https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Monday, September 09, 2013

SIWEZI KUVUMILIA:Katibu Mkuu mgeni, si kwa Yanga au Simba



Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
WIKI iliyokwisha ilikuwa na mshike mshike mzito kutoka kwa klabu ya Yanga, baada ya kusemekana kuwa uongozi ulikuwa na lengo la kumuajiri Katibu Mkuu Mkenya, baada ya nafasi hiyo kukaimiwa kwa muda sasa na Lawrence Mwalusako.
Mwenyekiti wa Yanga, Yusuf Manji, pichani.
Ulikuwa ni mshike mshike mkubwa mno. Kila mmoja alisema lake, huku majibizano hayo yakichangiwa na habari hizo za Patrick Naggi kupewa nafasi hiyo nyeti ndani ya Yanga.

Ili kukoleza joto hilo, Baraza la Wazee kwa kupitia Katibu wao Ibrahim Akilimali, alitangaza hali ya hatari kwa Naggi kuwa asipoangalia atatolewa madirishani.

Hiyo ni kutokana na wao kupinga vikali, hivyo raia huyo wa Kenya afungashe virago vyake kama kweli alikuwa ameajiriwa na klabu yao ya Yanga, moja ya timu kongwe kabisa barani Afrika.

Yanga iliyoanzishwa rasmi mwaka 1935, haikuwahi kuongozwa na Katibu Mkuu mgeni, akiwapo Naggi mwenyewe. Hii ndio kusema kuwa, endapo hilo lingefanikiwa, basi ndio wangeanza mwanzo wa mwendelezo huo kwa maslahi ya klabu yao.

Inawezekana si tatizo kwa timu kama Yanga au Simba kuwa na Katibu Mkuu ambaye si raia wa Tanzania. Inawezekana kabisa Mkenya, Mganda na wengineo kupewa nafasi hiyo.

Kwani kuna ubaya gani? Mbona nafasi za makocha zinapewa wageni? Tunapotaka kuzungumzia soka la Kimataifa na mikakati yake, Siwezi kuvumilia kuona licha ya Dunia kuendelea, lakini baadhi ya klabu zetu zinajiendesha ndivyo sivyo.

Hata hivyo, hata huyo Yusuph Manji na jopo lote la uongozi wa Yanga haliwezi kufanya lolote zaidi ya kuwasikiliza wanachama wao. Wanachama ambao kwa sababu wanazojua wao, eti wamekuwa wakiwaweka mbele kuliko kitu kingine.

Kama leo tutalaumu kwanini wazee wa Yanga wametoa tamko zito la kumtoa Naggi dirishani endapo atathubutu kuwa Katibu Mkuu wao, tulaumu pia uongozi kwa kushindwa kuwa makini na kutetea misimamo ya kimaendeleo.

Ni juzi tu Yanga walitangaza kuitisha Mkutano Mkuu wa dharula. Mkutano huu ulikuwa na nia ya kuwapa nafasi wanachama wao wapitie mkataba wa Azam TV.

Wajuzi wa mambo ya soka walishangaa. Shirikisho la Soka nchini (TFF) nalo likashangaa. Hawa Yanga, chini ya viongozi wao waliowachagua kwa ridhaa yao wanashindwa kutoa uamuzi hadi waitishe mkutano?

Kuna nini katika suala hilo? Hizi fedha za kuandaa mkutano huo zingetoka wapi na kwa manufaa gani? Jibu lilishapatikana kwa Yanga. Ni pale waliposema hawawezi kukubali mechi zao zionyeshwe kwenye luninga ya klabu ambayo nayo ni mshindani wao, yani Azam.

Sawa, hilo lilikubaliwa ndio maana wakaambia pia katika mechi zao ambao wao ni wenyeji watasikilizwa, ila pale ambapo wao ni wageni hawatakuwa na sauti ya kugomea wasionyeshwe.

Jasho likawatoka. Wakaona wameshindwa kudhibiti hilo, maana timu zote 13 zimeridhia isipokuwa wao tu. Wakati hayo yanaendelea, ndipo serikali nayo ilipoingia na kuwataka mwanasheria wao apitie upya mchakato huo na Yanga kuamua kusitisha mkutano wao huo uliopangwa kufanyika katika Ukumbi wa PTA Sabasaba.

Ni kutokana na hilo, Yanga hii, yenye viongozi kama Manji kamwe haiwezi kuamua lolote la haja. Inawezekana kabisa wapo wasomi Tanzania ambao ni wanachama wa Yanga wanaweza nafasi ya Mwalusako, ila inapotokea nafasi ya kumuajiri mgeni asikataliwe.

Pamoja na hayo, inahitaji maelewano, ukizingatia kuwa klabu hizi zinazojiita kongwe, zinazolingia wanachama, zimesheheni watu wa kila aina na wenye mitizamo tofauti.

Ndio maana nasema, kwa Yanga hii si ya kuwa na Katibu Mkuu mgeni bila kuelimishana faida inayoweza kupatikana katika hilo.

Ukiacha hilo, Yanga pia imekuwa ikiwaweka mbele wanachama wao kwa kuwasikiliza na kuwapa nafasi ya kuamua, kama vile walivyowapa nafasi ya kuamua juu ya Azam tv.

Kinyume cha hapo kunaweza kuibuka mgogoro mzito utakaoweza kuathiri klabu hiyo ya Yanga. Hilo likitokea kamwe sitaweza kuvumilia.
+255 712053949

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...