https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Monday, July 22, 2013

Lushoto ni wilaya nzuri, ila madereva wake wakemewe kwa kupenda kuendesha mwendo wa kasi



KUTOKA Mombo kwenda wilayani Lushoto mkoani Tanga kwa wale wasiofahamu ni milima yenye mabonde. Ukiwa juu unaona chini kuko mbali kiasi cha kuwafanya wengine waogope.
 Wananchi wakifanya juhudi kulichomoa gari hilo lililotaka kutumbukia kwenye korongo baada ya mwendo wa kasi kumshinda dreva wake.
 Hili gari aina ya fuso lilikuwa likichungulia korongo likitazama kuanguka, baada ya mwendo wa kasi kumshinda dreva wake Lushoto vijijini. Kama lingeanguka sidhani kama kingetoka kitu katika gari hili.
 Ukiwa juu kabisa, tena ndani ya gari, ukiangalia chini utaona hali hiyo katika maeneo ya wilayani Lushoto, mkoani Tanga. Ni sehemu nzuri, ila asilimia kubwa ya madereva wanapokuwa safarini wanakimbiza magari yao. Serikali ikemee.
Wananchi hawa walikutwa kando ya barabara wakijadili jambo, katika vijiji vilivyopo wilayani Lushoto, mkoani Tanga juzi.

Barabara pia ni nyembamba yenye kila kitu cha kuogopesha kama vile makorongo na mawe katika baadhi ya maeneo. Hata hivyo hali hii si sababu ya kuwafanya madereva wengi wakimbize magari yao.

Wenzangu na mimi waoga nashika roho zao mkononi. Wengine wanatapika kwa woga kutokana na kona nyingi sambamba na mwendo wa kasi. 

Kutokana na hilo, wale madereva wasiojua barabara hii ya kwenda Lushoto wakifika Mombo wanawapa wenyeji waendeshe.

Hili si tatizo hata kidogo. Na ingawa wilaya ya Lushoto haina historia ya ajali, lakini ni wakati sasa wa serikali kuwaambia madereva hao waendeshe kwa ustaarabu.

Wapunguze mwendo maana kinga ni bora kuliko tiba. Ingawa hakuna ajali za mara kwa mara, lakini kwa barabara za Lushoto inapotokea ajali hiyo hakuna kinachopona.

Handeni Kwetu ilifanya ziara katika wilaya Lushoto na kujionea mengi mazuri. Ila juu ya mwendo wa kasi lazima lifanyiwe kazi na wahusika, hasa usalama wa barabarani.

Jambo jingine licha ya barabara kuogopesha na mwendo kuwa wa kasi sana, ila hakuna askari wa barabarani. Yupo mmoja tu karibu na maeneo ya Mombo lakini njia nzima hakuna hadi kufika Lushoto mjini.

Nadhani suala halijakaa sawa. Mungu ibariki Tanzania.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...