https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Thursday, January 31, 2013

Vita ya ukahaba Tanzania, wakamatwe na wateja wao


Changudoa akizungumza na mteja wake, katika moja ya mitaa ya jiji la Dar es Salaam.

Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
TANZANIA imezidi kuingia kwenye vitendo viovu vikiwamo vya ukahaba, jambo linalosababisha serikali kuliangalia hilo kwa kina.
 
Hawa walikutwa mida mibovu, nao eti wapo kazini.

Leo tunashuhudia baadhi ya sehemu zenye mwingiliano mkubwa wa watu wengi, serikali inapenyeza jicho lake kiasi cha kuwakamata au kuwakimbiza akina dada wanaofanya vitendo vya kuuza miili yao.


Ni jambo jema kwa Tanzania ya leo. Tanzania yenye kukosa rutuba na mvua katika sehemu nyingi, hiyyo kwa kiasi fulani kufikiria labda uchafu wetu mitaani unaleta yote hayo.

Dar es Salaam imesambaa watu wanaofanya biashara ya ukahaba, japo ni kwa kutofautiana hali zao. Kwa mfano, Buguruni mtaa wa Sewa wapo akina dada wanaofanya biashara hiyo.

Hawa hawana thamani kabisa, maana gharama zao haizidi 1000 hadi 15,000 kwa kila mzunguuko mmoja.

Watu hawa hawawezi kukaa na wale wanaojiuza Kinondoni makaburini au wale waliokuwa kwenye madanguro ya thamani na wale wanaojiuza kwa kujigharamia viingilio vya club za thamani.

Msichana huyo ni yule anayejiweza, maana hujiwekea bajeti ya 20,000 na kuendelea kwa kujua pesa zake zitarudi atakapopata mteja ambaye ni dhahiri naye anajiweza ndio maana akaenda kwenye kumbi za starehe zilizotapakaa jiji lote.

Ukitaka kujua wingi wao, tembelea katika madanguro yao, kwa wale waliokusanyika pamoja, kama vile Mwananyamala Hospitali, Uwanja wa Fisi, Sinza na maeneo mengi ya jiji.

Pamoja na yote hayo, akili yangu haileti majibu sahihi kwa wale wanaofukuzana na akina dada poa. Nasema hivyo maana biashara hii inachangiwa kwa kiasi kikubwa na wanaume.

Hawa ndio wanaokwenda kuwanunua tena wengineo ni wenye heshima zao mitaani, kiasi cha kutoamini. Hivyo basi, katika kupambana na suala hilo la watu wanaojiuza, nguvu kubwa pia inatakiwa kuelekezwa kwa wanaume wanaonunua miili ya changudoa.

Tufanye nao mazungumzo kuwabana pia na kuwajua wateja wao. Pia hawa watupe ratiba kamili ya mijibaba hiyo ambayo inaacha wake zao ndani na kuwafuata changudoa kwa sababu wanazojua wao.

Huu ndio ukweli. Handeni Kwetu inathamini juhudi za serikali kupambana na watu hao, lakini pia wanaume ndio wa kukamatwa zaidi ili waache tabia hiyo mbaya katika jamii.

Kwanini nasema hivyo? Msichana anayefanya kazi hiyo ya kujiuza kuanzia saa mbili usiku hadi majogoo au wale wanaojipanga kama nyanya kusuburi wateja wao wakikosa kabisa, sidhani kama ataendelea kukaa hapo kupiga miayo zaidi ya kutafuta kazi nyingine.

Wakati baadhi yao ukifanya nao mazungumzo wanasema ugumu wa maisha na kukimbilia kwenye kazi ya ukahaba, basi huko nako wakute maisha magumu zaidi ya waliyokuwa wakifanya awali.

Wabaki na njaa yao, pale wanapokosa wateja, jambo ambalo hakika litasaidia kwa kiasi fulani kuwaondosha kwenye kazi hiyo. 

Lakini, kama kila anayeingia kwenye kazi ya ukahaba anaona nafuu ya maisha kwa kupata wateja, hakika idadi ya makahaba itaongezekana mara dufu.

Msako unapofanywa na kukutwa wao na wateja wao, wote wawajibishwe kwa pamoja bila kuoneana haya. Tena kama ni adhabu kwa wanaume iongezwe zaidi ili waone kumbe ni hatari kufanya tendo la ndoa kwa makubaliano ya kuuziana.

Kinyume cha hapo tutazidi kuwa na Taifa lisilokuwa na maadili, huku changudoa wakijipanga barabarani kama wauza samaki, bila haya wala soni, kwakuona wapo wa kuwanunua kwa bei wanazotaka wao.

Huu ndio ukweli wa mambo. Serikali za Mitaa kwa kushirikiana na serikali Kuu inaweza kuliondoa tatizo hili kwa kuanzia chini, wanaouza miili yao na wale wanaonunua wote ‘Mazikanyange’.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...