https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Saturday, June 15, 2013

Wadau waendelea kumlilia Langa Kileo, kuzikwa Jumatatu


Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
CHAMA Cha Muziki wa Hip Hop Tanzania (TUMA), kimetuma salamu ya rambirambi kufuatia kifo cha msanii wake Langa Kileo, aliyefariki juzi katika Hospitali ya Taifa Muhimbili na kuibua machungu upya kwa wapenzi wa muziki huo nchini.
Marehemu Langa Kileo enzi za uhai wake.
Wiki iliyopita, wadau wa muziki wa Hip Hop walimpoteza Albert Mangweha ‘Ngwair’, aliyezikwa katika makaburi ya Kihonda mjini Morogoro, huku mapema wiki hii msanii wa filamu, Jaji Khamis Kash alifariki Dunia na kuleta hofu katika ulingo wa sanaa hapa nchini.

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Tanzania Urban Music Association (TUMA), Fredrick Mkoloni, alisema kuwa Tanzania imempoteza msanii mwingibne mwenye uwezo wa juu katika uimbaji wa muziki wa Hip Hop.

Alisema kwasababu hiyo, TUMA wapo mstari wa mbele katika kipindi hiki kigumu cha mfululizo wa vifo vya wasanii Tanzania, ambapo pia wamewataka wadau, mashabiki na wasanii kwa ujumla kumuombea marehemu ili akapumzike kwa amani.

“Huu ni wakati mgumu kwa Watanzania wote baada ya Langa naye kufariki Dunia, hivyo tunaomba ndugu zetu tushirikiane katika kipindi hiki kigumu cha kuondokewa na ndugu yetu, ikiwa ni siku chache baada ya kuzikwa Ngwair mkoani Morogoro.

“TUMA tutaendelea kushirikiana kwa namna moja ama nyingine katika kifo cha Langa, huku tukiomba na wasanii wote tushirikiane katika msiba wa ndugu yetu Langa,” alisema.

Wasanii mbalimbali wameonyeshwa kupata mshtuko mwingine, akiwamo Kalapina, aliyeibuka na kusema hofu imezidi kutawala na kumuombea marehemu aende akapumzike kwa amani.

Kalapina alisema kuwa Langa ni miongoni mwa wasanii wenye kutoa mashairi mazito, hivyo Hip Hop imezidi kukumbwa na wasiwasi wa aina yake kwa kuwapoteza vijana wao wenye makali ya hali ya juu katika ramani ya muziki huo nchini.

“Langa ni msanii mzuri mwenye uwezo wa juu, hakika nitamkumbuka kwa mengi, maana kifo chake ni pigo kwa Watanzania na wadau wote kwa ujumla,” alisema Kalapina.

Naye Kala Jeremia, alisema kuwa kifo cha Langa ni pigo zaidi katika muziki wa Hip Hop hapa nchini, baada ya kurafiki katika Hospitali ya Muhimbili.

“Tutaendelea kumkumbuka msanii mwenzetu Langa, maana wote safari ni moja,” alisema Kala ambaye tuzo yake ya wimbo bora wa Hip Hop aliyposhinda ameamua kuipeleka katika familia ya Ngwair kutokana na kuthamini mchango wake.

Ratiba ya kifo cha Langa imepangwa kuwa msanii huyo ataagwa siku ya Jumatatu kuanzia saa saba mchana, ambapo saa 10 alasiri atazikwa katika makaburi ya Kinondoni jijini Dar es Salaam.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...