https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Monday, May 06, 2013

Ruge Mutahaba afungua ukweli sakata lao na Lady Jay Dee

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
WAKATI watu wakiwa kwenye wasiwasi kwa kipindi kirefu sasa katika sanaa ya muziki wa Bongo Fleva, hatimae uongozi wa Clouds Media Group kwa kupitia Mkurugenzi wa Utafiti na Matukio, Ruge Mutahaba, umemtaka msanii wa Bongo Fleva, Judith Wambura, Lady Jay Dee kujipanga na kupokea changamoto badala ya kutafuta mahali kwa kujiegemeza kwa kueneza matusi kwao hali inayochafua heshima yao katika jamii.

Clouds Media wamefungua mdomo kwa mara ya kwanza kwa kipindi cha miezi mitano tangu Jay Dee alipokuwa akiwarushia makombora kwa madai kuwa wameharibu soko la muziki wa Bongo Fleva sambamba na kuitangaza bendi ya Skylight kwa ajili ya kuiangamiza Machozi Bendi iliyoanzia katika mgongo wake.
                                                      Ruge Mutahaba
Akizungumza jana jijini Dar es Salaam ambapo pia alikuwa akirushwa moja kwa moja katika redio ya Clouds FM, Mutahaba alisema Jay Dee amekuwa akilalamikia mambo mawili ambayo ni bendi ya Skylight na matangazo yake yaliyoshindwa kurushwa hewani japo alilipia Sh 240,000.
                           Lady Jay Dee
Alisema suala hilo walilimaliza baada ya kumueleza kuwa redio yao haiwezi kukataa matangazo kwakuwa ndiyo wanayowafanya waendelee kuwa kinara katika suala zima la kuiendesha Clouds FM.

“Nilimwambia kamwe hatuwezi kukataa matangazo na kama kuna lolote limefanyika, basi ni kwa bahati mbaya, ukizingatia kuwa tayari alishafanya kazi nyingi pamoja na kupewa urahisi kwenye kazi zake kwa kupitia Clouds FM.

“Pamoja na yote hayo, bado matusi na kejeli yaliendelea hasa katika mitandao ya kijamii jambo lililotufanya tuamuwe sasa kujibu japo hapo kabla tuliamua kubaki kimya kwa ajili ya kulinda hadhi ya kazi zetu,” alisema.

Kuhusu shutuma za kuitangaza zaidi Skylight Bendi, Ruge alisema bendi hiyo si mali ya Joseph Kusaga, Mkurugenzi wao wala yeye, kama madai hayo yanavyotolewa bila kufanya utafiti, isipokuwa ni mali ya Sebastian Ndege.

“Kama kuna mvutano kati ya Machozi Bendi na Skylight basi ni wa kibiashara maana wote wanalipa fedha za matangazo na kama chanzo ni Jay Dee kuporwa wanamuziki wake, hilo si jambo geni kwenye muziki.

“Dada yangu Asha Baraka asingekuwa makini angelia sana, maana kila bendi inayoanzishwa au kuendeshwa lazima ichukuwe wanamuziki kutoka kwake, ukizingatia kuwa ni jambo la kawaida hivyo tumuomba Jay Dee atumie busara katika hili pamoja na kuumiza kichwa kupokea ushindani na changamoto kama hizo za kuchukuliwa wanamuziki,” aliongeza Ruge.

Aidha, Ruge alisema Clouds FM ni redio ya watu binafsi, hivyo si ina utaratibu wake katika utendaji wa kazi, ikiwapo kuchagua nyimbo au kuacha kupiga kama kuna mtu amekwenda kinyume, hasa wale wanaopita nje na kuanza kuwatusi, kuwakejeli bila kukumbuka fadhira walizofanyiwa kabla ya kuwa maarufu wao.

Pia alisema Clouds FM ipo tayari kufanya majadiliano ya wazi na mtu yoyote mwenye hisia tofauti juu yao, huku ikiwataka wasanii waongeze bidii katika kazi zao ili wasimlaumu mtu wanapoanguka na kuwapisha wengine, maana muziki unaonekana ni wa kupokezana vijiti.

Maneno ya Ruge huenda yakapoza moto uliowashwa na Lady Jay Dee akiwatuhumu kuwa wamedhamiria kuangusha kipaji chake na bendi yake, huku akitumia sana njia ya mitandao ya kijamii kupambana vita hiyo na kuwaacha watu njia panda.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...