https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Monday, May 13, 2013

Mkuu wa Mkoa Kilimanjaro atoa maneno mazito kwenye kikao chake na wanahabari

Mkuu wa Mkoa Kilimanjaro, Leonidas Gama
AWALI ya yote, nimefarijika kupewa nafasi hii muhimu ya kufungua Kongamano hili la Tatu la Wanahabari na wadau wa Habari Mkoani Kilimanjaro

Ni matumaini yangu kwamba Kongamano hili limekutanisha waandishi wa habari na wadau mbalimbali kutoka hapa Mkoani na kila mmoja kwa nafasi yake ni kama sehemu ya familia moja katika kusukuma mbele gurudumu la maendeleo ya Mkoa wetu.

Ndugu  Mwenyekiti,
Ili kufikia lengo la kuinufaisha  jamii ya Wanakilimanjaro na Taifa kutokana na  huduma mbalimbali zitolewazo na taasisi tofauti, ushirikiano wa pamoja kati ya Serikali, Wafanyabiashara wa bidhaa na huduma, wananchi pamoja na vyombo vya habari ni jambo la msingi.

Ndugu  Mwenyekiti,
Napenda kutumia fursa hii kutoa pongezi kwa wanachama wote wa MECKI chini uongozi wa  mwenyekiti wa MECKI Rodrick Makundi na kamati nzima ya utendaji kwa kuwa mstari wa mbele kuhakikisha kuwa Klabu yenu inasonga mbele na kutekeleza majukumu yake kwa kufuata utaratibu mliojiwekea.

Kama mlivyoelezea malengo ya kongamano hili, naamini kongamano hili litafungua ukurasa mpya wa mahusiano yaliyoboreshwa baina ya wanahabari na wadau wengine kwa ujumla wake kwani kwa kipindi kifupi nilichokuwepo mkoani hapa nimeshuhudia mchango mkubwa wa vyombo vya habari katika kuisadia serikali kutekeleza vyema wajibu wake lakini pia kukosoa pale ilipokuwa inaonekana inafaa.  Kukosoa na siyo kulaumu au kulalamika.
Ndugu  Mwenyekiti ,
Kutafuta na kutoa habari katika nchi yetu ni haki ya kikatiba kama ilivyobainishwa na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 katika Ibara ya 18(b) inayompa uhuru Mtanzania kufanya shughuli zake katika tasnia ya habari.

Katiba yetu kupitia Ibara hiyo inatamka wazi kuwa kila mtu anayo haki kutafuta,kupokea na kutoa habari bila kujali mipaka ya nchi.

Napenda niwahakikishie wanahabari wa mkoa wa Kilimanjaro kuwa serikali ya mkoa wa Kilimanjaro inatambua kuwa kazi zinazofanywa na wanahabari ni kazi halali kwa mujibu wa Katiba na Sheria za nchi yetu.  Fanyeni kazi kwa kuzingatia weledi na maadili ya nchi yetu.
Hivyo napenda niwatie moyo kuwa mfanye kazi kwa bidii, kujiamini na uhuru kama wananchi wengine wanavyofanya shughuli halali katika mkoa wetu.

Ndugu  Mwenyekiti,
Katika nchi yetu kuna tatizo la watu kutumia vibaya nafasi walizonazo ambazo ni kwa ajili ya kuutumika umma badala yake wanazitumia nafasi hizo kwa maslahi yao wenyewe au kutumikia makundi ya wachache katika jamii. Napenda nieleweke kuwa tatizo hili limeshaanza kuingia katika tasnia muhimu ya habari jambo ambali kwa maoni yangu naona ni hatari kwa uchumi na amani ya nchi yetu.

Tasnia ya habari ina mchango mkubwa katika kustawisha maendeleo ya nchi katika nyanja zote muhimu kama itatumika vizuri kwa waandishi wa habari kusimama katika nafasi yao ya kuutumikia umma wa watanzania.

Lakini ikiwa kinyume chake tasnia ya habari itatumika kueneza uongo, fitina, chuki na uhasama kwa wananchi  jambo ambalo madhara yake kwa wananchi ni kukosa nafasi ya kufikiria namna ya kufanya kazi kwa bidii ili kupambana na umasikini, badala yake watabaki kunyosha vidole kwa kila mmoja kumuona mwenzie ni adui na si ndugu tena huku taifa likirudi nyuma baadala ya kusonga mbele.

Madhara makubwa ya ukiukwaji wa sheria na maadili katika uandishi wa habari ni kuingiza nchi katika machafuto, jambo ambalo litatugharimu kurudi nyuma katika maendeleo tuliyofikia, mipango tuliyojiwekea, rasilimali zetu na  maisha yetu.   Napenda niwatahadharishe kuwa wapo watu wasio penda mafanikio ambayo tumefikia.  Na wanaweza kuwatumia ninyi wanahabari kupotosha umma na hatimaye nchi yetu ikaingia kwenye machafuko.  Sote ni mashahidi na tumejionea jinsi vyombo kama hivi vilivyoweza kutumika katika nchi kama Rwanda na Burundi katika kuchochea fitina, chuki, mifarakano mikongoni mwa wananchi na hatimaye kusababisha machafuko yaliyogharimu upotevu wa mali na maisha ya watu.

Ni vyema wanahabari mkazingatia maadili ya taaluma yenu kwa kuhakikisha mnaandika habari za kweli na zilizofanyiwa utafiti wa kina, kwani kalamu ni sehemu ya silaha katika uwanja wa vita.
Ndugu  Mwenyekiti,
Nchi yetu ni ya kidemokrasia, na kila kwenye demokrasia ya kweli haki za msingi za binadamu zinazingatiwa na hakuna uhuru usio na mipaka. Napenda niwakumbushe wanahabari kuwa uhuru wa mtu unaishia pale unapoanzia uhuru wa mtu mwingine.

Uhuru wa habari unaelezwa wazi katika Ibara ya 18 (a) ya katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.   Ni kujua kuwa Katiba hii imeweka mipaka ya uhuru huo katika Ibara ya 16(1) inayompa mtu uhuru wa kuhifadhiwa nafsi yake, maisha yake pamoja na kuheshimiwa.

Ni matarajio yangu kuwa wanahabari wa Mkoa wa Kilimanjaro hamtaniangusha kwa kuandika habari bila ya kuzingatia sheria, haki za binadam na maslahi ya Mkoa na Taifa.

Ndugu  Mwenyekiti,
Tunaelekea katika kuandika katiba mpya ya Jamhuri ya Mungano wa Tanzania, huu ni wakati wenu kuwaelimisha wananchi mambo muhimu yanayopaswa kuzingatiwa na kuacha kushabikia masuala yanayoweza kupotosha mchakato mzima.  Wengi duniani hawajaweza kupata Katiba katika hali ya utulivi na amani. Nawapongeza wananchi wa Mkoa wa Kilimanjaro.

Msikubali kwa namna yoyote kuvuruga misingi imara iliyowekwa na waasisi wa Taifa hili, wakiongozwa na Hayati baba wa Taifa Mwl Julius Nyerere ambaye kwa kipindi cha uhai wake wote alihubiri na kuamini katika umoja na mshikamano miongoni mwa watanzania. 
Aidha waandishi wa habari si vyema kujiingiza katika misuguano isiyokuwa na misingi na baadhi ya taasisi bali ni nyema kila mmoja kwa nafasi yake akatimiza wajibu wake badala ya kuviziana kwa baadhi ya mambo.  





Ndugu  Mwenyekiti,
Pamoja na waandisi wa habari lakini pia ni wajibu wa wadau kuhakikisha kuwa wanatoa ushirikiano kwa wanahabari, kwa kuacha kuficha taarifa ambazo zinapaswa kuwafikia wananchi, kwani jambo hili limekuwa likileta msuguano baina ya wadau na wanahabari na kufikia hatua ya kuhatarisha mahusiano baina ya pande hizi mbili. 
Mara kadhaa tumemsikia Rais Jakaya Kikwete akisisitiza taasisi na ofisi za Umma kutoa habari kwa waandishi ili nao waweze kuihabarisha jamii kulingana na jambo husika

Ndugu  Mwenyekiti,
Nitoe  wito kwa  wadau wote wa habari mkoani Kilimanjaro, itumieni ipasavyo Klabu hii ya waandishi wa habari (MECKI) katika masuala yenu yanayohusu kuuhabarisha umma mambo mbalimbali, Watumieni waandishi wa habari kuuhabarisha umma, shirikianeni na wekeni wazi habari kwa maslahi ya umma kutegemeana na taraibu na sheria za uandishi wa habari.


Fanyeni kazi kwa karibu na Halmashauri zetu zote katika mkoa wetu kuripoti habari za maendeleo ya wananchi hasa wa vijini. Katika eneo ambalo serikali inatenga fedha nyingi za maendeleo ni halmashauri, hivyo basi habari zinazogusa maendeleo ya wananchi zipo katika halmashauri zetu.

Moja kati ya matatatizo yaliyomo katika jamii ni watu kutojua kinachoendelea hasa juhudi zinazofanywa na serikali na taasisi zingine katika kuwawezesha wananchi kujiletea maendeleo. Kama kuna kiongozi au mtumishi asiyetoa ushirikiano kwa waandishi mniambie.

Ndugu  Mwenyekiti,
Napongeza mpango wenu wa maendeleo uliopita na huu mliuiweka wa sasa. Wekeni mipango madhubuti ya maendeleo na utekelezaji wake.
Sitarajii kusikia suala la Sacoss likiwasilishwa kama mpango tutakapokutana katika kongamano lijalo. Nataka kusikia kutoka kwenu juu ya maendeleo ya Sacoss yenu. Mkiwa na uchumi imara mnaweza kufanya shughuli zenu kwa amani na kujiamini kutokana na nguvu za kiuchumi zitakazotokana na SACOSS yenu.


Tumieni kongamano hili kuelezana na kupanga utaratibu mzuri wa kufanya kazi na chombo hiki, na waandishi wa habari kwa ujumla, ili  taarifa zote za maendeleo ziwafikie wananchi kwa maslahi ya umma.

Mwisho, kubwa zaidi ni ninyi kama wadau kuwaona wanahabari kama sehemu ya jamii badala ya kuwaona ni maadui na wenye lengo la kuharibu sifa za taasisi zenu au kampuni.

Vyombo vya habari vinaweza kujenga kama mtavitumia vizuri lakini pia vinaweza kubomoa kama hamtaonyesha ushirikiano.

Baada ya kusema hayo natangaza rasmi kuwa Kongamano hili la Tatu la Wanahabari kuhusu Maendeleo ya Mkoa wa Kilimanjaro limefunguliwa rasmi.
 
Ahsanteni sana kwa kunisikiliza.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...