https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Saturday, July 13, 2013

Wasanii waache anasa, wajiwekee akiba ya maisha yao



Na  Kambi Mbwana, Dar es Salaam
SWALI linaloumiza vichwa mashabiki wengi wa sanaa, ni kwa nini wasanii wetu wanashindwa kumudu maisha au kuendelea kusimama walipo pindi wanaposhuka kisanaa.
Msanii Diamond akiwa jukwaani
Hii ni kwa sababu mara nyingi wasanii wetu wanaishi maisha ya leo, ambayo ni ya kitajiri kuliko kipato chao halisi, wakiweka mbele anasa bila kujipanga kwa ajili ya kesho.
Msanii Lady Jay Dee
Mathalani maisha anayoishi sasa msanii Nassib Abdul ‘Diamond’, si ajabu huko mbela ukasikia bado anapanga nyumba, baada ya kushuka kisanii.
Msanii Linah wa THT akiwa kwenye poziiiii

Msanii Mr Blue, akiwa kwenye pozi.
Leo hii Diamond anatajwa kama msanii anayeshika chati kwa kulipwa fedha nyingi, huku watu wakimtolea mfano kuwa msanii anayejituma kisanii kati ya wengine wanaofanya sanaa ya muziki wa kizazi kipya.


Ukiacha Diamond kwa sasa, wapo wasanii waliotesa mno miaka ya 2000 hadi 2011, maana hata shoo zao za muziki zilionyesha kuwa wao ni wakali na wana mashabiki wengi.



 Msanii Profesa Jay
Msanii Ray C akiwa kwenye pozi la aina yake.
Tangu kushika kasi kwa muziki huu wa kizazi kipya, wasanii wetu ili wapate fedha nyingi wanategemea upatikanaji wa shoo, tofauti na zamani ambapo walitegemea mauzo ya albam.

Wapo ambao hawakutegemea mauzo ya albam na walikuwa na malengo ndio ambao hadi leo tunawaona wamweza kumudu maisha yao hata baada ya kushuka kisanii.

Wasanii kama Juma Kassim ‘Nature’, Joseph Haule ‘Profesa Jay’, Lucas Mkenda ‘Mr. Nice’ na Saida Kalori, hawa walikuwa wakiingiza fedha nyingi sana katika shoo zao.

Bado wasanii kama vile Judith Wambura ‘Lady Jay Dee’, Rehema Chalamila ‘Ray C’, Selemani Msindi ‘Afande Sele’, Hamis Mwinjuma MwanaFA, Amwene Yessaya ‘AY’ na wengineo waliishi kama wafalme kutokana na umahiri wao kisanaa.

Hao ni wachache tu kati ya wengi waliovuna fedha za muziki huu, japo leo baadhi yao wapo wapo tu mitaani wakiwa hawana cha maana.

Maisha yao yamezidi kuwa magumu na kubaki historia tu ya majina yao, ambayo siku hizi huwa yanarudi kwenye chati baada ya kufariki dunia.

Hii ni ajabu mno na ndio maana msanii Ommy Dimpoz alipoamua kusema  kuwa wasanii wanakufa masikini, akitolea mfano wa Albert Mangweha ‘Ngwair’, wengi walishindwa kumuelewa.

Ni Tanzania tu ambapo msanii anapoupinga umasikini kwa kuangalia walioshindwa kuwa matajiri licha ya vipaji vyao, jamii inamchukia na kumuona ana dharau.

Haya ni kwa uchache tu, lakini si ajabu yakatokea mbele, pale wasanii wanaowika leo kama vile Ommy Dimpoz, Barnabas, Linah, Mwasiti na wengineo eti kufa masikini.

Kwa mtu kama mimi wala sitashangaa, maana wengi wao wanaishi maisha ya kuigiza, wakitaka kujionyesha wao ndio kila kitu na kushindwa kuweka akiba katika maisha yao ya baadaye.

Ni kweli kuna changamoto nyingi kama wanavyosema wengine, lakini kwa msanii kuingiza Sh milioni moja ya shoo yake na kuimalizia disko bado atakuja kulaumu kuibiwa haki zake?

Tunawaona jinsi wanavyoshindana kununua magari na kunywa vileo, wengine wanafika mbali zaidi kwa kujiingiza kwenye utumiaji wa dawa za kulevya.

Ajabu, utumiaji huo wa dawa za kulevya kwa wasanii unatafsiriwa kama kuathirika kisaikolojia, baada ya kutumiwa bila faida na wanaotajwa kama wadau wakubwa wa muziki wa kizazi kipya hapa nchini.

Inaweza kuwa kweli, ila lazima tujue kuwa wasanii wengi wa Tanzania wanapenda maisha ya kuigiza.

Wasanii wengi wa kizazi kipya wanaona ili aonekane maarufu, ni lazima ajiingize kwenye dawa za kulevya ambazo huharibu mpangilio mzima wa maisha yake.

Hili lazima wasanii wenyewe waliangalie upya kwa ajili ya maisha yao, wajaribu kuweka akiba kwa kidogo chao wanachopata.

Tusipokuwa makini tutaendelea kuwa watu wa malalamiko yasiyokuwa na mpango wowote, wakati wenyewe wanashindwa kutambua mbinu za kuwapa maisha bora.

Ikumbukwe kuwa, si wasanii wote wanaoweza kulinda maisha yao yasishuke kisanaa, ukiacha wasanii wachache waliofanikiwa kubaki kama walivyo, wengi wao wamepotea.
Kupotea huko kunakwenda sambamba na ugumu wa maisha, hivyo nitashangaa ugumu wao kulaumiwa mtu mwingine, wakati yeye angeweza kufanya lolote kwa ajili ya maisha yake kwa ujumla.
Nadhani huu ni wakati wao sasa kukaa na kuangalia mbinu za kuboresha maisha yao, sambamba na kuacha starehe zisizokuwa na mpango, ukiwapo ulevi wa gharama kubwa na kuharibu maisha yao.

Tusipokuwa makini, hata huyu Diamond anayeonekana anazo fedha kwa sasa, kesho atashusha lawama kwa wadau, wakati ameshindwa kujipanga mwenyewe, maana waswahili wamesema ikiwama mulika.
+255 712 053949



No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...