https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Monday, July 15, 2013

SIWEZI KUVUMILIA: Victor Wanyama, ni funzo kwa wachezaji wetu Tanzania


Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
WADAU wa soka nchini Kenya wapo kwenye shangw za aina yake, baada ya Victor Mugabe Wanyama kusajiliwa kwenye klabu ya Southampton ya Uingereza kwa Paundi Milioni 12.

Mrisho Ngassa, nyota wa Yanga na Taifa Stars
Wanyama ametokea katika klabu ya Celtic ya nchini Scotland, huku akifanikiwa kuwapa imani watu wa Kenya kuwa atafika mbali katika maisha yake ya soka.

Hii si furaha kwa watu wa Kenya tu, ila Afrika nzima tunawajibu wa kumuombea mchezaji huyo ili afike mbali zaidi katika maisha yake ya soka duniani.

Amefanya vizuri huku kujituma kwake hatimae kukimpeleka katika soka lenye ufundi na ushindani wa aina yake nchini Uingereza.

Nikiacha kumuangalia nyota huyo na mafanikio yake, kiu inanijia kuwageukia wacheza soka wa Tanzania. Hawa ambao hamu yao kubwa ni kwenda na kurudi katika timu za nyumbani.

Raha yao kubwa ni kusajiliwa Simba ama Yanga, bila kuangalia mbele, licha ya kufahamu utajiri mkubwa unaoweza kupatikana endapo watacheza soka la kulipwa.

Kumekuwa na kasumba za aina yake Tanzania. Wapo wachezaji wanaojiweka nyuma kujiandaa ili wafikie malengo yao. Mchezaji anakosa ratiba kamili ya mazoezi.

Mchezaji wa Tanzania hata kama ana uwezo, ila anajinyima kula, ama kuwa mwepesi kutega mazoezi yake. Wapo wachezaji ambao kila siku ni wategaji, wakisingizia kuumwa.

Mchezaji wa aina hiyo kufika malengo ya soka la Kimataifa ni ndoto, hata kama awe vipi. Kwa mfano, mchezaji kama Mrisho Ngassa licha ya kuonekana ni hodari Tanzania, ila kwenye soka la Kimataifa hana nafasi ya kucheza huko.

Akiingia kwenye vipimo anaonekana ni mwepesi. Makocha wenye kuangalia ubora, ni wazi atamuona hafai, hivyo kurudi tena Tanzania kwa ajili ya kucheza Simba au Yanga.

Na ndio maana kila siku tunawaona wanavyoona furaha kwenda Yanga kusajiliwa Simba, bila kujua kuwa wanavyoendelea kung’ang’ania soka la Tanzania, maendeleo yao yanachelewa.

Hakika siwezi kuvumilia. Siwezi Kuvumilia kuona kila siku, wachezaji wetu wa Tanzania wanashindwa kuwa na mbinu zenye kuwafikisha mbali ili iwe sehemu ya maendeleo yao.

Kwanini wachelewe? Je, lini watajiandaa kucheza soka la kulipwa? Ni lini wachezaji wetu watajenga miili yao kwa kujisimamia imara katika mlo na mazoezi?

Nadhani ni wakati wao sasa kuinuka na kuona wamekalia noti kwa kushindwa kujituma na kusaka namba Ulaya. Tunao wachezaji wengi wazuri na wakijiwekea mikakati watafika mbali.

Na wachezaji wa Tanzania lazima wajuwe kufika timu zinazocheza ligi Kuu Uingereza au Italia si jambo rahisi. Haiwezi kutokea kwa Mrisho Ngassa, Juma Kaseja, Mwinyi Kazimoto kulala na kuamka ameitwa katika timu za Mataifa hayo.

Hata kama wakiitwa huko, basi itawalazimu kuanza katika ligi ndogo, maana katika soka ni jambo la kawaida. Nadhani wacheza soka wa Tanzania waongeze bidii.

Vijana kama vile Mbwana Samatta, Thomas Ulimwengu, Henry Joseph Shindika na wengineo wanaocheza soka la kulipwa nje ya nchi waongeze bidii ili wafike mbali.

Ndio mpango unaoweza kuitangaza Tanzania katika soka la Kimataifa, ukizingatia kuwa sasa Kenya kwa kufanikiwa kuwa na nyota anayecheza soka nchini Uingereza, watu wengi watakuwa wanaiangalia nchi hiyo pamoja na wachezaji wao.
0712 053949

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...