https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Sunday, May 19, 2013

Yanga rahaaaa, Utamu, ila Simba ilikuwa gonjwaaa

Wachezaji wa Yanga wakinyanya Kombe lao

Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
SIKU ya Jumamosi ya Mei 18, mashabiki wa soka wa Simba, nchini Tanzania hawataisahau kwasababu iliongeza machungu yao ya kukosa ubingwa na kuambulia nafasi ya tatu katika kinyang’anyiro cha Lihi ya Tanzania Bara iliyofikia tamati.

Machungu hayo yalitokana na Simba kukubali kichapo cha mabao 2-0 dhidi ya Yanga, timu ambayo ama kwa hakika iliutumia vyema udhaifu wa wapinzani wao wa jadi na kuwabugiza mabao hayo.

Kilichouma zaidi, ni pale wachezaji wa Simba, akiwamo Mrisho Ngassa kucheza chini ya kiwango na kusababisha manung’uniko makubwa kwa wadau wa Msimbazi. Makala haya yanaaendelea chini, endelea kuisoma
Duh Kimenuka. Ndivyo wanavyosema hawa mashabiki wa Simba wakiangalia bila kuamini matokeo ya mechi yao dhidi ya Yanga, baada ya kupigwa bao 2-0.
Mwamuzi Martin Saanya akipatiwa huduma ya kwanza, baada ya kugongana na wachezaji uwanjani.
Hapa mshambuliaji wa Simba, Mrisho Ngassa akitembezwa uwanjani kama mwali vile du. Hili ni tukio lililowashangaza na kuwasononesha watu wengi uwanjani hapo jana.
Majanja. Hawa jamaa walikutwa uwanjani wakishangilia kwa staili ya aina yake, baada ya kujigeuza vinyago kama ishara ya matusi kwa Simba. Kweli kushinda kuna raha yake aisee.
Shabiki wa Yanga akipelekwa kupewa huduma ya kwanza baada ya kuzimia wakati mchezo ukiendelea.




Raha ya mechi bao, ushindi. Chezea Yanga weweee
Kwa bahati mbaya zaidi, licha ya benchi la ufundi hali ya hatari inazidi kuwa upande wao, bado haijaweza kufanya mabadiliko ya haraka katika kipindi cha kwanza, hivyo timu yao kuzidi kuchoshwa na kukubali kipigo hicho kitakatifu.


Kwa matokeo yale, Yanga iliweza kutwaa taji la 24 la ubingwa wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, huku ikilinda heshima yake kwa kuwatandika watani zao.

Yanga ilimaliza msimu wa Ligi Kuu ikiwa na pointi 60, ikifuatiwa na Azam FC yenye 52 na Simba 45 

Simba hii ilikuwa gonjwa pande zote, huku mchezo huo, ukichezeshwa na refa Martin Saanya wa Morogoro, aliyesaidiwa na Samuel Mpenzu wa Arusha na Jesse Erasmo kutoka Morogoro, wakati Yanga walienda mapumziko wakiwa mbele kwa bao 1-0 lililotiwa kimiani na Didier Kavumbangu dakika ya tano ya mchezo huo.

Simba hii ilikuwa dhaifu. Haikuwa na makeke kama inavyojulikana. Pengo la wachezaji Emmanuel Okwi, marehemu Patrick Mutesa Mafisango lilionekana dhahiri.

Nafasi zao zilisababisha Simba kuwafunga Yanga mwaka jana kwa mabao 5-0, idadi ambayo iliongeza shauku ya mashabiki na kuuweka mchezo huo katika hali joto hasira.

Uwanja wa Taifa ulijaa kuliko ilivyokuwa kawaida, huku kila mmoja akijiweka mbele kushangilia timu yake. Kuonyesha kuwa bundi alikuwa akilia upande wa Simba, mashabiki wa Simba walianza kupata woga dakika za mwanzo za mchezo hadi pale walipofungwa na kujikuta wakimezwa na kelele za wanazi wa Yanga.

Hii ni kawaida katika mechi kubwa kama hizo. Wakati Simba wakiendelea kuwaza namna gani watatoka salama katika Uwanja huo, mshutuko wa kelele upande wa Simba ulisikika, pale mwamuzi alipowapa penati.

Kwa masikitiko makubwa, mchezaji Mussa Mude wa Simba, alipiga kidhaifu, bila kutumia umakini, hivyo kusababisha penati yake kupanguliwa na mlinda mlango wa Yanga, Ally Mustafa ‘Barthez’.

Penati hiyo baada ya Mrisho Ngassa kuangushwa dakika ya 27 na Nadir Cannavaro, hata hivyo ilikuwa ni siku ya kufa nyani, miti yote inateleza, hivyo kuonyesha ilikuwa ni siku ya kiama cha Simba.

Katika mchezo huo, Yanga ilitawala kipindi ca kwanza karibu chote ingawa mwishoni mwa kipindi hicho, kidogo Haruna Chanongo aliitia majaribioni ngome ya Yanga kama mara mbili hivi na kusababisha kona mbili mfululizo, lakini hazijakuwa na mashiko.

Mara baada ya mchezo huo kumalizika, aibu kubwa ilitawala kwa upande wa Simba na kujikuta wakiliacha jukwaa kwa ajili ya kurudi makwao shingo upande na machozi ya hasira kuwabubujika.

Kila mtu alikuwa akisema lake, hasa njiani, pale baadhi ya watu walipoanza kuhoji uhalali wa Ngassa kuchezwa dakika 90, wakati alionyesha udhaifu mwanzoni kabisa mwa mchezo huo.

Kilichowauma zaidi wanachama na mashabiki wa Simba, ni pale Ngassa alipokubali kufalishwa jezi ya Yanga na kutembezwa katika uwanja huo kama mwali.

Haya yaliwakera mashabiki wa Simba na kuwafurahisha Yanga. Ni wazi, kitendo hicho kilikuwa cha kihistoria katika mchezo huo. Lakini kwa Ngassa ni mara ya kwanza.

Akiwa kwenye malumbano na mabosi wake wa zamani, Azam FC, mchezaji huyo mwenye makeke mengi uwanjani, aliwashangaza watu wengi pale alipoamua kuibusu jezi ya Yanga macho kwa macho.

Kila alishikwa na bumbuwazi. Akitaharuki na kujiuliza. Kwanini Ngassa. Mbona anafanya vitu vya aina hii? Wengine wakasema haya ni mambo ya Ulaya Ulaya.

Kwenye mechi za ainaa hii zenye upinzani, si ajabu mtu kubusu au kuvaa jezi ya timu pinzani.

Simba SC; Juma Kaseja, Nassor Masoud ‘Chollo’, Haruna Shamte, Mussa Mudde, Shomary Kapombe, William Lucian ‘Gallas’, Mrisho Ngassa, Mwinyi Kazimoto, Abdallah Seseme/Ranmadhani Singano ‘Messi’, Amri Kiemba/Jonas Mkude na Haruna Chanongo/Felix Sunzu. 

Yanga SC, Ally Mustafa ‘Barthez’, Mbuyu Twite/Juma Abdul, David Luhende, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Kevin Yondan,  Athumani Iddi ‘Chuji’, Simon Msuva, Haruna Niyonzima, Frank Domayo, Didier Kavumbangu na Hamisi Kiiza/Niaar Khalfan.


No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...