https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Sunday, July 21, 2013

Pikipiki yaua wawili Handeni, mmoja yupo mahututi Hospitali ya wilaya Korogwe


Na Mwandishi Wetu, Handeni
PIKIPIKI inaendelea kupeleka huzuni majumbani mwa watu hapa nchini, baada ya jana saa moja za jioni katika kijiji cha Komsala, wilayani Handeni mkoani Tanga, kutoa roho za vijana wawili na mmoja kuwa mahututi.
Pikipiki zinavyotoa roho za Watanzania. Hii sio iliyopata ajali iliyokuwa kwenye habari hii. Imetumika kama mfano tu.
Aliyetajwa kufariki katika ajali hiyo iliyotokea eneo la Changalawe, katika kijiji hicho cha Komsala, ni Vitalis William anayejulikana kwa jina la ‘Kihiyo’ na mwingine ambaye hadi sasa hajafahamika.

Ajali hiyo imedaiwa kuwa ni kutokana na mwendo wa kasi, ambapo pikipiki iligongana uso kwa uso na mwendesha baiskeli anayetokea kijiji jirani na hicho, akijulikana kama jamii ya wafugaji.

Majeruhi wa ajali hiyo ametajwa ni mkazi pia wa Komsala, anayejulikana kwa jina la Mambo, anayejishughulisha pia kwa kazi ya uendeshaji wa Bodaboda, moja ya vitu vinavyotoa angamiza roho za watu wengi.

Mashuhuda wa ajali hiyo ambao hata hivyo hawakupenda kuyataja majina yao, walikiri kuona ajali mbaya katika maisha yao, huku majeruhi akiwa katika hali mbaya zaidi.

Majeruhi hiyo kwa sasa yupo katika Hospitali ya wilaya ya Korogwe akipewa matibabu, wakati kwa waliokufa hasa Kihiyo yeye taratibu za mazishi nyumbani kwao zimeanza kufanyika.

“Yule majeruhi yupo kwenye hali mbaya mno maana kila aliposhikwa alisikika akilalamika maumivu, hivyo kwa sasa yupo hospitalini, ambapo Kihiyo ambaye pia wamekuwa na ukaribu mno akiwa ni marehemu,” alisema mpashaji huyo.

Kamanda wa Polisi mkoani Tanga, Costantine Massawe, amesema kuwa taarifa hizo zimefika ofisini kwake na upelelezi zaidi unaendelea kufanyika juu ya tukio hilo.

“Ni kweli tumepata taarifa za msiba huo uliotokana na ajali ya pikipiki katika kijiji cha Komsala, wilayani Handeni mkoani Tanga,” alisema Massawe kwa njia ya simu.

Ajali za pikipiki ni miongoni mwa matukio yanayosababisha vifo vya watu wengi, huku taarifa zikiripoti kuwa mara nyingi zimesabishwa na mwendo wa kasi wanapokuwa barabarani.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...