https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Wednesday, January 09, 2013

SIWEZI KUVUMILIA



Stars isiwang’ang’anie Samatta na Ulimwengu

Mbwana Samatta, akiwa uwanjani.

Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
MWISHONI mwa wiki, Shirikisho la Soka nchini (TFF), lilitangaza kumtuma Mkurugenzi wao wa michezo, Sunday Kayuni, kwenda nchini Kongo katika klabu ya TP Mazembe kwa ajili ya kufanya mazungumzo juu ya wachezaji wa Tanzania wanaokipiga hapo, Mbwana Samatta na mwenzake Thomas Ulimwengu.

Pamoja na mambo mengine, Kayuni alitarajiwa kukutana na uongozi wa TP Mazembe ili kujadili namna gani inaweza kuwaachia nyota hao kwa ajili ya kuitumikia timu yao ya Taifa, Taifa Stars.

Safari ya Kayuni inatokana na wachezaji hao kuingia kwenye utata mara kwa mara wa kuachiwa na timu yao hiyo kwa ajili ya kujiunga na kambi ya Stars, huku mara ya mwisho vijana hao hawakucheza mechi kwasababu ya kuumwa kama walivyosema.

Kwa bahati mbaya, matokeo hayo yalikuwa magumu sana kwao, hasa pale walipoonekana wasaliti kwa Watanzania na kujikuta wakizomewa uwanjani, ingawa walikuwa nje ya uwanja. 

Hii ni hatari, hasa kwa kuiangalia TFF hii ambayo macho yao yote yapo kwa Samatta na Ulimwengu. Kwa sababu hiyo, hakika siwezi kuvumilia.

TFF na wadau wengine wa soka wanapaswa kuwekeza zaidi kwa wachezaji vijana, maana ndio suluhisho pekee la kukuza mpira wa miguu na sio kila mmoja kuwaangalia Samatta na Ulimwengu.

Bado ni vijana wadogo wanahitajika ndio kwenye soka, lakini kama tukiwa na wachezaji wengine wenye uwezo kama wao, maendeleo yatakuwapo.

Najua wapo wachezaji mfano wao wanahitaji kuitwa katika timu hiyo, lakini jinsi ya kuonekana ndio utata.

Vijana walionea katika kila kijiji, Kata, wilaya na Mkoa hawajui namna ya kujionyesha na kuitwa Stars. Kwa sababu hiyo, kocha Mkuu wa Stars, Kim Poulsen, anapaswa pia aitumie vyema falsafa ya kukuza soka la vijana.

Wao ndio nguzo na hakika hilo linajulikana kwa kiasi kikubwa. Huu ndio ukweli wa mambo.

Tanzania imekuwa ikifanya mambo kisiasa zaidi, hata katika soka uwanjani. Hii leo kutaka kuwang’ang’ania Samatta na Ulimwengu ni kutaka tu ajenda hiyo kuzungumzwa na wadau wa michezo. Tayari wachezaji hao wamesharipo kambini kwa ajili ya kujiandaa dhidi ya Ethiopia.

Hatuwezi kwenda hivyo. TFF iweke mipango zaidi kwa kuhakikisha kocha wao anatembelea katika mikoa au wilaya zinazoshirikisha ligi za vijana zenye ushindani kutokana na vijana wake kupania kuonyesha vipaji vyao.

Nimekuwa nikiangalia juhudi na utendaji kazi wa viongozi wengi kwenye medani ya soka, nimegundua kuwa waliokuwa wengi, wanaangalia zaidi wachezaji wenye majina kwa ajili ya kubeba kwenye vyombo vya habari.

Mtindo huu sio mzuri na ndio maana kocha wa zamani wa Taifa Stars, Mbrazil, Marcio Maximo alilipinga kwa nguvu zote.

Kupinga kwake kulisababisha maendeleo hasa kwa kuwapika wachezaji kama vile Samatta, Mrisho Ngassa na wengineo ambao leo hii wamekuwa na faida kubwa katika medani ya soka.

Wadau ambao walikuwa wakimpinga Ngassa, Kigi Makasy na wenzake leo hii ndio macho yao na huwataja sana wasipokuwa uwanjani.

Kwa bahati mbaya, tunahitaji kuwa na vijana wanaocheza soka la kulipwa nje yaa nchi. Lakini, kuna taratibu za wachezaji kurudi kwenye Mataifa yao kwa ajili ya timu ya Taifa.

Sisi kwetu Tanzania tumekuwa tukiwahitaji hata pale ambapo si wakati muafaka kwao. Kwa timu zinazojiendesha kwa mipango hatuwezi kuelewana nao.

Labda kwa Simba na Yanga ambao mara kadhaa wao wamekuwa watu wa sifa, wakijivunia nyota wao kuitwa Stars hata kama wanaathiri program za kocha wao, jambo ambalo si sahihi hata kidogo.

Kulisema hili hakuhitaji wote tuwe na digrii, maana ni dhahiri mikakati hii inaonekana na jinsi inavyoleta usumbufu kwa kiasi kikubwa.

Ndio maana nasema siwezi kuvumilia. Tufanye mambo yetu kwa kuangalia namna ya kutuwezesha kusonga mbele na sio kubakia kulalama juu ya wanasoka waliokuwapo nje, akiwamo Samatta na mwenzake badala yake tubuni namna ya kuwaongeza wengine.

0712 053949
0753 806087

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...