https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Sunday, September 08, 2013

Rais wa Zanzibar Dkt Shein awataka wataalamu kulitumikia Taifa lao

Na Salum Vuai, Maelezo
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, amesema wahitimu wa fani mbalimbali za afya wanaosomeshwa na serikali hawana budi kubaki nchini na kuitumikia jamii yao. Dk. Shein ametoa wito huo jana baada ya kuzindua majego mapya ya dahaklia ya wnafubzi wa kike na jengo la madarasa, katika Chuo cha Taaluma ya Sayansi za Afya, Mbweni nje kidogo ya mji wa Zanzibar.
 IMG_4153

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein,alipokuwa akitoa hutuba yake kwa Wananchi na wanafunzi (hawapo pichani) wakati wa Sherehe za Uzinduzi wa jengo la madarasa  ya Chuo cha Taaluma za Sayansi ya Afya, lililogharamiwa na Serikali ya Oman kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, huko Mbweni Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja jana. Kushoto ni Waziri wa Afya Juma Duni Haji na Mshauri wa Mambo ya Afya, Wizara ya Afya ya Oman, Dr. Sayeed Sultan Bin Yarub Bin Qaatan Al- Busaid, (kulia).

IMG_4140



Mshauri wa Mambo ya Afya,Wizara ya Afya ya Oman,Dr.Sayeed Sultan Bin Yarub Bin Qaatan Al- Busaid,akitoa salamu zake wakati wa sherehe za uzinduzi wa madarasa mapya ya kusomea katika Chuo cha Taaluma za Sayansi ya Afya,yaliyojengwa na  Serikali ya Oman,na ushirikiano wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.[Picha na Ramadhan Othman,Ikulu.

Akizungumza na wanafunzi na wananchi mbalimbali waliohudhuria hafla hiyo, Dk. Shein alisema, serikali inatumia gharama kubwa kuwasomesha wanafunzi wake, hivyo nao wanapaswa kutimiza ihsani na utu kwa kufanya kazi nchini badala ya kukimbilia nje. Amesema kwa bahati mbaya, wapo baadhi ya wananchi na watumishi wa umma wakiwemo wafanyakazi wa sekta ya afya ambao husomeshwa kwa fedha nyingi za serikali lakini baada ya kumaliza masomo yao huondoka nchini na kukwepa wajibu wao wa kuwatumikia wananchi wanyonge waliogharamia fedha hizo

“Hili siyo jambo zuri kwani siku zote ni vyema binadamu azingatie ihsani anayofanyiwa na wenzake”, alisisitiza. Akitoa mfano kwa kunukuu hadithi ya Mtume Muhammad (S.A.W), Rais Shein aliwanasihi vijana wote wanaopata fursa ya kusomeshwa na serikali, kuwa na uzalendo na mapenzi kwa jamii yao inayowategemea kuihudumia. Alisema kwa hadithi hiyo, alisema Mtume Muhammad (S.A.W) anautanabahisha umma juu ya ubaya wa kuwaacha watu wanaoutegemea kwa kusema:

“Yatosha kwa mtu kupata dhambi kwa kumtupa yule anayemtegemea” Hata hivyo, alisema kama mtu anataka kuondoka kwenda kutafuta kazi nje ya nchi, serikali haimzuii, lakini kwanza ni lazima alipe fedha zote zilizotumika kumsomesha, kwa mujibu wa agizo la serikali kwa wizara zake zote. Alifahamisha kuwa, iwapo mtu atashindwa kulipa gharama hizo, wazee au familia yake italazimika kufanya hivyo.

Akizungumzia kukamilika kwa ujenzi wa majengo hayo pamoja na kupatikana vifaa vya kisasa, alisema hiyo ni njia moja ya kuimarisha mazingira ya utoaji mafunzo kwa vijana wanaojiunga na chuo hicho kwa masomo mbalimbali yanayotolewa hapo. Pamoja na kuwapongeza vijana waliobahatika kujiunga na chuo hicho katika huduma tafauti za afya, Dk. Shein alisema ni imani yake kuwa wanachuo wanaojiunga hapo, huchaguliwa kwa kutimiza sifa, na kwamba nao huamua kujiunga kwa kuelewa ugumu wa kazi yenyewe baada ya kumaliza masomo yao.
 
Alisema utoaji bora wa huduma za afya, lazima utanguliwe na huruma na ubinadamu, na kwamba kazi hizo humtaka mhudumu kuzingatia wito wa kuwahudumia wagonjwa kwa upendo pamoja na maadili ya taaluma yenyewe. “Kwa bahati mbaya, wapo baadhi ya wafanyakazi wa sekta ya afya ambao huweka pembeni vigezo hivyo na matokeo yake hutokea manung’uniko kwa wagonjwa wanaohudumiwa”, alieleza Dk. Shein Alisema, mlahaka mzuri na lugha nzuri kwa mgonjwa ni miongoni mwa mambo muhimu katika kumuhudumia mgonjwa.

Pamoja na changamoto mbalimbali zinazoikabili sekta hiyo na chuo hicho, Dk. Shein aliwapongeza viongozi na wafanyakazi wa hospitali za Unguja na Pemba na taasisi za afya kwa kujitahidi kuondoa udhaifu huo kwa lengo la kuwahudumia vizuri wagonjwa Alieleza kuwa, siku zote mgonjwa anahitaji huruma na imani kutoka kwa anaemuhudumia wakiwemo wanafunzi wanaohitumu kwenye chuo hicho.
 
Aliwahakikishia wanafunzi na watendaji wa sekta hiyo, kuwa daima serikali inatambua na kuthamini mchango wao kwa jamii, na hivyo inajitahidi kuimarisha maslahi yao kila uwezo unapopatikana. Aidha, alisema serikali inaendelea na sera yake ya kutoa matibabu bure kwa wananchi, ingawa katika baadhi ya maeneo, inapokwazwa na ufinyu wa bajeti huwataka kuchangia, lakini si nia ya serikali kuona wananchi wanapata shida.
Pia alifahamisha kuwa, katika kutanua wigo wa taaluma chuoni hapo, serikali imeamua kukiweka chini ya Chuo cha Taifa Zanzibar (SUZA), pamoja na kuanza kutoa digriii ya uuguzi kuanzia mwaka huu.

Aliishukuru serikali ya Oman chini ya uongozi wa Sultan Qaboos Bin Said, kwa uamuzi wake wa kujenga na kukiendeleza chuo hicho, akisema hiyo ni dalili ya mahaba makubwa kwa wananchi wa Zanzibar, ambao wana uhusiano wa miaka mingi na wenzao wa Oman.
Mapema, akitoa taarifa za ujenzi huo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Dk. Saleh Mohammed Jidawi, alisema hadi kukamilika kwake, ujenzi huo umegharimu dola za Kimarekani milioni 2.36, na samani zake dola 277,000.

Naye Waziri wa Afya Juma Duni Haji, alisema kujengwa chuo hicho na kuongezwa kwa dakhalia hizo, kutawaondoshea wanafunzi na walimu usumbufu kwani saa watapata nafasi ya kusoma na kufanya kazi kwa utulivu. Mkuu wa chuo hicho Dk. Haji Mwita, aliishukuru serikali kwa kushirikiana na uongozi na bodi ya chuo katika jitihada za kukiendeleza huku akiainisha changamoto kadhaa zinazohitaji kupatiwa ufumbuzi zikiwemo uhaba wa walimu, usafiri, vitendea kazi na uvamizi wa eneo la chuo unaofanywa na watu mbalimbali.

Kwa upande wake, Mshauri wa masuala ya afya wa serikali ya Oman, Dk. Sultan Al Busaidy, akitoa salamu sake kwa niaba ya nchi yake, alisema nchi yake inaona fahari kubwa kuiona Zanzibar ikipiga hatua katika kustawisha hali za watu wake, hasa katika sekta ya afya na elimu.

Alisema serikali ya nchi yake, inajivunia uhusiano wa dhati na udugu wa damu uliopo kati ya wananchi wa nchi mbili hizo, na akawaombea Wazanzibari mafanikio zaidi katika kuleta maendeleo. Ujenzi wa majengo hayo uliofanywa na kampuni ya Mazrui Building Contractors, uliwekwa mwezi Januari 2011, baada ya kuwekwa jiwe la msingi na Rais Dk. Shein tarehe 6 ya mwezi huo.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...