https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Tuesday, January 28, 2014

Cheza Kidansi wakutana kuujadili muziki wa dansi


Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

WADAU wa muziki wa dansi wanaotokea katika mkusanyiko unaojulikana kama Cheza Kidansi, juzi walifanya kikao cha kwanza na kuadhimia mpango wao kuwawezesha wanamuziki wa muziki huo na kuwakwamua kiuchumi.

Wadau wakijadiliana jambo katika kikao hicho cha Cheza Kidansi.
Kikao hicho kilifanyika katika Ukumbi wa Garden Breeze, ambapo kilihudhuriwa pia na mlezi wao Yusuph Mhandeni, maarufu kama Yusuphed Mhandeni, ambaye ni Mchumi wa Kata ya Makumbusho katika Chama Cha Mapinduzi (CCM).


Akizungumza katika kikao hicho, Yusuphed alisema kuwa mengi yaliyojadiliwa katika kikao hicho ni kuona muziki wa dansi unarudi katika chati yake ili wanamuziki wajimudu kiuchumi.


Alisema wanamuziki wengi wa dansi hawana maisha mazuri kuliko wenzao wa Bongo Fleva, hivyo hilo ni kati ya changamoto zinazoendelea kuwakumba.

“Aidha tulijadili pia namna gani wanamuziki hawa wanatumika kwenye matukio makubwa ndani ya chama na serikali, ukizingatia kuwa suala hilo litakuwa na tija kwao.


“Kwa sasa wasanii wa kizazi kipya ndio wenye soko kubwa na kufanikisha maisha bora kwao, ndio maana hata vituo vya redio bado vimeegemea zaidi huko, jambo ambalo nimefurahi kuona Cheza Kidansi wamejaribu kuliangalia hili kwa kina,” alisema Mhandeni.


Cheza Kidansi ni kundi linalotokea katika mtandao wa kijamii linaloendeshwa kwa kuutangaza muziki wa dansi na kuangalia changamoto zao ili kuuweka kileleni kama ilivyokuwa awali.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...