https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Wednesday, June 19, 2013

Chadema wanafuga ‘jini’ walitafutie damu ya kulinywesha


MGODI UNAOTEMBEA
Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
INAHITAJI akili ya kiuwendawazimu kupita huku na kule kusifia mwendelezo mbovu wa siasa za Tanzania, hasa baadhi ya vyama vya upinzani kufanya mambo ya kijinga.
Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe
Ni pale mwanasiasa anayejiona anakubalika kwa wananchi wake, anaamua kwa makusudi kuvunja sheria za nchi. Huu ni ujinga. Unahitaji kupingwa vikali na kila muhibiri wa amani.
Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi CCM na Rais wa Jamhuri ya Muunganao wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete.
Kwa wiki moja sasa, jiji la Arusha limekuwa likitawaliwa na uvunjifu wa amani, taharuki na kusababisha matatizo makubwa. Tangu siku ya Jumamosi ya Juni 15, wananchi wa Arusha wamekuwa wakiendelea kuishi kwa mashaka na wasiwasi mkubwa.

Watu watatu wamefariki Dunia, huku wengine kadhaa wakijeruhiwa vibaya, ikiwa ni baada ya bomu kurushwa katika mkutano wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), huku ukihudhuriwa pia na Mwenyekiti wao, Freeman Mbowe.

Ikumbukwe kuwa, matokeo ya ghasia jijini Arusha si mara ya kwanza, maana kila siku kunakuwa na mgogoro mkubwa na kuwaacha Watanzania wenzetu wakiwa hawaelewi cha kufanya.

Mara baada ya kutokea mlipuko huo, Mbowe, kama mwenyekiti wa Chadema, alitangaza kuwazuia wabunge wote wa chama hicho kuingia kwenye vikao vya Bunge.

Ni kauli tata sana kwa maendeleo ya Taifa. Taifa ambalo, linahitaji bajeti bora yenye maslahi na Watanzania wote. Lakini kuzuia wabunge kuhudhuria vikao vya Bunge, ni vitendo vya kushangaza mno.

Kwa mujibu wa Mbowe, aliwazuia wabunge kuhudhuria vikao vya Bajeti ili washiriki kwenye misiba ya waliokufa kutokana na mlipuko huo wa Soweto, jijini Arusha.

Mbowe anatangaza hatua hii huku akijua kuwa Chadema haipo Arusha peke yake. Chadema pia inahitaji kura za wananchi wote, kama vile Tanga, Kilimanjaro, Mwanza, Mbeya, Morogoro, Iringa na mikoa mingine kama kweli inahitaji kushika dola.

Lakini Chadema wao wameonekana kuweka nguvu kubwa kwa jiji la Arusha, tena wakifikia hata kuvunja sheria za nchi. Ndio hapo ninapoanza kujiuliza juu ya mwendo huu.

Tunahitaji viongozi wendawazimu. Wale wanaoweza kufanya kazi bila kuogopa sura au mihemko ya viongozi wa vyama vya siasa. Kwa mfano, sheria inajieleza juu ya vyama vya siasa vinavyofanya vitendo vya vurugu na adhabu yake pia.

Tunahitaji sasa serikali kwa kupitia Msajili wa Vyama vya siasa, John Tendwa kuwa makini zaidi. Jeshi la Polisi nalo lihakikishe kuwa linasimamia vyema usalama wa raia.

Usalama ambao mara kadhaa umekuwa hatarini kwasababu ya matakwa ya viongozi wachache wa kisiasa. Huu ndio ukweli. Jeshi la Polisi Tanzania, mkoani Arusha lilizuia mikusanyiko isiyokuwa na sababu.

Ili kuonyesha kuwa Chadema wana lengo lao binafsi, waliamua kufanya mkutano bila hata kupewa kibali cha polisi. Hapa Chadema walitegemea kitu gani?

Wanataka waendelee kuvunja sheria wakijua wanaogopwa, hawawezi kuchukuliwa hatua za aina yoyote? Kila mara wabunge wa Chadema wanafanya vitendo visivyokuwa vya kiungwana.

Mbunge kama vile Godbless Lema, Tundu Lissu, Mbowe, Mchungaji Peter Msigwa wamekuwa wakijifanya wao ndio kila kitu katika Taifa hili, jambo linaloibua maswali kede kede.

Kuheshimika kwao wanakuchukulia vibaya, ndio maana matamshi yao mara kwa mara hayajengi jamii bora zaidi ya kuibomoa kadri wanavyojua wao, lengo lao ni kuichafua serikali iliyopo madarakani, chini ya Rais Jakaya Mrisho Kikwete, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Hii sio njia nzuri kamwe. Tanzania inazidi kuingia kwenye migogoro kama hii kwasababu ya ujinga wa watu wachache, ambao nashawishika kusema kuwa wana uchu wa madaraka.

Mara baada ya mlipuko kutoka Jumamosi, Mbowe hakuonyesha kumfahamu mlipuaji huyo, zaidi ya kuwazuia wabunge kuingia bungeni, akiwamo Zitto Kabwe, ambaye alipaswa kuwasilisha Bajeti ya Wizara Kivuli ya Fedha na Uchumi.

Lakini siku moja baadaye, yani Jumapili, Mbowe huyu huyu anatangaza kuwa anamfahamu vyema mlipuaji wa bomu, akasema ni Polisi. Sasa kama ndio yeye, maana hakuna anayeweza kufanya uharifu akachekewa, isipokuwa anahitaji kuchukuliwa hatua kali.

Kauli ya Mbowe inakwenda sambamba na tamko la serikali Bungeni, kwa kupitia Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, William Lukuvi, aambaye alionyesha kupigwa na butwaa jinsi baadhi ya Watanzania wenzetu wanavyopigania kuiharibia sifa nchi yetu.

Lukuvi akafika mbali zaidi kwa kusema serikali itatoa Milioni 100 kwa mtu atakayetoa ushahidi wa wanaofanya vitendo vya kiharifu, kama hivyo vya kulipua mabomu, huku nikiamini kuwa Mbowe atatoa ushirikiano kwa kumtaja mtu huyo.

Kwa uelewa wangu na siasa za Tanzania, zenye kila aina ya mihemko, kutoka baadhi ya vyama upinzani, sidhani kama Chadema wangeweza kumuacha mhalifu, arushe bomu na kutokomea kusipojulikana.

Chadema wasingefanya ujinga huu. Wangemng’ang’ania. Kama wanaweza kushindana na polisi kwa kuwarushia mawe, wakisema ukombozi unakaribia, kwanini wamuache mtu anayepiga bomu katika mkutano wao wa kampeni?

Hapa nini kinatengenezwa? Kwa bahati mbaya wale wasiokuwa na uelewa mzuri juu ya mambo ya kisiasa, wanajikuta wakipumbazwa na janja za aina hiyo kwenye propaganda za kisiasa. Naweza kusema kuwa Chadema wao wenyewe wanafuga jini, hivyo walitafutie damu ya kulinywesha, tofauti na ile ya Watanzania inayomwagika bila sababu za msingi.

Angalia ajabu hii, mara baada ya bomu kurushwa kwenye mkutano huo, mtu ambaye anadaiwa kurusha, hakuweza kukamatwa mara moja kwasababu Polisi hawakupewa ushirikiano.

Ni pale walipoanza kurushiwa mawe na wananchi kwenye tukio hilo, ambalo baadhi yao wamepoteza maisha. Siasa za aina hii sio mahali pake. Kila mtu mwenye mapenzi mema na Tanzania ni wakati wake sasa kuwa makini na kuwa mkali zaidi.

Watanzania tunadanganywa na wanasiasa ambao wanatumia nguvu kubwa kuiweka nchi kwenye kisiwa cha umwagaji damu. Wanasiasa wa aina hii wanatafuta kitu gani?

Hata kesho wakifanikiwa kunyakua dola, wanataka waongoze watu wa aina gani? Inauma sana. Katika kuliangalia hili, naona kufanikiwa kwake ni ngumu, maana kwa bahati mbaya wapo wananchi wanaojifanya hawanazo.

Wanajifanya wana uchungu zaidi na nchi hii kuliko Baba wa Taifa, ambaye licha ya kuhangaika kwa mambo mengi, ila leo hii ametangulia mbele za haki.

Wapambanaji wengi waliohakikisha kuwa mimi na wengine wenye umri wangu wanakuja kuishi katika nchi hii. Nchi ambayo kutokana na uongozi bora, kuheshimiana na kupendana, kulisababisha kutapakaa kwa sifa nzuri ya kisiwa cha amani.

Kisiwa cha amani ambacho leo hii watu wanataka kugawanywa kwa dini zao, makabila yao na mikoa wanayotoka. Leo hii jiji la Arusha, lenye sifa kemkem linanuka damu.

Kila siku Arusha kimewaka. Kunanini? Nani kasema Arusha ni lazima damu zimwagike? Huu sio mwendo mzuri hata kidogo. Ni wakati wetu sasa kila mtu kuwa makini na aweke msimamo.

Kwa wale wanaopenda mabadiliko ya kiutawala, yani kutoka Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kuingia upinzani, pia sio sahihi kushinda kwa kurushiana mabomu na risasi za moto.

Wapo watu wanaocheka kwa vitendo hivi. Hao wanajidanganya kuwa muda wa mabadiliko umefika. Sawa, lakini mabadiliko hayo yana manufaa gani kama watu wanapoteza maisha?

Kwanini tusifuate sheria na taratibu za kiungwana? Angalia, wabunge wa Chadema baada ya kususia Bunge, walivamia jiji la Arusha, wakijifanya wao ndio wenye uchungu kuliko wengine.

Hizi ni janja za kisiasa tu. Hakuna jipya linaloweza kufanywa kwa amani kama watu wanapita kwenye migongo ya wananchi, bila huruma na kuangamiza roho za ndugu zetu na wengine kupata majeraha na kuharibu nguvu kazi ya Taifa.

Wapo radhi watu wafe lakini wao waendelee kujulikana katika mitaa na kaya zetu. Wapo radhi wafanye fujo wakiamini kuwa vyombo vya habari vitawaandika pamoja na kupata mijadala kwenye mitandao ya kijamii, ambayo imejaza wanasiasa uchwara.

Ni wale wanaoacha mambo ya maana na kujadili upupu wa mabwana wakubwa hawa ambao wengi wao wanaishi maisha yenye kila raha, wakati wanaowahadaa na kufariki wanalala njaa, wanakufa masikini.

Wanadanganya kila wawezalo. Wanafanya kila hira, lakini siku akitoka hapo anaingia tena bungeni kwa ajili ya kutunisha mfuko wake kwa posho za serikali.

Kulikuwa na haja gani ya viongozi wa Chadema kufanya mkutano bila kupewa kibali? Hizi si janja za kutaka waandikwe? Mwisho wa siku wabunge watatu, akiwamo Tundu Lissu, Joyce Nkya, Mustafa Akoonay wakikamatwa huku mwenyekiti wao, kinara wa yote hayo, Mbowe akifanikiwa kutoroka.

Ametorokea kusipojulikana. Watu wanajua ametoroka, walioandika wanaandika katika media zao. Kesho akikamatwa au kujisalimisha polisi aandikwe tena.

Huku ni kusumbua umma. Huku ni kutumia ujanja kujinufaisha kisiasa kwa mambo ya kijinga kabisa. Watanzania tuyaseme haya ili kuelimishana kwa ajili ya Tanzania yetu.

Taifa linakabiliwa na changamoto nyingi mno. Bajeti ya mwaka 2013/2014 imetangazwa huku ikishindwa kujibu namna gani wananchi wanaweza kuishi maisha bora.

Kodi kubwa itakuwa migongoni mwao. Bei za bidhaa zinazotumiwa na walalahoi zimeongezwa mara dufu. Biadhaa kama vile mafuta ya dizeli, petrol zitawafanywa wananchi waishi mashakani.

Kuongezwa kwa kodi hizo, kutaongezeka mfumko wa bei mara dufu. Nauli zitapanda na vyakula havitakatika. Watu watakufa njaa. Hapa ndipo tunapohitaji vichwa vya wabunge wetu, badala ya kuelemea kwenye mambo ya anasa, kupiga soga na kulinda umaarufu wao usipotee.

Tunayasema haya hata tutaitwa makada wa CCM au wale wanaombiwa wapo kwenye ndoa, yani wananchi wanaounga mkono siasa za Chama Cha Wananchi (CUF).

Nadhani kwa kulijua hili tunapaswa kuwa makini zaidi. Tuambiane ukweli, maana kinachoendelea leo jijini Arusha, kitakuwapo tena katika mikoa yetu, wilaya au vijiji vyetu.

Kama leo wanaokufa ni Wachaga wanaounga mkono Chadema,  basi kesho sumu hiyo itahamia wilayani Handeni, Korogwe, Lushoto, maana nao wanafuatilia masakata haya yanayofanywa kwa makusudi kama njia ya kulisumbua Taifa letu.

Nachukizwa na vitendo vya kihuni. Natamani sheria ichukuwe mkondo wake. Kwa wale wanaofanya uhuni wa aina hii wakibainika wakamatwe na kufunguliwa mashtaka au kuvifuta vyama vya aina hii.

Najua hili ni jambo litakalozusha ghasia na machafuko, maana watakimbilia kwenye huruma za wananchi, lakini akheri ya pengo kuliko jino bovu.

Chadema ni kero na lazima wajirekebishe, maana wanachofanya sasa, akipatikana kiongozi makini, asiyekuwa na woga na anayesimamia vyema sheria zake, wanasiasa wengi kwenye vyama vya aina hii wanastahili kutulizwa mihemko yao.
Mungu ibariki Tanzania.

+255 712053949
+255 753806087
Mwisho


No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...