https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Saturday, September 21, 2013

Je, uliyekuwa naye ana mwingine ampendae?



Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
NI wiki nyingine tena msomaji wangu tunapokutana katika safu hii inayokujia kila Jumamosi, ikiwa na lengo la kuelezea mambo mbalimbali yanayohusu uhusiano na maisha.
Wawili wapendanao, pichani.
Nashukuru kama wewe ni mpenzi wa safu hii kiasi cha kuwa pamoja kila Jumamosi. Kwa wewe ambaye si shabiki zaidi, hivyo nakuombea ili tuwe wadau kwa ajili ya kujadili mambo haya.

Ndugu msomaji wangu, ni rahisi mno kujihusisha na mapenzi na waume au wake za watu bila wewe mwenyewe kujua. Hii ni kutokana na baadhi yao kufanya siri katika mambo haya.

Wapo baadhi ya wanaume au wanawake wakiulizwa juu ya uhusiano wao, hukanusha vikali. Mara kadhaa majibu yao ni kuwa wapo huru. Ati hawana uhusiano na mtu mwingine.

Ukiwachambua zaidi, wanakueleza walikuwa nao lakini wameachana naoa kwa sababu mbalimbali. Majibu haya mara kadhaa ni kurahisisha mamabo tu ili aingie kwa mtu mwingine.

Hata hivyo, katika mambo haya, mtu ambaye ana mtu mwingine ni rahisi kumgundua hilo, hasa kama atajiweka busy kwa mtu wake huyo. Kwa wale ambao kwa mwezi wanakutana mara moja, tena kwa nusu saa kamwe hawezi kujua kama mtu wake ana mpenzi mwingine.

Hii ni kwasababu mtu huyo anaweza kuendelea kuwa kwenye uhusiano na watu wote wawili bila kuonyesha utofauti. Hawa ni matapeli wa mapenzi.


Wapo wengi mtaani. Yule msanii Sam wa Ukweli aliwahi kuimba kuwa Hata kwetu wapo.

Chunga sana katika hilo ili usiingie kwenye mikono ya wajanja wa mapenzi na wanaopenda kufunga tera.

Kwanini nasema hivi? Wewe kama ni mwanaume umeingia kwenye uhusiano na msichana katika siku za hivi karibuni, jaribu kumchunguza zaidi mtu wako.

Kuanzia leo, hebu tumia muda wako kumvuta zaidi mpenzi wako. Jaribu kumpigia simu kila utakapohitaji. Kama hatapokea muda ambao wewe unajua ametingwa na kazi, jaribu tena baadaye.

Msumbue zaidi. Japo kwa kila saa au dakika uwe kwenye mawazo yake. Mpigie simu alfajiri kumuasha ajiandaye kwenda kazini.

Kufanya hivyo, ni dhahiri kuwa nafasi hiyo mara kadhaa huwa ngumu kwasababu kama anapendwa na wanaume zaidi ya wawili, ni dhahiri nafasi hiyo inaweza kuwa na ukakasi kwake.

Atakapofika kazini na muda mwingine pia fanya hivyo. Kwa kawaida, mtu mwenye uhusiano na mwanaume mwingine, nafasi hiyo kwake itakuwa ngumu mno hivyo kushindwa kuwadhibiti wote.

Wakati mwingine mshtukize katika mambo yako. Kwa mfano bila kujua umemfuata ofisini kwake muda wa kazi unapokwisha kwa ajili ya kumrudisha nyumbani.

Hii haijilishi una usafiri au utapanda daladala. Ukifanya hivyo, kuna uwezekano mkubwa huwa anafuatwa na mpenzi wake mwingine, hivyo pia kuwa mtego mwingine kwake.

Haya na mengine mengi yatamfanya akuone wewe ni king’ang’anizi, hivyo kumkera, hasa kama hakuwa na nia nzuri kwako. Kama alikuwa na lengo la kukuchezea ni wazi atashindwa kuwa na wewe.

Atakutafutia sababu za kukuacha, maana umemfanya awe busy na wewe wakati kuna mwingine anampenda. Kwa kawaida, mtindo huo na wewe pia utakupa picha kamili.

Utagundua kama hapo ulipo si mahali sahihi kwasababu ulichokuwa unakihitaji kwake ni tofauti. Kuna mengi ya kufanya, lakini si lazima usumbuke sana, ukizingatia kuwa siku zote mtu anayependa kwa dhati haoni mateso katika hilo.

Lakini usipofanya mtindo huo, hakika mtu uliyekuwa naye anaweza kuendelea kuwa na wewe kwa muda wakati ana mpenzi wake, mchumba wake ambaye muda wowote atafunga naye ndoa.

Kwa mtindo huo, wewe utakuwa kwenye wakati mgumu na kupata uchizi, hasa kama ulitumia gharama kubwa kuliweka sawa penzi lako ukiamini ndio chaguo lako halisi.

Tumia nafasi yako vizuri kujiridhisha kwa uliyekuwa naye kwa ajili ya kukufanya ufurahie mapenzi, ukizingatia kuwa uhusiano wenye uongo, uzandiki, usaliti unasababisha mfadhaiko na kusababisha kifo endapo mapenzi yataendelea kukujia tofauti.
+255 712053949

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...