https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Monday, September 16, 2013

NADIN LEONARD DIM:Mwamuzi chipukizi anayekuna wengi uwanjani


Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
NYOTA njema huonekana alfajiri. Msemo huu maarufu hapa nchini Tanzania umezoea kutumiwa kila mtu anapotaka kuelezea jambo zuri linaloanza kuonekana mapema, hasa kwa watoto.
Mwamuzi chipukizi wa mpira wa miguu, Nadin Leonard Dim, pichani.
Mtoto anayefanya mambo mazuri licha ya umri wake huo, ni rahisi mtu kuweka msemo huo, kama ishara ya kubariki mwenendo wa kitu kinachoonekana mbele yake na kinachosubiriwa kwa hamu.

Ndio, msemo huu naweza kuutumia ninapomzungumzia Nadin Leonard Dim, mtoto mwenye miaka 16 anayefanya kazi nzuri katika fani ya kupuliza filimbi, yani mwamuzi wa kati.

Ni mwepesi mno, Anahaha uwanja mzima. Hana hata chembe ya uonevu anapokuwa dimbani akichezesha mechi, jambo linaloonyesha shauku ya kuona mazuri mengine ya kijana huyo wa baadaye.

Kwa waliobahatika kumuona Nadin, hasa katika mechi mbalimbali anazokuwa dimbani, hasa zile za kirafiki katika mitaa mbalimbali ya jiji la Dar es Salaam, atakubaliana na mimi kuwa ni hazina.

Mapema mwaka huu Nadin alichezesha mechi ya kirafiki kati ya Ashanti United na Moro United na kuwakuna wengi. Nadin ambaye kwa sasa ni mwamuzi wa daraja la tatu, wilaya ya Ilala, Ijumaa iliyopita alichezesha mechi ya kirafiki kati ya bendi ya Mapacha Watatu na Mashujaa Music.

Alifanya vitu vikubwa katika mchezo huo na kuamsha mijadala ya kila aina kutoka kwa wadau wa michezo waliodhuhuria mchezo huo katika Viwanja vya Leaders Club, Kinondoni, jijini Dar es Salaam.

Katika mazungumzo yake aliyofanya na Handeni Kwetu Blog, Dim anasema kuwa anapenda sana kazi hiyo ya kuchezesha soka kwasababu kila mtu anamsapoti anapokuwa dimbani.

Anasema kuingia kwake kwenye kazi hiyo kunatokana na yeye kupewa filimbi tangu alipokuwa katika shule ya Sekondari Azania, jijini Dar es Salaam, akiendelea na elimu yake ya sekondari.

“Wakati naendelea na masomo yangu, shule iliamini naweza mno kusimama dimbani kucheza mechi mbalimbali, jambo ambalo baadaye nilipata ushauri kuwa niingie rasmi.

“Mwalimu wangu  wa michezo ninayemfahamu kwa jina la Kaboneka, alinishauri pia nitafute kozi kwa ajili ya kupata elimu inayohusiana na mambo ya mwamuzi ili nifike mbali zaidi,” alisema Dim.

Anasema baada ya kupewa ushauri huo, aliamua kuufanyia kazi na kushiriki katika kozi ya ukocha kwa watoto iliyoandaliwa na Chama Cha Soka Kinondoni (KIFA) mapema mwaka huu.

Hatua hiyo imempa mwangaza zaidi na kufanikiwa kupenya na kupata daraja la tatu  wilaya Ilala. Kwa hatua aliyofikia sasa, Dim anaweza kuitwa na kupewa mechi mbalimbali za vijana na zile za kirafiki.

Anasema hana woga anapokuwa uwanjani kwasababu lengo lake ni kuchezesha kwa haki bila kuangaliana usoni. Dim anasema hata kama katika moja ya timu anayochezesha kuna mtu anayempenda, hawezi kumpa wepesi ili amfarahishe na kumnyonya mwingine.

“Nahitaji kufika mbali zaidi katika mchezo wa soka, hivyo kwa sasa ninachotaka kuifanya ni kuona nachezesha mechi kubwa zaidi zinazoshiriki ligi Kuu, kama vile Simba, Yanga, Mtibwa Sugar na nyinginezo.

“Naamini mpango huu utakuwa na mashiko katika harakati zangui za kimaisha, ukizingatia kuwa nina hamu ya siku moja nionyeshe namna soka linavyopaswa kuchezeshwa uwanjani,” alisema Dim.

Dim anayesoma kidato cha pili shule ya Sekondari Azania, amezaliwa mwaka 1997 katika Hospitali ya Mbezi Juu, jijini Dar es Salaam. Kwa sasa anaishi na wazazi wake Vingunguti jijini hapa.

Dim anayevutiwa na soka la Mbwana Samatta, mshambuliaji wa timu ya TP Mazembe ya Congo, ana mipango kabambe ya kuhakikisha kuwa anafika mbali ndani nan je ya nchi.

Mtoto huyo anayevutia kumuangalia anapochezesha soka, anaitaka TFF kufanyia kazi malalamiko ya waamuzi ili kuondoa kero sugu za ugumu wa maisha unaowakabili na kufikia kudai hongo.

“Huu ni wakati wa kuwaza namna gani ya kukuza soka letu, hivyo hakuna njia ya mkato katika hilo na ndio maana naendelea kujipanga ili mambo yaende vizuri katika soka la Tanzania.

“Naamini kwa kufanya hivyo soka letu litasonga mbele na kufikia malengo yetu, hasa kwa kuhakikisha kuwa TFF wanasimamia vyema mfumo wa utendaji kazi wa waamuzi hasa katika maslahi yao,” alisema.

Katika hatua ya kushangaza zaidi, Dim mwamuzi chipukizi na mwenye ndoto lukuki, anasema hana anayempenda katika idadi ya waamuzi wote Tanzania na kusema ndoto zake zitatimia kwasababu wengi wanamuunga mkono na kumpenda asimame langoni.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...