https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Friday, March 28, 2014

Wananchi Handeni walalamika kuporwa ardhi yao


Na Kambi Mbwana, Aliyekuwa Handeni
WANANCHI wa Kijiji cha Komsala, wilayani Handeni, mkoani Tanga, wamemlalamikia mwekezaji anayejulikana kwa jina la Amina Singa, kuwa anapora ardhi zao, huku serikali ya Kata Kwamatuku, ikishindwa kuwatetea wakulima wadogo na kuelemea upande wa mwekezaji.
Katibu wa Baraza la Kata ya Kwamatuku, Nassib Bakari, pichani.
Mwandishi wa habari hizi alitembelea katika kijiji hicho na kufanya mazungumzo na wananchi sambamba na Baraza la Kata juu ya mgogoro huo unaosababisha malalamiko mengi kutoka kwa wakulima hao.
Mjumbe wa Baraza la Kata ya Kwamatuku, Mwanahamisi Nyata, pichani.
Akizungumza kwa huzuni kubwa, mkulima aliyejitambulisha kwa jina la Hausi Zuberi, alisema kuwa mwekezaji huyo amechota eneo lake, kama alivyofanya hivyo kwa wananchi wengine waliopakana na shamba lake.
 Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Muhingo Rweyemamu pichani.
Alisema hali hiyo imewafanya waishi kwa mashaka wakiamini kuwa ataendelea na tabia yake hiyo, licha ya kumiliki eneo zaidi ya heka 120 hali ya kuwa anashindwa kulilima.
Hausi Zuberi, mmoja wa walalamikaji wa migogoro ya ardhi katika Kata ya Kwamatuku, wilayani Handeni, mkoani Tanga.
“Mwekezaji huyu ni kero kubwa kwetu kwasababu amechota maeneo yetu wakulima tusiopungua 6 baada ya kuvuka mbele ya mpaka wake, hali inayotufanya tuishi kwa hofu tukiamini kuwa ataendelea kutupora,” alisema.

Naye Paulina Athon Simbaulanga, alisema kuwa uporaji huo umebarikiwa na Baraza la Kata, baada ya kutembelea eneo hilo, jambo linalowafanya waamini kuwa kuna njia ya mkato iliyopitwa katika kufanikisha uporaji huo.

“Amina alikuja kijijini kwetu na kuomba heka 60, lakini sasa ana heka 120 na bado anapora sisi tusiokuwa na hata heka 5, licha ya yeye kumiliki eneo kubwa.
“Hatujui hizo heka nyingine amezipata vipi na sheria za ardhi zinasemaje katika hilo, ingawa serikali ya kijiji inajua na mgogoro huu umebarikiwa na viongozi wetu,” alisema.

Alipotafutwa Amina, alisema hawezi kuzungumzia suala hilo kwakuwa wananchi hao ndio waliovamia shamba lake, licha ya kushindwa kusema ni kiasi gani cha shamba analomiliki kijijini hapo kutoka heka 50 zinazotakiwa kisheria.

“Kwanza mtakuwa umefanya makosa kama mmeamua kufanya mazungumzo na wananchi hao kabla yangu, hivyo siwezi kusema lolote,” alisema Amina.

Katibu wa Baraza la Kata ya Kwamatuku, wilayani Handeni, mkoani Tanga, Nassibu Bakari Bigo, alikiri kuupokea mgogoro huo wa Amina na wakulima wa kijiji cha Komsala, huku akisema kesi za aina hiyo zimeendelea kushamiri katika maeneo mengi katika Kata hiyo.

“Tuliupokea mgogoro huo, lakini kwa kiasi kikubwa umechangiwa na serikali ya kijiji husika kwa kushindwa kutatua kesi hizo na watu kusaka haki yao Baraza la Kata,” alisema Bakari.

Kwa mujibu wa Bakari, kesi za migogoro ya ardhi zimeshamiri katika eneo lao, hivyo viongozi wa vijiji wanapaswa kusimamia vyema sheria za ardhi, huku wakitoa elimu kwa wakulima na wananchi wao, wakiwamo walalamikaji wa kesi inayomhusisha Amina, kutokana na mashahidi wao kushindwa kufika walipoitwa na Baraza la Kata.


No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...