https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Wednesday, January 02, 2013

Bongo Movie wauteka msiba wa Sajuki

Wastara aliyeshikwa kichwa akilia kwa uchungu kutokana na msiba wa mumewe Sajuki



Wastara aliyefunikwa uso akilia kwa uchungu

Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
MUUNGANO wa wasanii wa filamu Tanzania, unaojulikana kama Bongo Movie, umeuteka msiba wa msanii Juma Kilowoko, maarufu kama Sajuki kwa kuiomba familia ya marehemu ili wauzike mwili wa msanii mwenzao Ijumaa saa tano asubuhi, katika makaburi ya Kisutu.

Alieoa nyumba moja na Sajuki, Haroub Mbeleki, kushoto, akizungumza machache na wadau wa sanaa waliofika msibani.

Ombi hilo lilikubaliwa na baba mzazi wa marehemu, Juma Kitilu na kuagiza watu walioweka msiba mwingine nyumbani kwao Songea, kuvunja na kupanga safari ya kuja jijini Dar es Salaam kwa mazishi.

Katika kikao kilichoitishwa na Rais wa Shirikisho la Filamu Tanzania TAFF, Simon Mwakifwamba, kilitangaza taratibu za msiba huo ambapo pia Kamati sita ziliundwa kwa ajili ya kuweka sawa.
Msanii mkongwe wa filamu Natasha, akiingia msibani.

Akizungumza na Handeni Kwetu msibani hapo, Mwakifwamba alisema kamati hizo ni Kamati ya Mazishi, Kamati ya Fedha, Kamati ya Itifaki, Kamati ya Chakula, Kamati ya Habari, Kamati ya Usafiri na Kamati Kuu inayobeba na kusimamia kamati zote zilizoundwa katika msiba huo.
Baba wa marehemu, Mzee Juma Kitilu, kulia akizungumza nyumbani kwa mtoto wake, marehemu Sajuki leo.

Alisema kuwa wameshukuru baba wa marehemu kukubaliana na wazo lao la kumzika mwenzao Dar es Salaam kutokana na umuhimu wake na hamu ya kutaka kuzikwa na mamia ya mashabiki wake.
Marehemu Sajuki enzi za uhai wake

“Hili ni pigo la wasanii na mashabiki wao kwa ujumla, hivyo tunachoshukuru kuwa familia imetuelewa na wote kuwa kitu kimoja, hasa kwa kuhakikisha kuwa waliokuwa Songea nao wanaingia hapa kuanzia au kesho,” alisema.

Wasanii wa vichekesho Tanzania, Mtanga kushoto na Kiwewe wakiingia msibani Tabata Bima leo.

Baba yake Sajuki, mzee Kitilu alisema kuwa ameona hana sababu za kuwakatalia wasanii kwa ombi la kushiriki kwa karibu msiba wa mwenzao, jambo lililomfanya akubali haraka kwa ajili ya umuhimu wao.
Mtangazaji wa Clouds Tv, Zamaradi Mketema, akizungumza na wadau wa filamu katika msiba wa Sajuki nyumbani kwake Tabata Bima leo.

“Sina sababu ya kuweka ngumu kwa wasanii wanaotaka kumzika mwenzao, hivyo wale wote waliokuwa Songea, nimewaambia wafunge safari kwa ajili ya kuja Dar es Salaam kumzika Sajuki Ijumaa,” alisema.

Awali, Handeni Kwetu ilimshuhudia mke wa marehemu, Wastara akilia kwa kuomboleza msiba wa mume wake, akisema kuwa alishatangaza kifo chake kwa wiki ya mwisho ya mwaka 2012.

“Uliniambia nikuagie kwa wote uliowakosea katika kipindi cha maisha yako, kumbe ulishajua unataka kuniacha peke yangu? Nitaweza mimi jamani maisha ya peke yangu Sajuki wangu,” alisikika Wastara akilia na kushikwa na kwi kwi ya uchungu.

Kutokana na imani ya Kiislamu, kupatikana picha ya Wastara ni kazi kubwa, maana mara baada ya kufikwa na msiba huo, taratibu za kidini zilianza kuchukua mahali kwake na kuhakikisha haonani na wanaume nje ya familia yake.

Sajuki alikufa saa moja asubuhi katika Hospitali ya Taifa Muhimbili, ikiwa ni baada ya kukaa hapo kwa siku kadhaa akitibiwa. Kabla ya kifo chake, Sajuki alikuwa na maradhi ya tumbo, huku akianguka siku chache zilizopita jijini Arusha, alipokwenda kufanya shoo.

Kuanzia saa mbili za asubuhi, mamia ya watu na wasanii yalikuwa yakizidi kuingia nyumbani kwa marehemu, Tabata Bima kwa ajili ya kushiriki msiba wa Sajuki, uliohuzunisha watu wengi.




No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...