https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Saturday, January 25, 2014

Makundi ya nyuki yapungua kutokana na uharibifu wa mazingira

Mkuu wa Mkoa Tanga, Chiku Gallawa, pichani.
Na Oscar Assenga, Tanga.
IMEELEZWA kuwa uharibifu wa mazingira unaotokana na ukataji miti ovyo,uchomaji wa moto misitu ikiwemo uharibifu wa vyanzo vya maji husababisha kupungua kwa makundi ya nyuki mkoani Tanga.

Kauli hiyo alitolewa na Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Luteni Mstaafu Chiku
  Gallawa wakati akizungumza na waandishi wa habari ofisi kwake hivi karibuni ofisini kwake ambapo alisema changamoto nyingine ni uhaba wa maafisa ugani katika mamlaka za serikali za mitaa.

Alisema licha ya kuwa na changamoto hizo uzalishaji wa asali mkoani hapa umeongezeka kutoka kilo 32,559 mwaka 2011/2012 na kufikia kilo 139,573 Octoba mwaka 2013 wakati uzalishaji wa nta nao pia umeongezeka kutoka kilo 1886 mwaka 2011/2012 na kufikia kilo 42,000 Octoba mwaka jana.

Mkuu huyo wa mkoa alisema katika mkoa wa Tanga kuna vituo viwili vya  uchakataji wa asali ambapo kimoja kipo wilayani Lushoto ambacho wanafungasha asali na kutengeneza bidhaa mbalimbali na kile cha wilayani Mkinga ambacho hakijaanza kutumika kutokana na uzalishaji mdogo.

Aliongeza kuwa katika mwaka wa fedha 2012/2013 mkoa umefanikiwa  kuanzisha kituo kimoja cha kuchakata asali kilichopo Kata ya Bungu wilayani Korogwe pamoja na kuongeza vikundi vya wafugaji nyuki kutoka 264 mwaka 2011/2012 na kufikia 291 Octoba mwaka jana.

Alieleza kuwa katika kipindi cha mwishoni mwa mwaka jana hifadhi mbili  za nyuki zimeanzishwa katika wilaya za Kilindi, Manzuki 12 wilaya ya Mkinga na mbili wilaya ya Korogwe.

Alisema kupitia wakala wa misitu Tanzania mkoa umegawa mizinga ya kisasa 100 kwa kila halmashauri kwa lengo la kuongeza hamasa ya wananchi kufuga nyuki ikiwemo kuzitaka kuhakikisha kila kikundi cha ufugaji kinafikisha idadi kama hiyo ilianishwa badala ya 12 ya sasa ili kupata faida.

Hata hivyo alisema mkoa ulitumia maonyesho ya Kimataifa ya Biashara na  Kongamano la Uwekezaji Kanda ya Kaskazini yaliyofanyika mkoani hapa kama fursa kwa wafanyabishara na wajasiriamali wa mazao yanayotokana na ufugaji wa nyuki kuonyesha bidhaa na huduma zao ili kupanua masoko
ndani na nje ya nchi.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...