

Mapema Rais wa Ivory Coast, Allasane Ouattara aliyehudhuria mkutano huo aliunga mkono kauli hiyo ya Rais Kikwete kwa kusisitiza kuwa vijana lazima wawekewe mazingira mazuri na kuwezeshwa kukabiliana na kumudu changamoto za kiuchumi, kitamaduni na kiteknolojia wanazokabiliana nazo.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...