https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Saturday, July 06, 2013

MAMBO FULANI MUHIMU: Kuzoeshana pesa kunaweza kuvuruga upendo wa kweli



Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
NI jambo la kumshuruku Mungu kuona anaendelea kutupigania kwa kutubariki kila jema na kusukuma gurudumu la maisha yetu.
Picha ya wawili wapendanao
Hakuna anayepaswa kushukuriwa isipokuwa yeye, maana kila tunalofanya hapa chini ya jua kunatokana na mazuri yake na upendo wake kwa binadamu wote duniani.

Na kwa wale wanaosumbuliwa na matatizo ya hapa na pale, pia ni mipango yake hivyo badala ya kumkufuru tutaje jina lake mbele kwa kuwa ndio kila kitu katika maisha yetu.

Baada ya kusema hayo, leo napenda kuzungumzia matatizo ya baadhi ya wapenzi wanavyoweza kujichanganya kwa kuzoeshana pesa kama karata ya kuwafanya waishi kwa amani tele.

Si vibaya kupeana pesa au thamani nyingine, ila inapotokea huna si lazima ufanye kila uwezalo, ikiwapo kukopa au kukwapua kwa ajili ya kuwaridhisha wapenzi wetu, hata kama tuwapende kiasi gani.

Katika Dunia ya leo, kitu kinachoongoza kuwatenganisha watu kwenye mapenzi yao basi suala la pesa linashika nafasi ya kwanza. Hizi ndio zinazoweza kufanya kila kitu, hivyo wachache wao kujikuta wakifarakana.

Ndugu msomaji wangu mpendwa, hupaswi kutanguliza pesa kwa mtu wako, hasa unapoanzana naye katika uhusiano wenu. Jifanye kama huna, ili ufahamu uhalisia wa huyo unayetaka kuwa naye.

Kwanza wapenda hela wengi wao hawawezi kuvumilia njaa, lazima atafanya vituko akiamini huna cha kumhonga. Huyo yupo kimaslahi zaidi. Anaangaliaa fedha ili ajikimu katika maisha yake.

Nasema hivyo kwasababu kama utatanguliza pesa na kufanikiwa kuwa naye, kesho anaweza kukuacha kama mtoto yatima utakapopunguza huduma kwake, maana amefahamu wewe ndio ATM yake.

kIla anachotaka kwako unampa. Tena zile anazotaka na wakati mwingine kwa ujinga wako unamuongezea mara mbili yake. Kwa bahati mbaya, kesho unaingia kwenye mgogoro wa kifedha, unalazimika kupunguza au kusitisha kabisa kumpa pesa kama ulivyomfanyia mwanzo.

Suala hilo haliwezi kumfurahisha hata kidogo. Lazima ajuwe umesitisha kwasababu umemchoka. Kama hivyo haitoshi, wengine huamua kuangalia upande mwingine, kwa wenye fedha zao.

Hilo ni tatizo kubwa linaloanzisha mfarakano katika uhusiano wa kimapenzi, hivyo wakati mwingine kuwatenganisha wawili hao. Angalia, licha ya kutumia gharama zako nyingi kwa mtu huyo, awe mwanamke au mwanamume, lakini unaachana naye na kila mtu kuangalia maisha yake.

Ni kama vile ulimaliza kuni kwa kuchemsha mawe. Hupaswi kuishi hivyo na mtu unayetaka kuanzisha naye uhusiano wowote, ukiwapo ule unaoweza kuzalisha ndoa kama wanavyofanya vijana wa leo.

Nadhani huu ni wakati wetu kujua kuwa si lazimaa tutangulize fedha kwa wale tunaohitaji kuwa nao kimapenzi. Tunaweza kuwafanyia kila kitu, sambamba na kuwanunula magari, lakini wasituweke moyoni.

Wanasema upendo wa kweli unatoka moyoni. Kujikweza, kujifanya tunazo fedha ni njia za kutumia gharama ambazo si muda wote zinaweza kutuletea amani, hasa pale tutakapoingia kwenye hatua mbaya za kiuchumi.

Pale tutakaposhindwa kupata fedha za kuwapa wapenzi wetu kama tulivyowazoesha awali, hivyo tuliangalie suala hili kwa kina kwa ajili ya kutufanya tuwe na amani moyoni.

Tusipokuwa makini, tutaweka mbele pesa ili kuwaridhisha wapenzi wetu, huku wao wakiwa wepesi kutumia nguvu zetu na kuwapatia wale wanaowapenda kwa dhati na kuharibu mpangilio mzima wa maisha yetu.

Tuzinduke na kuishi kama Mungu alivyotujalia na hakuna haja ya kutumia nguvu kubwa kuwapatia pesa watu, ingawa sio vibaya kuwapa chochote kitu watu wetu kwa namna moja ama nyingine.

Nawatakia Mfungo mwema wa Ramadhan Waislamu wote duniani, hasa wale watakaojaliwa kufunga katika siku za hivi karibuni.
0712 053949
0753 806087

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...