https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Tuesday, May 14, 2013

Miss Tanzania 2012 Brigitte Alfred asisitiza malengo kwa warembo


Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
MISS Tanzania mwaka 2012, Brigitte Alfred, amewakumbusha wanaopenda kushiriki mambo ya urembo kuhakikisha kuwa wanakuwa na malengo kabla ya kujiunga kwenye tasnia hiyo duniani.
               Miss Tanzania 2012, Brigitte Alfred
Akizungumza jijini Dar es Salaam juzi, Brigitte alisema kuwa malengo ndio silaha ya kumuwezesha mtu kutimiza kile anachokihitaji katika kipindi cha maisha yake.

Alisema wapo mabinti wazuri na wenye sifa zote, ila wanashindwa kuendelea na kufika nafasi za juu kutokana na kutoweka malengo tangu mwanzo wanapojiunga kwenye sanaa hiyo ya urembo.

Brigitte ambaye anashikilia taji hilo kubwa la urembo Tanzania, alitumia muda huo kuwakumbusha washiriki na wasichana wanaotaka kuwa warembo kuhakikisha kuwa wanapigania ndoto zao.

“Mimi tangu mwanzo nilisema nakwenda Tanzania kushiriki Miss Tanzania, nikitokea Kenya ambako nilikuwa masomoni, jambo ambalo hakika nimelifanikisha kwa kiasi kikubwa.

“Wakati huu ambao naelekea kukabidhi taji kwa mrembo mwingine, naendelea na harakati zangu maana ukishaingia kwenye sanaa hii na kushika taji ni mwendelezo wa maisha mengine kwa kutumia mgongo huu ambao wengi wanautamani japo baadhi yao wanakosa malengo,” alisema Brigitte.

Brigitte kwa sasa anaelekea kukabidhi taji hilo kwa mrembo mwingine, hasa baada ya kinyang’anyiro cha kuelekea Miss Tanzania 2013 kushika kasi kutokana na sehemu mbalimbali kuandaa mashindano hayo ambayo baadaye yatahusisha mikoa, Kanda na baadaye fainali za Taifa zitakazofanyika jijini Dar es Salaam.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...