https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Sunday, September 01, 2013

Kocha Stars amuita Mkude kuivaa Gambia, Ujerumani yaombea ITC watatu Tanzania



Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
KIUNGO wa Simba, Jonas Mkude ameitwa kwenye kikosi cha Taifa Stars kinachojiandaa kwa mechi ya mchujo ya Kombe la Dunia dhidi ya Gambia itakayochezwa Septemba 7 mwaka huu jijini Banjul.
Kocha wa Taifa Stars, Kim Poulsen
Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Kim Poulsen amemuongeza mchezaji huyo ili kuimarisha sehemu ya kiungo. Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager imeingia kambini tangu Agosti 29 mwaka huu kwenye hoteli ya Accomondia jijini Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotumwa kwenye vyombo vya habari na Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka nchini (TFF), Boniface Wambura, timu hiyo imefanya mazoezi leo asubuhi kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume wakati kesho Jumatatu (Septemba 2 mwaka huu) saa 10 jioni itafanya mazoezi kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Katika hatua nyingine, Chama cha Mpira wa Miguu cha Ujerumani (DBU) kimetuma maombi ya Hati ya Uhamisho wa Kimataifa (ITC) kwa wachezaji wawili wa Tanzania ili wajiunge na klabu mbili tofauti za nchini humo.

Maombi hayo yaliyotumwa kwa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) ni kwa ajili ya wachezaji Henry Claud Egito aliyezaliwa Desemba 31, 1984 jijini Dar es Salaam, na Dominic Johnson aliyezaliwa Agosti 14, 1991 jijini Tanga.

Wachezaji hao wanaombewa ITC kama wachezaji wa ridhaa. Egito anaombewa hati hiyo ili ajiunge na klabu ya FSV Lokomotive Dresden wakati Johnson anatakiwa na klabu na TSV 1967 Schwabbruck.

Aidha, usaili wa waombaji uteuzi kwenye uchaguzi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na Bodi ya Ligi Kuu (TPL Board) unaendelea na unatarajia kukamilika leo (Septemba 1 mwaka huu).


Kamati ya Uchaguzi ya TFF chini ya Mwenyekiti wake Hamidu Mbwezeleni ilianza usaili juzi (Agosti 30 mwaka huu) ambapo matokeo ya usaili yanatarajiwa kutangazwa keshokutwa (Septemba 3 mwaka huu).

Kati ya Septemba 4 na 6 mwaka huu, Kamati ya Uchaguzi kupitia Sekretarieti ya TFF itawasilisha kwenye Kamati ya Maadili ya TFF mashauri yote ya maadili ili kujadiliwa na kutolewa uamuzi na kamati hiyo.

Vilevile kati ya Septemba 4 na 6 mwaka huu ni kipindi cha kukata rufani kwenye Kamati ya Rufani ya Uchaguzi kwa masuala yasiyo ya maadili. Kwa watakaokata rufani wanatakiwa kuambatanisha na ada ya rufani kwa Katibu Mkuu wa TFF kabla ya saa 10 kamili jioni ya Septemba 6 mwaka huu.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...