https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Wednesday, June 26, 2013

MGODI UNAOTEMBEA: Ubaguzi wa dini umeongeza joto la wasiotaka Muungano Visiwani Zanzibar


Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
INAHITAJI moyo wa chuma mno kuendelea kusikiliza maneno machafu, kejeli kutoka upande mmoja wa Muungano, yani Zanzibar, dhidi ya wenzao Tanzania Bara.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete akiwa na Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shen.


Ni matusi kupita kiasi. Katika watu 10 mjini Zanzibar, nane kati yao wanaubwatukia Muungano, wakiuita wa kinyonyaji na hauna manufaa kwao, tangu ulipoasisiwa mwaka 1964 kutokana na matakwa ya viongozi wawili, yani Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Abeid Aman Karume, Rais wa kwanza wa Zanzibar.
Waasisi wa Bara na Visiwani, Marehemu Julius Nyerere na Abeid Aman Karume wakikubaliana juu ya Muungano huo.

Hawautaki hata kidogo. Wanazungumza mengi kuelezea ukweli huo mbele ya jamii nyingine, hasa Bara, ambao wo wameonekana kama ving’ang’anizi wa Muungano huo.

Si vibaya mtu kutoa maoni yake, kusema kile anachokiamini, ila ubaya unakuja pale mtu huyo anapotoa kashfa ili anayosema yasikilizwe na kueleweka.

Mengi yanasemwa, ila binafsi naweza kuzungumzia sakata hilo kuwa linachangiwa kwa kiasi kikubwa na ubaguzi, udini, ndio maana tunashuhudia mnyukano, kuchomeana nyumba za ibada, hasa makanisa visiwani humo.

Zanzibar ambayo watu wake wengi ni wenye dini ya Kiislamu, wanaona hakuna mwingine mwenye ruhusa ya kuishi huko isipokuwa yule mwislamu.
Mtu yoyote mwenye asili ya Bara, hasa akiwa Mkristo, basi hana nafasi ya kuishi Zanzibar kwa raha, kama wao wanavyoishi Tanzania Bara.

Ni ajabu mno. Ingawa Wazanzibar wengi wanaona Visiwani ni kwao peke yao, ila wenzao wa Bara wameendelea kuwa kimya.

Ukimya huo unachangiwa na roho ya upendo dhidi ya ndugu zao Zanzibar, ndio maana kwenye mitaa yao bado wameendelea kuwapa hadhi ile ile na haki ile ile.

Japo ndio kuna mapungufu mengi katika muungano wa Bara na Visiwani, lakini yanaweza kuzungumzika kwa ajili ya kuuboresha na sio kuuvunja kama wanavyotaka baadhi yao.

Zaidi ya hapo, huwezi kutofautisha ubaguzi wa dini, ukabila uliokuwa kwa kiasi kikubwa katika nyoyo za watu wa Zanzibar.

Wale wanaoona kuwa kuendelea kuwa kwenye muungano huo, kunasababisha wachache wakose fursa ya kuoiona Zanzibar inakuwa nchi huru, tena Taifa la Waislamu.

Hili si jambo lenye mbolea kwa Zanzibar. Zanzibar ambayo licha ya wachache wasiojitambua wakijipambanua kuwa wanaweza kusimama wenyewe, lakini bado wamekuwa wakitegemea vitu vingi kutoka upande wa Bara.

Hili tukilisema, wapo watakaobisha, hasa wale wanaaokesha kuomba siku moja Zanzibar ijitenge katika Muungano huo na wafanikishe adhma yao ya kuwa Dola la Waislamu.

Na endapo suala hilo litafanikiwa, basi hata wale waliozaliwa mjini Zanzibar ila wenye asili ya Tanzania Bara, kuna uwezekano mkubwa watakimbizwa.
Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, katika uhai wake alikuwa akilielezea suala hili mara kwa mara.

Hakuonekana mwenye kupenda kuona Zanzibar wanajitenga au Bara wanajitenga. Nyerere anayekumbukwa na wengi duniani, alisikika mara kwa mara akisisitiza muungano wenye kujali utu wa kila Mtanzania, bila kuangalia yeye ni mwenye asili ya Zanzibar au Bara.

Tumesikia au kuona mara kwa mara matamko ya watu wa Zanzibar, wakiwamo viongozi wao wakisimama na kuukosoa muungano huo kwa vitendo.

Kwa bahati mbaya, wapo wanaokosoa muungano huo katika majukwaa ya kisiasa, lakini katika serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK), wanabaki kimya.
Hawa ni wanasiasa. Watu ambao wanachokisema kwa wakati huo, si watakachokitenda muda ujao.

Kwanini nasema hivyo? Ukiangalia mfumo mzima wa vyama vingi Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, upande wa Zanzibar wameelemea sana katika utawala wa Kiislamu.

Mtu anayekuwa Muislamu, Visiwani Zanzibar ana nafasi kubwa kushinda katika Uchaguzi wowote, ukiwapo Ubunge.

Si vibaya, hasa kama aliyeshinda amechaguliwa na wananchi wake, 
ukizingatia kuwa tupo katika kuitetea vyema Demokrasia.

Angalia, licha ya Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kuonekana kukubalika mno katika siasa za Tanzania kwa miaka mitano hii, lakini Zanzibar haina nafasi.

Katika Uchaguzi Mdogo wa Jimbo la Chambani, ambapo mshindi wake alikuwa ni mgombea ubunge kwa tiketi ya Chama Cha Wananchi (CUF), Yussuf Salim Hussein, aliyepata kura 2708, Chadema wao walipataa kura 12 tu, wakiwa na mgombea wao Siti Ussi Shaibu.

Chama Cha Mapinduzi (CCM), wenyewe walipata kura 202 wakiwakilishwa na mgombea wao, Sarahan Said, wakati kile chama kipya kilichotokea katika mgongo wa CUF, yani Alliance For Democratic Change (ADC), ikiwakilishwa na Said Miraaj, ambaye pia ndio mwenyekiti wa Chama hicho.

Kwa waliofuatilia siasa za Zanzibar kwenye Uchaguzi huo wa Chambani watakubaliana na mimi kuwa wapo waliosimama hadharani wakisema kuwa ADC kinasimamiwa na Kanisa, kama kilivyokuwa Chadema.

Mtu anapotoa maneno kama haya, ni wazi wananchi, hasa Zanzibar ambao siku zote wamekuwa wakichukizwa na Ukristo, kamwe hawawezi kukipigia kura.

Nasema haya kwasababu sipendi fitina. Kuacha kuuzungumza ukweli, ili niwafurahishe wale wazandiki, wasiopenda ukweli.
Huu ndio ukweli wa mambo. Kinachoongeza joto katika Muungano wa Bara na Visiwani, ni vita ya ubaguzi wa dini.

Si kweli kama Tanzania bara inanufaika kwa kiasi kikubwa na Muungano huo, ila wale wanaosema hayo ndio wenye chuki, choyo na ubaguzi wa dini.

Ndio hao wanaotamani Zanzibar iwe nchi ya Waislamu, jambo ambalo si sahihi hata kidogo, ukizingatia kuwa suala hilo linaweza kuibua mizozo na migogoro kila siku.

Angalia, wakati wanasiasa, hasa waliokuwa kwenye Chama tawala wanazungumza siasa zenye kujenga zaidi, wenzao wameona njia sahihi ni kuupinga Muungano, wakiamini kuwa wananchi wengi watawaunga mkono.

Ndio hapo zinazoitwa taasisi za kidini, kama vile Uamsho walipoingia na kushika kasi na kuzua taharuki ya aina yake.

Hawa walipita kila kona kuhubiri dini na kuupinga muungano. Wenyewe wanaziita harakati za kuipa hadhi ya juu ya Kitaifa na kuwa nchi kamili. Yani kuwa na mamlaka yake ndani na nje ya nchi.

Kama vita hivi vya mgogoro wa Muungano visingechochewa na ubaguzi wa dini, sidhani kama majadiliano ya kuuboresha yasingefikiwa kwa pande zote mbili.

Kwa bahati mbaya zaidi, wakati wananchi hao wanatafuta namna gani ya kuuvunja Muungano huo, kwa kuangalia tofauti zetu za kidini, yani Uislamu na Ukristo, ukapenyezwa tena mjadala wa Serikali tatu.

Huu ulipenya katika Tume ya Maoni ya Katiba Mpya, chini ya Mwenyekiti wake, Jaji Joseph Sinde Warioba.

Maoni haya yalizungumzwa sana na baadhi ya viongozi wa kidini visiwani Zanzibar pamoja na wachache kutoka CUF, chama kinachoongoza nchini kwa ushirikiano, kati yao na CCM, chini ya Rais wake, Dk. Ali Mohamed Shein.

Mengi yanayosemwa sasa ni kuzidi kupandikiza chuki miongoni mwa Watanzania. Yanayosemwa sasa yatawapandisha hasira wengine na kuingia kwenye mgogoro, wakati pande mbili hizi zimekuwa zikiishi kwa upendo na kuheshimiana kwa kiasi kikubwa.

Ni wakati wetu Watanzania wote kwa kupitia Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, yani Bara na Visiwani, kuona kuwa badala ya kutaka chokochoko za kugawana, wenzetu walioendelea wanatafuta namna ya kuungana ili wapate nguvu zaidi.

Sidhani kama ni sahihi Wapemba kupigania sana kuugawa Muungano huo, wakati wanajua fika Bara wamezagaa wao kila mahali na hakuna anayekimbizwa.

Hata hivyo haitoshi, tayari pande mbili hizi zimeleta mwingiliano wa kimaisha na kuwafanya waishi kwa amani, furaha na amani ya aina yake.

Kwa bahati nzuri, licha ya Visiwani kuonekana kushikilia kuuvunja muungano, wakieneza mno hoja za udini, ila wenzao Bara wamekuwa wazalendo zaidi.

Ndio maana bado wabunge wake wanaishi kwa upendo katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Wanaendelea kulipwa posho, mishahara na stahiki zao zote.

Wanafanya na kupata kila kinachostahili kama watumishi wa umma. Haya ni maisha yenye neema mno.

Badala yaendelezwe, wanajitokeza wachache, makundi ya watu wakitaka kutugawa kwa kila wanavyotaka wao.

Binafsi nimekuwa muumini mkubwa wa Muungano huu wa Bara na Visiwani. Naupenda kwasababu hakuna haja ya kuuchukia.

Sioni maana ya kuuponda. Mwenye upendo kwa wengine, asiyekuwa mbaguzi, mwenye choyo katu hawezi kuukataa Muungano huu, iwe mchana au usiku.

Na kama Muungano huu una mapungufu, kasoro, hakuna njia ya kuuboresha? Sitaki kusema watu wa Bara wote wanaotoa huduma za kijamii Zanzibar waondoke Zanzibar, japo naamini watatoka huko kama kelele hizi, ubaguzi huu, choyo hiki kitaendelea kushika hatamu kila siku ya Mungu.

Ni wakati wetu sasa kila Mtanzania, bila kuangalia anatoka Bara au Visiwani kusimama mstari mmoja kuwakataa wanaotaka kuuvunja Muungano huu.

Tena wale wanaoukataa kwa kuingiza hoja za udini, ukabila, maana daima huo umesababisha mapigano na kuyagawa Mataifa mengi.

Mwenye hoja za kutaka kuuvunja Muungano, pia asisite kuelezea njia zinazoweza kuchukuliwa kwa ajili ya kuunusuru Muungano huo unaopigiwa kelele.

Nayasema haya kwa mapenzi makubwa na Taifa langu, maana kwangu hakuna zaidi kati ya Mzigua au Mpemba.

Hawa wote ni ndugu zangu na wana haki sawa ya kuishi katika moja ya vijiji, wilaya au mikoa ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Nikirejea katika baadhi ya maneno ya Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere juu ya kuupigia kelele Muungano huu, alisema kuwa baada ya Muungano huo kusambaratika na Wazanzibar kujitenga, watagundua kuwa kumbe wao bado si wamoja.

Makundi mawili yatajitokeza, moja Waunguja na wengine Wapemba. Wachache hao wanataka kujitenga kwasababu ya Muungano wa Tanzania Bara na Visiwani.

Nje ya Muungano huu, bado Zanzibar hawatabaki salama, kama itakavyokuwa upande wa Bara nao kujitenga kwasababu za kijinga, hasa udini, ukabila nilioelezea katika makala haya.

Katika kuliweka sawa jambo hili, shime viongozi wote wa vyama vya siasa na serikali ya Bara na Visiwani kusimama kidete juu ya kuunusuru Muungano huu unaotikiswa kwa sasa.

Sio kweli kama kuna mmoja ananufaika zaidi ya mwenzake na hata kama yupo, huyo anayenyonywa anayo haki ya kupaza sauti yake juu kwa njia ya kutafuta suluhu.

Mungu ibariki Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Bara na Visiwani.
0712 053949
0753 806087

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...