https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Thursday, May 09, 2013

Wadau, Serikali inamuangaliaje Francis Cheka



Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
NI mtoto tu anayesubiri kuungua kwa kuugusa moto kwa ajili ya kugundua kwamba unaunguza ama vipi. Ila kwa watu wazima wanaojitambua, hata kwa macho tu, wataweza kung’amua kilichopo mbele yake, pembeni yake ni moto na unapougusa madhara yake ni kuungua.
                                        Francis Cheka
Ila, inapotokea mtu mzima anashindwa kujua moto unaunguza ni ujinga, hivyo kila anayeweza kuwa kwenye mtazamo huo anastahili kuzomewa. Kinyume cha hapo siwezi kuvumilia.

Siwezi kuvumilia, hasa kila ninapoangalia kipaji cha mwanasumbwi, Francis Cheka anayetokea mkoani Morogoro kinaangaliwa ovyo ovyo tu. Kwa miaka zaidi ya mitatu sasa, Cheka ameweza kuwa juu na kupeleka kilio kwa kila bondia anayekutana naye ulingoni.

Kwa kuangalia hili tu, ni dhahiri kuwa Cheka ni bondia makini na anastahili kupewa ushirikiano kutoka kwa wadau wa ngumi. Kwa mfano, serikali pia inaweza walau kumjali bondia huyu kwa kuhakikisha kuwa anafanya safari kuelekea kwenye mapambano makubwa duniani.

Kwa bahati mbaya, serikali yetu imekuwa ikifanya mambo kiujanja ujanja tu. Hata Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo siku zote imekuwa ikifanya mambo ambayo si yenye kukuza michezo.

Angalia, kila kipaji katika Taifa hili kimeibuka kwa juhudi zake. Hakuna hata mmoja aliyetokea kwenye mikono salama. Ni tofauti na baadhi ya nchi zilizoendela duniani.

Kila siku mabondia wa Tanzania, wadau wao wamekuwa wakilia wimbo wa kukosa wadhamini wa uhakika. Licha ya kujaa kwa makampuni ya kila aina na taasisi za muhimu, lakini ni chache zinazojitokeza kudhamini mchezo wa masumbwi, japo kutoa Milioni moja au mbili.

Mapromota wa masumbwi ambao nao wanasumbuliwa na ukata, wanatumia muda mwingi kusumbukia fedha za kuandaa pambano, huku wakitarajia faida ya viingilio vya mashabiki.

Hakuna mipango wala ushirikiano hapa. Waswahili wana msemo wao, supu ya mbwa inanywewa ikiwa ya moto. Kutokana na hilo, Cheka akitumiwa vyema na wadau pamoja na serikali anaweza kufanya makubwa duniani katika sekta ya masumbwi.

Watu watauliza au kushangaa. Ndio, maana watakumbuka kuwa sio Cheka peke yake aliyewahi kutesa katika masumbwi hapa nchini. Ukiacha Said Kinyong’oli, pia alikuwapo Rashid Matumla, akitokea katika familia ya wacheza ngumi ambao hadi leo wanatamba.

Mwili wa Matumla ungeweza kutumiwa vyema, hakika angeweza kupanda ulingoni kushiriki mapambano makubwa duniani. Lakini hao wote waliwika kwa miaka michache na kupotea.

Naweza kusema sisi hatuna akili ya kuendeleza watu wenye vipaji kwa ajili ya maslahi ya Taifa. Tumebaki kuwa wapiga makofi na kushangalia ujuha wetu katika kila jambo hata kama halina tija.

Wakati huu, ni dhahiri kuwa kama Cheka hajajiweka sawa zaidi kwa juhudi zake, huenda baada ya miaka miwili au mitatu ijayo kutoweka. Hakika siwezi kuvumilia hata kidogo.

Ni wakati wetu sasa kukaa chini na kuangalia mwenendo wetu. Tumtangaze Cheka nje ya nchi pamoja na mabondia wetu wengine kwa ajili ya kupata mapambano makubwa na yenye soko.

Tutafate nafasi ya kujichomeka katika Mataifa makubwa, ili iwe njia nzuri ya kukuza na kuendeleza sekta ya masumbwi. Kwa sasa Cheka naweza kusema kuwa hana mpinzani Tanzania.

Atacheza na nani sasa? Kila anayeingia naye ulingoni anampiga kama mtoto wake wa kumzaa. Juzi, Thomas Mashali aliyejigamba sana, aliweza kutandikwa, huku Cheka akiwa anasumbuliwa na mkono.

Naamini huu ni wakati wa kuangalia mwenendo wetu kwa ajili ya kusonga mbele katika kona ya masumbwi. Ili aweze kutimiza malengo yake, inahitaji muda kidogo wa kujiandaa ili kuongeza uzito wake.

Huo ndio ukweli wa mambo. Kinyume cha hapo tuendelee na porojo zetu, mzaha wetu, huku vipaji vyetu vikizidi kutumbukia katika shimo la ufukara.

Tunaomba radhi kwa usumbufu, hasa kwa makala haya kukujia leo Alhamis badala ya Jumatatu kama ilivyokuwa kawaida yake.
 

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...