https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Friday, May 17, 2013

Mkuu wa Kikundi cha matapeli wanaojifanya ni maafisa wa Takukuru anaswa jijini Mwanza na hirizi zake mfukoni

Mtuhumiwa Simon Jumbe anayetajwa kujifanya afisa wa Takukuru.
TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Mkoa wa Mwanza imefanikiwa kumnasa mtu mmoja ambaye anasadikika kuwa mkuu wa genge la watu wanaojifanya Maafisa wa Ofisi ya TAKUKURU Mkoani hapa.

Akitoa taarifa kwa waandishi wa Habari ofisini kwake Kamanda wa TAKUKURU Mkoa wa Mwanza Ayubu Akida alisema kwamba kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo aliyefahamika kwa jina la Simon Jumbe (32) lakini amekuwa akitumia majina mengie kwa kujiita Mapunda na SP ni kutokana na mtego uliowekwa na maafisa wake.
Kamanda wa TAKUKURU mkoa wa Mwanza Ayoub Akida, akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake leo.
“Tuliweka mtego huo kutokana na kuwepo taarifa za siri kutoka kwa raia wema ambapo walitueleza kwamba kuna wimbi la baadhi ya watu ambao wamekuwa wakiwadanganya watu kuwa wao ni maafisa na watumishi wa TAKUKURU baada ya kuweka mtego Mei 13 mwaka huu tumefanikiwa kumnasa huyu maeneo ya Kata ya Mkuyuni Wilayani Nyamagana” alisema Akida.


Kamanda Akida alieleza kwamba tangu mwezi April na Mei tumekuwa katika hekaheka za kuwatafuta watu hao baada ya taarifa za kuwepo watu hao wanaojitambulisha kuwa watumishi na wamekuwa akiwadanganya watu na kufanya kazi ambazo si za ofisi ya Takukuru ikiwa ni zile za Taasisi zingine za serikali.

Kamanda wa TAKUKURU mkoa wa Mwanza Ayoub Akida
“Katika kipindi hicho tuliweza kupokea taarifa za matukio kumi ya kutoka kwa watu waliotapeliwa katika Wilaya za Misungwi na Jiji la Mwanza ambapo baada ya kumnasa mtuhumiwa huyu na kumhoji alidai kuwa yeye peke kwa kutumia utapeli huo ameweza kujipatia kiasi cha shilingi milioni 4,637,000/= kutoka kwa watu kumi na mbili”alisema Kamanda.

Naye mmoja wa watu walioathirika na kutapeliwa aliyejitambulisha kwa jina la James Belindo mkazi wa Nyakato Buzuruga Wilayani Ilemela alisema kwamba alimfahamu mtuhumiwa kwasababu alikuwa jirani yake naye mtuhumiwa alitumia mwanya huo wa ujirani akimweleza kuwa kuna magari 12 yameletwa ofisini kwao yaani Takukuru hivyo kuna nafasi za kazi ambazo anaweza kumuunganishia.


James Belindo mmoja kati ya waliotapeliwa.
“Alidai kama nina ujuzi wa kuendesha gari yaani udereva basi nimwambie, nilimweleza sina lakini kuna jamaa yangu, naye akasema hamna tabu nimpeleke atakuwepo ofisi ya Takukuru Mkoa, akaomba vyeti na leseni kisha akamweleza kuwa inatakiwa kufunguliwa majarada matano na kuomba kiasi cha 475,000/- lakini hakupata kazi hiyo”alieleza kwa masikitiko.

Kamanda Akida amewatahadharisha wananchi kuwa makini na kundi la matapeli hao wanaojifanya watumishi wa Takukuru ambao wamekuwa wakiidhalilisha na kuipaka matope ofisi yake na kuharibu taswira iliyopo kwa jamii na kuwataka kufika ofisi za Takukuru na kutotoa fedha bila utaratibu wa taasisi hiyo.

Aidha alisema kwamba kutokana na kuwepo kundi hilo ofisi yake imewataka wananchi kuendelea kutoa taarifa za siri zitakazofanikisha kunaswa kwa watu hao ambao wamekuwa wakiwadanganya kuwatafutia kazi,kuwatisha ili wawapatie fedha kunyume na huduma zinazotolewa na ofisi za Takukuru Wilayani na Mkoa.


No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...