https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Wednesday, July 17, 2013

MGODI UNAOTEMBEA:Mwendo huu wa Chadema ni mbeleko ya CCM


Na Kambi Mbwana, Handeni
KUAMINI ni tendo la hiyari. Ila ni wazi kuwa mwendo huu wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), juu ya siasa za Tanzania inajiweka kubaya.
Mwenyekiti wa Chadema Taifa, Freeman Mbowe
Hili ukilisema wapo watakaobisha. Watavaa vibwaya kuporomosha matusi kadri ya uwezo wao. Hao ni wale wasiopenda kuambiwa ukweli. Wakiambiwa wanachukia.

Hata hivyo, ukweli siku zite unauma lakini unasaidia kumuweka mtu huru na lazima tujuwe kuwa kuamini ni tendo la hiyari. Leo hii ambapo baadhi yao wanaamini Chadema ndio kila kitu, ukiwaambia juu ya njia mbaya wanayopita ni ngumu kukuelewa.

Ni wazi Chadema kwa sasa ndio Chama Cha upinzani katika siasa za Tanzania Bara. Nasema Tanzania Bara kwakuwa chama hicho kinachoongozwa na mwenyekiti wake Freeman Mbowe, upande wa pili wa Muungano, yani Zanzibar hawana chao.

Kule hakuna anayeiamini Chadema. Ingawa Wazanzibar wengi hawaiamini Chadema kwa sababu za kidini, ila hata mwenendo wao wenyewe, kuangalia sana Kanda ya Kaskazini kunasababisha kuibua maswali kama wengine wanawajitaji.

Katika Uchaguzi Mdogo wa Jimbo la Chambani, uliofanyika mjini Zanzibar ambapo Chama Cha Wananchi CUF kiliibuka mshindi kwa mgombea wao kinyang’anyiro hicho cha Ubunge, Chadema waliambulia kura 11 tu.

Katika hali ya kushangaza zaidi, chama kipya ambacho hakina hata mwaka mmoja, yani ADC, chenyewe kilipata kura 112, ikiwa ni ishara kuwa katika visiwa hivyo Chadema hawana chao.

Katika mchanganuo wa kura hizo katika jimbo la Chambani, Chama Cha Mapinduzi CCM wenyewe walipata kura 202, wakati CUF wao 2708 na kunyakua jimbo hilo.

Sio Zanzibar tu, ila katika sehemu nyingi za Tanzania Bara, pia Chadema haijulikani na haina heshima. Hii ni kwasababu sera na mpangilio wao haueleweki.

Wanachoweza wao ni kubuni matamko yasiyokuwa na mashiko kwa Watanzania wote, ukiacha wale waliokuwa katika Mkoa wa Kilimanjaro, Arusha, Mbeya Mjini na baadhi ya maeneo wanapokubalika.

Wajuzi wa mambo ya siasa wanajua kuwa ili chama kifanikiwe kushika dola, walau kinastahili kuungwa mkono na watu wengi. Chama kinachojulikana Tanga tu na kuheshimiwa, kamwe haiwezi kuwa njia ya kuwapatia Dola.

Wakati haya yanaendelea kutokea, Chadema wanajikuta wakiubua maswali yasiyokuwa na majibu. Viongozi wao wa chama na serikali mtazamo wao unasua utata.

Kwa mfano, mara baada ya kutokea mlipuko wa bomu uliosababisha vifo vya watu watatu katika Mkutano wa Kampeni za udiwani uliofanyika jijini Arusha, Mbowe kama Mwenyekiti alitangaza kuwazuia wabunge wake kuingia bungeni.

Lengo la Mbowe lilikuwa ni kuwataka wabunge hao washiriki mazishi ya wafuasi wao waliokufa kwa mlipuko wa bomu. Mazishi ambayao Chadema walijua kuwa walitakiwa wasiandamane au kuaga kwa makundi kwasababu za kiusalama.

Kwakuwa wanajua mtaji wao ni propaganda chafu dhidi ya wananchi na serikali yao iliyopo madarakani, Chadema waligoma. Wakaamua kufanya wanavyotaka wao.

Hii ilisababisha kuzua mgogoro baina yao ni Jeshi la Polisi. Jeshi ambalo kila siku ya Mungu Chadema wamekuwa wakitoa lawama, wakiwadhihaki na kuwatusi pia.

Mara kadhaa tunasikia Jeshi la Polisi likitwa PoliCCM. Maneno mengi dhidi ya walinzi hawa wa raia na mali zao yanatoka katika vinywa vya watu wanaojipambanua kuwa wanahitaji kuwaongoza Watanzania.

Huu sio mpango mzuri. Ili Watanzania waendelee kuwa na heshima na vyama vya siasa, ni wazi Chadema kama Chama Kikuu cha upinzani Tanzania Bara, lazima kijisahihishe.

Kabla ya kuzungumza jambo, lazima wakae na kufanyika tathimini. Huu ndio ukweli wa mambo.

Kinyume cha hapo Chadema wataendelea kuwagawa wananchi, huku wale wanaowaunga mkono pia wakitafakari uwapo wao. Kwa mfano, Chadema kwa kupitia kikao cha Kamati Kuu kimetangaza kuwafundisha vijana wao namna ya kujilinda.

Hii ndio kusema kuwa Chadema wameona jeshi halali la Tanzania limeshindwa kuwalinda. Ingawa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imekataza vikundi vya namna hiyo, kikiwamo hiki cha Red Brigade kilichotangazwa na Chadema.

Wataalamu wa mambo wanahisi kuunda vikundi vya aina hii ni kuzalisha chuki na machafuko. Kwa Chadema ambao wamekuwa wakilalamikia jeshi la Polisi kesho vijana wao hawatafanya fujo?

Leo hii wakiwa wakomavu na mafunzo hayo hawatawarushia mabomu askari wetu? Haya ni maswali yanayotakiwa yajibiwe na kila Mtanzania juu ya siasa za Tanzania, hususan Chadema.

Chama ambacho dhamira yao inaweza kuyeyuka kama watashindwa kujiweka sawa. Mwendo wao si mzuri. Kauli zao nyingi inaonyesha inatoka bila kufanyiwa uchunguzi.

Kwa mfano, Chadema wao waliweza kususia vikao halali vya Bunge kwa kisingizio cha mazishi ya wafuasi wao. Mbaya zaidi, waligomea katika Bunge la Bajeti.

Bunge ambalo tangu lilipomalizika, tayari kumekuwa na matokeo magumu ya kupandishwa kwa kodi katika baadhi ya huduma, zikiwapo za simu za mikononi.

Leo hii Mtanzania ambaye hata kula yake haijulikani, bado atapaswa kulipia kiasi cha Shilingi 1,000 kwa namba yake (simcard). Hii ni kodi tofauti na gharama nyingine za muda wa maongezi ambazo zimepanda mara dufu.

Ingawa wabunge wa CCM wapo wengi bungeni, wakifikia 245 tofauti na wale wa upinzani hususan Chadema, ila kuwapo kwao kungesaidia kuibua hoja katika mrejesho wa hutuba ya Waziri wa Fedha, Dk William Mgimwa na wataalamu wake.

Kitendo cha uwapo wao, huenda kingezindua zile hoja zenye mashiko na Watanzania wote. Lakini waligoma kuingia kwasababu ya Arusha, wabunge wao wote wakiwapo huko, bila kujua kuwa Tanzania ina mikoa mingine inayohitaji uwapo wa wapinzani.

Bado kuna mikoa kama vile Mwanza, Geita, Morogoro, Tanga, Ruvuma, Pwani na mingineyo, hivyo si vizuri pia kwa chama hiki kuangalia zaidi Kanda ya Kaskazini.

Aidha tunahitaji hoja zaidi badala ya kupayuka maana huko kunaoanyesha mapungufu ya hadharani kabisa. Kwa mfano, katika makala yangu ya Mbunge wa Mbeya Mjini kwa tiketi ya Chadema, Joseph Mbilinyi Sugu, nilipinga kumuita Mpumbavu Waziri Mkuu Mizengo Pinda.

Wapo waliokosoa na waliosifia pia. Katika makala ile, nilijaribu kusisitiza wanasiasa wetu, viongozi wetu kupenda kuweka hoja badala ya mihemko isiyokuwa na tija.

Huu ndio ukweli. Hivyo hata hili suala la Red Brigade la Chadema linaweza kuwa baya zaidi kama litatumiwa tofauti. Chadema lazima wajuwe wana kila sababu ya kuilinda amani ya nchi yetu.

Sioo Chadema tu, ila vyama vyote vya siasa vinastahili kupigania amani maana ndio msingi wa maendeleo. Leo hii kama kila mtu ataweza kuunda vikosi anavyojua mwenyewe tutasababisha mwingiliano na machafuko yasiyokuwa na mpango.

Shughuli za ulinzi wa Taifa letu tushiriki kwa pamoja, ila zaidi jeshi la Polisi lina imudu zaidi kazi hiyo. Muhimu ni kuwapa moyo na kuwapa ushirikiano pia.

Hakuna haja ya mwanasiasa kutoa maneno ya kejeli kwasababu Dola ipo chini ya CCM. Tusipokuwa makini na kufanya siasa za kuvumiliana, hata kesho Chadema wakiingia Ikulu au ama CUF basi machafuko, lawama za mtindo huo zitashika kasi.

Angalia nchini Misri. Mwaka jana wananchi waliweza kuandamana kushinikiza rais wao Hosni Mubarak ajiuzulu. Walifanikiwa. Mubarak alitoka na uchaguzi huru wa kwanza kufanyika.

Lakini wakati watu wakiwa hawajui kinachotokea, wananchi hao hao tena wanaingia barabarani kumtaka rais wao Mohamed Morsi ang’oke kwa madai kuwa ameshindwa kuliongoza Taifa hilo.

Pia wakafanikiwa, hasa baada ya jeshi kumsaliti na kumuengua. Hii ni ishara kuwa hata Tanzania hayo yanaweza kutokea. Kama wananchi watafundishwa kufanya vurugu, maandamano, matusi na kejeli dhidi ya serikali au jeshi, basi hata kama Chadema wakiingia Ikulu, mtindo huo utaendelea kushika kasi.

Ni vyema tukajifunza katika hili. Tanzania tunakabiriwa na changamoto nyingi has azan ugumu wa maisha. Ni vyema basi tukatumia muda mwingi kuwaza namna ya kujiletea maendeleo na sio kupanga namna ya kulisumbua Taifa kwa namna yoyote ile.

Ni wakati wa wanasiasa wetu kutumia busara na siasa za uvumilivu ili iwe nafasi ya kujiletea maendeleo. Vyama vya upinzani kama kweli vinahitaji kuwakomboa Watanzania kama wenyewe wanavyosema, wasimamie kwanza katika suala zima la amani yetu inayoelekea ukingoni, ukizingatia kuwa kaatika siku za hivi karibuni, kumekuwa kukitokea matukio ya kuogofya, hasa ya utekwaji na uteswaji.
+255 712 053949

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...