https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Thursday, January 23, 2014

Yanga yatangaza bifu na TFF ikisema inawahujumu baada ya kumsimamisha Emmenuel Okwi



Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
KLABU ya Yanga, imesema kwamba Shirikisho la Soka nchini limedhamiria kuwahujumu baada ya Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji kumsimamisha mchezaji wao Emmanuel Okwi kukipiga kwao kwa madai kuwa usajili wake umejaa mizengwe, ikiwa ni siku mbili kabla ya Ligi kuanza katika viwanja mbalimbali nchini.


Katibu Mkuu wa Yanga, Beno Njovu, pichani.
Akizungumza na waandishi wa Habari jijini Dar es Salaam leo jioni, Katibu Mkuu wa Yanga, Beno Njovu, alisema kuwa haiwezekani Kamati hiyo izuie mchezaji siku mbili kabla ya ligi kuanza.

Alisema hali hiyo iliwahi kutokea pia kwa wachezaji Mbuyi Twite na Mrisho Ngassa, ingawa baadaye walicheza kwa mvutano mkubwa, hivyo kuchelewesha ndoto zao katika sekta ya mpira wa miguu.

“Ikiwa wewe ni TFF lazima ujuwe kuwa wonachama wote wana haki sawa, hivyo kinachofanywa na TFF kwa sasa ni kutuhujumu sisi Yanga kwa kutoa uamuzi wakati ligi inaanza Jumamosi.

“Hatuwezi kukubaliana nao na mpaka sasa hatujapata barua kutoka kwao, hivyo Jumamosi Kamati ya Utendaji itakaa na kutoa uamuzi haraka kwa ajili ya kuangalia mwenendo huu usiokuwa na tija kwa soka la Tanzania,” alisema Njovu.

Aidha, Njovu alitumia muda huo pia kuwazungumzia wajumbe mbalimbali wa TFF, ikiwamo Kamati ya Sheria, ambapo aliyekuwa Katibu Mkuu wa Simba, Evodius Mutawala, Hans Poppe na wengineo wajumbe ambao kamwe hawawezi kutoa uamuzi wenye mashiko, ukizingatia kuwa mwenyekiti wao Ismail Aden Rage, alitangaza kuwa kamwe Okwi hatachezea Yanga.

Kwa mujibu wa Njovu, Yanga imechoshwa na mwenendo mbaya wa TFF wa kuwahujumu, hivyo wanachokifanya kwa sasa ni kukaa ili watowe tamko zito dhidi ya Shirikisho hilo.


No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...