https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Monday, September 02, 2013

SIWEZI KUVUMILIA:Hongera Cheka, tunaokuthamini tupo nyuma yako


Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
WATANZANIA wenye mapenzi mema na mchezo wa ngumi lazima waheshimu mchango wa bondia Francis Cheka. Huyu ni bondia mwenye makali ya kutosha.
Bingwa wa Dunia, Francis Cheka, pichani.
Kila anapoingia ulingoni amekuwa akifanya vitu vya kufurahisha wadau wa ngumi kutokana na kufanikiwa kuibuka na ushindi, hivyo kuzidi kukuza jina lake.

Baada ya kuwapiga mabondia mbalimbali kutoka Tanzania na nchi kadhaa za Afrika, Ijumaa iliyopita, Cheka alifanya tena maajabu kwa kumtandika Phil Williams, bondia kutoka nchini Marekani.

Pambano hilo la Ubingwa wa Dunia mkanda wa (WBF) na kufanyika katika Ukumbi wa Diamond Jubilee, Cheka alishinda kwa pointi.

Pamoja na kuheshimu mchango wa Cheka, bado malalamiko yangu yapo kwa serikali na wadau wenye uwezo wa kuwekeza zaidi kwenye mchezo huo.

Serikali yenye uwezo wa kukuza na kuendeleza mchezo huo, sanjari na kutambua mchango wa Cheka na mabondia wengine wa Tanzania.

Hii si mara yangu ya kwanza kuandika makala inayoelezea kumuunga mkono bondia huyo mwenye maskani yake mkoani Morogoro.

Nimeshawahi kusema mara kadhaa, huku kilio changu kikitokana na umahiri wa bondia huyo anayestahili kulindwa ili afike mbali zaidi.
Tunahitaji sapoti ya Cheka ili aendeleze ubabe katika Mataifa makubwa, kama vile Marekani, Uingereza, Ujerumani na mataifa mengine.

Hivi karibuni Cheka alizungumzia mpango wake wa kupunguza kupanda ulingoni kwa mabondia wa Tanzania. Alisema hivyo kwakuwa lengo lake ni kupiga hatua ya juu zaidi katika mchezo huo wa masumbwi.

Hata hivyo, uamuzi huu kwa Cheka unaweza kuwa na changamoto, ukizingatia kuwa bondia anaingiza pesa anapopanda ulingoni.
Kama hivyo ndivyo, je wadau wa ngumi wanajipanga vipi kuhakikisha kuwa mkali huyo anapata pambano ya Kimataifa zaidi kwa manufaa yake?

Hakika siwezi kuvumilia kuona mabondia wetu wenye makali tunashindwa kuwathamini. Hii si mara ya kwanza. Tanzania inapenda zaidi kuvuna kabla ya kupanda.

Kwanza tupande ili kesho tuvune. Hatuwezi kupiga hatua kama hatuna mipango. Bila shaka huu ni wakati kuwekeza zaidi kwa mabondia wetu, akiwamo Cheka.

Ni wazi ana heshima na nguvu za kutosha. Kwa kulijua hilo, sote tutasonga mbele. Katika mchezo wa masumbwi, kuna changamoto nyingi.

Wakati mwingine bondia anapanda ulingoni akiwa hajui kinachoendelea juu ya fedha. Wakati mwingine wanapanda bila kutanguliziwa pesa zao.

Bondia anakuwa na pambano bila kujua namna gani atalipwa fedha zake. Huu ni wakati wa kuwa makini zaidi. Kinyume cha hapo mchezo wa masumbwi utashindwa kupiga hatua na kufifisha ndoto za mabondia.

Licha ya kuwa na wakali kama vile Cheka, ambaye ana uwezo wa kulitangaza Taifa, lakini nguvu zao huenda zikaisha kama hawatawezeshwa kusonga mbele.

Nafikiri ni wakati wa kuangalia changamoto zetu ili kesho mabondia wetu wapige hatua. Binafsi naunga mkono juhudi za mchezo huo.

Naheshimu mno ujuzi wa Cheka na hakika lazima wadau wote, wakiwamo viongozi wa serikali kuona namna gani ya kuweka mipango kabambe.

Michezo ni ajira. Michezo ina uwezo wa kuwapatia maisha bora vijana wetu, hivyo lazima tujiweke sawa kwa ajili ya kuangalia namna ya kulifanyia kazi suala hilo.

Huu ndio ukweli wa mambo. Kwa wale mabondia wenye makali, akiwamo Cheka, ni wakati wake wa kuendelezwa, kusimamiwa na kushauriwa namna ya kuwa bora zaidi.

Ningefarijika siku moja kusikia serikali imemgharamia Cheka aende japo katika nchi mbili ili kuangalia mapambano makubwa ya Dunia, ukizingatia kuwa huo ndio mpango mzuri wa kupanua mtandao wake kimasumbwi.

Kinyume cha hapo nitaendelea kuona mipango butu ya viongozi na wadau wa mchezo wa masumbwi hali inayochelewesha maendeleo ya mchezo wa ngumi hapa nchini.
Tukutane wiki ijayo.
+255 712053949

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...