https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Monday, May 13, 2013

Siasa kwenye soka ndio mchawi wa maendeleo yetu Tanzania



SIWEZI KUVUMILIA
Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
NDIO hapo ninaposhangaa kuona waliokuwa kwenye nafasi za uongozi wanaona njia nzuri ni kuweka siasa kwenye suala zima la michezo, ukiwamo mpira wa miguu Tanzania.
Juma Kaseja, mlinda mlango wa Simba

Hili kwa kiasi kikubwa linasababisha mpira wa miguu uzidi kupumulia mashine kila siku, licha ya kuwa na wachezaji wazuri na wenye vipaji vya aina yake.

Hii siwezi kuvumilia kamwe. Kuna kila sababu ya wadau wa michezo wakiwamo wa mpira wa miguu kuacha tabia hiyo haraka iwezekanavyo kwa ajili ya maendeleo yetu.

Nasema hivi nikiangalia zaidi mfumo wetu. Mfumo ambao kuanzia kwenye klabu hadi kwenye Shirikisho la Soka nchini TFF ni siasa tupu zinazoendelea kufanywa.

Hii haiwezi kukaa sawa. Angalia, klabu ya Simba imekuwa chanzo cha kushindwa kuwika katika soka kutokana na siasa. Mwenyekiti wake Ismail Aden Rage wakati mwingine anashindwa kujibu hoja zenye mashiko, hasa wanachama wake wanapohoji yenye kuleta maendeleo.

Katika hilo, jibu kubwa analoweza kutoa mwenyekiti huyo ni kutangaza taratibu za muda mfupi, kama vile kujenga uwanja, licha ya kujua kuwa hakuna kinachoweza kufanikiwa.

Kwa miaka kadhaa sasa Simba ikiwa na viongozi tofauti tofauti imekuwa ni watu wa porojo. Porojo ninazofananisha na siasa, maana ndizo zinazotuharibia kila siku.

Sio Simba tu, ila hata Yanga, ndio wanayofanya kila siku, jambo ambalo linatakiwa liangaliwe upya kwa faida ya soka Tanzania. Wakati hayo yanakera kwa klabu zetu, TFF nao ndio aina yao ya maisha, kuweka siasa kusipowezekana.

Suala la Uchaguzi wa TFF liliingiwa na siasa za kutisha, hadi kufikia serikali kwa kupitia Waziri wa Michezo kuzuia Uchaguzi huo. Jambo hilo lilisababisha ujumbe kutoka Shirikisho la Mpira wa Miguu duniani kutua kuweka mambo sawa.

Kitendo cha kuja kwa watu hao, kumetoa majibu kuwa sisi hatuwezi kujiendesha bila wazungu. Na hiyo ni kwasababu tunapenda sana kuweka siasa hata pale pasipohitaji.

Leo hii ujumbe huo wa FIFA umetuma salamu na kutoa mwongozo wa Uchaguzi kufanyika baada ya kuweka mambo sawa hasa katika baadhi ya kanuni pamoja na kuundwa Kamati ya Nidhamu.

Kamati hii iliwahi kupigiwa kelele na wadau wa michezo, akiwamo Michael Wambura aliyekuwa akililia haki yake ya kuchaguliwa katika Shirikisho hilo nchini TFF.

Wambura alikuwa akiyalilia hayo kwasababu mapungufu yalionekana sambamba na kuwekewa siasa katika kila anapokwenda au kutaka kufanya kwa ajili ya kumkwamisha.

Ajabu ni kuwa leo hii kwasababu Wazungu wametangaza hayo yafanywe, TFF wanakubali. Kwanini? Hii inaonyesha jinsi Watanzania tusivyojitambua na kusubiriwa kupangiwa na Wazungu hata pale tunapoweza kufanikisha ya kwetu.

Hii haiwezi kuwa sawa hata mara moja. Lazima tukubali kuwa tumekwamishwa na tabia zetu za kupenda siasa hata pale pasipohitaji siasa kwa namna moja ama nyingine.

Huu ndio ukweli wa mambo. Kuna kila sababu ya kutambua kasoro zetu kama lengo ni kujenga na kuweka tija katika harakati zetu. Mpira ni kazi inayolipa fedha nyingi.

Watoto wa wenzetu wanachezea fedha nyingi kwa muda mchache, wakati sisi Watanzania hilo hatulioni na tumeona kuwa porojo ndio mahali pake na kubaki kama tulivyo.

Hii si njia nzuri hata kidogo. Ni wakati wa kutambua uozo wetu kwa ajili ya maendeleo ya soka Tanzania. Kwa bahati mbaya, wachache wao wanaposema ukweli, huonekana wazandiki.

Kila siku nimekuwa nikisema, muhimu ni kufahamu mtu alipojikwaa na sio kuangalia zaidi alipoangukia. Hatari hii itaendelea kuota mizizi kila siku ya Mungu, hata baada ya Rais Leodgar Tenga kumaliza muda wake na kurithi mwingine atakayechaguliwa.

Nchi za wenzetu wamefahamu makosa yao na leo wanasonga mbele, wakati sisi tupo kama tulivyo licha ya kuwa na watu wengi wenye vipaji kama vile Mrisho Ngassa, Juma Kaseja, Mwinyi Kazimoto, Nadir Haroub Cannavaro na wengineo wengi.

Ndio maana nasema ni wakati wetu wa kuacha siasa kwa ajili ya kufanya kazi kwa moyo ili tuendeleze soka letu kwa maendeleo yetu pamoja na Taifa letu kwa ujumla.

Kinyume cha hapo badala ya kwenda mbele tutarudi nyuma na hatuwezi kwenda mbele hata kama klabu zetu au vyama vyetu vya soka viongozwe na malaika.
0712 053949
0753 806087

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...