https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Wednesday, September 04, 2013

MGODI UNAOTEMBEA:Hoja ya uhamiaji isiishie mkoani Kagera


Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
UHAMIAJI haramu ni ile hali ya mtu wa Taifa lingine kuingia kwenye nchi nyingine bila kufuata sheria. Kwa mfano, raia wa Rwanda kuingia Tanzania kienyeji.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete.

Hafuati utaratibu uliowekwa na nchi huru yenye mamlaka zake. Huyo anavunja sheria, hivyo kwa ujio wake huo, anaweza kufanya vyovyote anavyotaka.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Bernard Membe.

Hali hii ya uhamiaji haramu si ngeni duniani. Kumekuwa na mwingiliano na sababu nyingi zinazowafanya watu watamani kuingia katika nchi nyingine bila kupiga hodi.

Kila siku wanasikika waliokamatwa baada ya jaribio lao la kuzamia kushindwa. Wapo wanaorudishwa makwao bila kupenda na wale pia wanaowekwa kizuizini.

Wakati tunaangalia jambo hilo, lazima tukubali kuwa sheria zetu, utendaji kazi wetu umewapa urahisi watu wengi kuingia Tanzania soni.

Wahamiaji haramu wanaingia na kuweka makazi bila hata kuonwa na kuendelea na maisha yao. Na wale wanaonekana, wakati mwingine hawafikishwi popote, hasa kama watafanikiwa kutoa chochote kitu kwa watu wa uhamiaji au hata polisi.

Akiwa mkoani Kagera katika ziara yake ya kikazi, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete, aliwatangazia vita wahamiaji haramu.

Aliwataka wote walioingia Tanzania bila kufuata sheria wabebe kilichokuwa chao na kurudi kwenye nchi zao. Akaonyesha ukali zaidi kwa kuwapa siku 14 kabla ya kuingia kwenye oparesheni ya kuwarudisha makwao.

“Nilitoa maagizo kwa wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama yaani JWTZ, Polisi, Usalama wa Taifa na Uhamiaji watengeneze mpango kabambe wa kuyashughulikia matatizo hayo. 

Watayarishe na kutekeleza operesheni maalum itakayo au zitakazokomesha ujambazi, kuondoa wahamiaji wasiokuwa halali na kuondoa mifugo iliyoingizwa nchini kinyume na utaratibu na ile iliyoko kwenye maeneo yasiyo stahili,” Rais Kikwete aliyasema haya pia katika Hotuba yake ya kila mwezi.


Pamoja na kusema hayo, lazima watu tufahamu kuwa kasi inayapoonekana mikoani ya wahamiaji haramu, ni zaidi katika majiji makubwa, hasa Dar es Salaam.

Dar es Salaam ndio jiji pekee linaloweza kuwaficha wahalifu, wahamiaji haramu bila kuonekana. Ni rahisi kuona mtu anaendelea na biashara zake maeneo mbalimbali bila kuwa na kibali cha kuishi na ambaye pia hajafuata taratibu za kuingia.

Ni tofauti na Mataifa mengine. Nchini Botswana, wameweka sheriaa kali mno ya wahamiaji haramu. Hata wale waliofanikiwa kuwa na kibali cha kuishi huko wanapata shughuli pevu.

Kwa mfano Mtanzania anayeishi nchini humo, anaposhindwa kufahamu mwisho wa kibali cha kuishi humo, ni sababu yake ya kurudi kwao hata kama hataki.

Hata atakapojisalimisha katika ofisi za uhamiaji, hatapata ushirikiano wowote zaidi ya kurudi anapotoka. Ndio hapo anapotoka kwanza nje ya mipaka ya nchi hiyo na kurudi tena kama mgeni, ambapo hapo atapewa siku kadhaa za kuishi.

Haya ni tofauti na Tanzania. Nchi ya ukarimu na kitu kidogo. Ndio maana maeneo mengi hasa Dar es Salaam yanakumbwa na ongezeko la wahamiaji haramu.

Maeneo ya Kinondoni Shamba na mengine yote yana idadi kubwa ya watu wasiokuwa raia wa Tanzania na ambao hawajafuata sheria. Huko utakutana na watu wa Malawi wakiishi bila wasiwasi wowote.

Na inapotokea mjumbe au mwenyekiti anajua mtaa wake una wahamiaji wasiokuwa na kibali cha kuishi, basi amepata uhakika wa kupata hela ya sukari siku anapoamka mweupe.

Anachofanya ni kujichukulia visenti kutoka kwa watu hao na kushindwa walau kuwashauri wafuate taratibu za kuishi nchini. Hili ni jambo la kushangaza mno.

Rais Kikwete ameyasema hayo bila kujua kuwa maagizo yake mengi yanaishia njiani. Ni zima moto. Hakuna mipango kabambe, hivyo matamko yake kuishia kudharauliwa.

Siku 14 alizotoa kamwe haziwezi kuwa na faida. Zaidi zimeripotiwa kuchochea uhasama kwa wale wanaoshi sehemu mbalimbali za Tanzania, hasa vijijini, ambapo imeripotiwa baadhi ya watu hao kuingiza mifugo kwenye mashamba ya Watanzania, kama ishara ya kukerwa na kauli ya Kikwete.

Muleba suala hili ni kama mkuki kwao. Kwa kupitia Mbunge wao wa Muleba Kaskazini, Charles Mwijage, alizungumza kwa machungu pale aliposikia malalamiko ya wapiga kura wake kutokana na wafugaji kutoka nchini Rwanda kuingiza mifugo yao kwenye mashamba yao Watanzania.

Tamko la Mheshimiwa Kikwete lilielemea sana kwa Mikoa ya Kigoma, Kagera na Geita, huku majiji ya Dar es Salaam, Arusha, Mwanza na Tanga yakiachwa.

Mkoa wa Tanga nao una idadi kubwa ya wahamiaji haramu wanaotoka kwenye nchi zao na kuweka makazi ya kudumu au wanaofanya njia ya kuelekea kwingine wanapohitaji.

Mapema mwaka huu, maafisa wa uhamiaji wa Tanzania mkoani Tanga waliwakamata wahamiaji haramu 227 katika kipindi cha Januari hadi Novemba 2012.

Idadi kubwa ya wahamiaji hao walikuwa ni Waethiopia, lakini baadhi walitokea nchi nyengine kama vile Pakistan, Bangladesh, Denmark, Zambia, China, Uganda, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Guinea, Switzerland, Sri Lanka, Uturuki, Msumbiji na Italia

Hivyo kauli japo kauli ya Rais Kikwete ni njema, iliyosababishwa na raia wa Tanzania kukosa uhuru na usalama wa kutembea anavyotaka, ila juhudi sielekezwe nchi nzima.

Ingawa si dhambi raia wa Kenya, Uganda, Msumbiji, Malawi, Zambia, Congo na wengineo kuja kuishi Tanzania, ila muhimu ni kufuata sheria zilizowekwa.

Na inapotokea mtu ameweza kuja kuishi Tanzania, isiwe sababu ya kujifanya wapo juu ya sheria na kuanza kuwaletea kasumba zisizokuwa na maana kwa wenye nchi yao.

Mwaka 1982, Rais wa awamu ya kwanza, hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliweza kuwaruhusu wakimbizi wanaopenda kuwa raia wa Tanzania.

Historia inaonyesha kuwa jumla ya wakimbizi 30,000 waliweza kutumia fursa hiyo, wakati mwaka mwaka 2010 wakimbizi 160,000 wa kutoka nchini Burundi nao walikuwa raia wa Tanzania.

Serikali iwabane zaidi watendaji wake na pia juhudi za kukomesha uhamiaji haramu usibaki mikoa ya Kagera kama alivyotangaza rais Kikwete, maana janga hilo lipo pia jijini Dar es Salaam.

Tusipokuwa makini, tunaweza kudhibiti uingiaji wa wahamiaji haramu mikoa inayopakana na nchi jirani, lakini idadi kama hiyo kutokomea kwenye majiji yenye mwingiliano mkubwa.

Kama mtu anaweza kuishi Dar es Salaam bila kufanywa chochote, tamko la kudhibiti suala hilo lina mhusu nini? Kama leo hii mtu mwenye asili ya China anaweza kuja na kuishi kama wanavyoishi wengine, kwanini aishi kwa presha?

Sitaki kuamini kama watu wote wanaoishi jiji la Dar es Salaam ni raia au wanaishi kwa kufuata sheria. Wakati wao wakiishi bila presha, lakini kwao wao Mtanzania hawezi kuishi kwa raha kama atakuwa ameingia kienyeji kama nzi wa chooni.

Leo hii Mtanzania hawezi kuishi China ovyo ovyo bila kuwa na shughuli ya uhakika, ila wao wameweka makazi. Tena wengine wanafanya kazi inayostahili kufanywa na Mtanzania.

Ndio hapo utakapowakuta wamesheheni katika miradi mingi ya kimaendeleo, hasa ujengwaji wa barabara, ambapo nao wanashika chepe au kuwasimamia Watanzania.

Na kama huo uhalifu utakwisha sehemu ya mikoani na kuhamia jijini Dar es Salaam, hatauoni kama tunapoteza muda bure? Naheshimu utendaji kazi wa Rais Kikwete ila mara nyingi anaangushwa na washauri wake. Wale wanaovunja sheria kwa sababu ya kuneemesha matumbo yao.

Wale wanaojua fika kuwa operesheni za kudhibiti wahamiaji haramu zina maanufaa kwao kwasababu waya Kagera, tumie Aidha, niliwataka Maafisa wa Uhamiaji watimize ipasavyo wajibu wao. 

Ukweli ni kwamba, mambo haya kuendelea kwa muda mrefu kiasi hiki ni kwa sababu ya udhaifu wa mamlaka husika.

kambimbwana@yahoo.com
+255712053949

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...