https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Saturday, May 18, 2013

Diwani wa Mswaha, wilayani Korogwe afanya shughuli za utoaji majini wilayani Muheza

 Mganga wa jadi Aweso Kipaku ambaye ni diwani wa kata ya Mswaha iliyopo wilayani Korogwe, akiwa ameshikilia kitu kinachodaiwa ni jini alilolitoa katika moja ya darasa la shule ya msingi Kwemsala iliyopo kata ya Mtindiro wilayani Muheza juzi, wengine aliyevaa fulana ya punda milia ni mwenyekiti wa kamati ya shule hiyo Shabani Hamisi.

Na Mashaka Mhando, Muheza
LICHA ya serikali mkoani Tanga kusikika ikipiga marufuku masuala ya utoaji uchawi katika sehemu mbalimbali za wilaya zake mkoani humo, lakini diwani wa Kata ya Mswaha, iliyopo wilayani Korogwe, Aweso Kipaku ambaye pia ni mganga aliendeleza shughuli hizo katika kijiji cha Kwemsala, wilayani Muheza mkoani Tanga, kwa madai kuwa shule ya kijiji hicho ilikuwa na imani za ushirikina. 

Akifanya kazi hiyo, juzi katika shule hiyo Diwani huyo aliyealikwa na kamati ya shule ya kijiji hicho, alianza kupita kila darasa la shule hiyo huku akionekana amepandisha mapepo yaliyokuwa yakimuongoza huku wananchi wa kijiji hicho wakijazana kuona kazi anayofanya diwani huyo.

Diwani huyo mara baada ya kukimbizana na vitu vilivyokuwa havionekani kwa macho, alipoingia kwenye ofisi inayokaliwa na walimu, alipiga kelele kutaka aletewe unga wa sembe, maji na kuku alipopata vitu hivyo, aliibuka na pembe kubwa iliyokuwa imefungwa vitambaa vyeupe na vyekundu.

"Wananchi hivi vitu vilivyotoa mnavyoviona ndivyo vilivyokuwa vikiwasumbua wanafunzi, lakini jini jingine kubwa limekimbia huko katika makazi...Kazi ya kupambana nalo nitaifanya kesho (Ijumaa iliyopita)," alisema diwani huyo huku akiwa amekishika mkononi.

Akizungumza na wananchi mara baada ya diwani huyo kutoa vitu hivyo, Mwenyekiti wa kamati ya shule Shaban Hamis alisema tatizo la wanafunzi kuanguka katika shule hiyo lilianza tangu mwaka juzi na walipoitisha mkutano wa kijiji, viongozi wa dini walisema wangefanya maombi kuwanusuru watoto hao, lakini hawakuweza kufanya maombi hayo.

"Tuliona watoto wetu wanaendelea kuanguka wakipelekwa hospitali wanelezwa wana matatizo ya kisaikolojia, lakini tukiwapeleka kwa waganga wa kienyeji wanatibiwa na kupona, tukaona ni vema tumlete mganga huyu Kipaku (Diwani) ili awanusuru watoto wetu," alisema mwenyekiti huyo.

Mwalimu mmoja shuleni hayo Sophia Msangeni, alisema tatizo la wanafunzi kuanguka limekuwa likisababisha kushuka kwa taaluma shuleni hapo hatua ambayo ilikuwa ikileta kero na usumbufu mkubwa mara inapotokea suala la watoto kuanguka ambapo kwa siku wanaanguka watoto 20.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...