https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Sunday, March 02, 2014

Kaijage: Zambia ni mwisho wa maandalizi yetu


Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam

KOCHA Mkuu wa timu ya Taifa ya wanawake, Twiga Stars, Rogasian Kaijage, amesema kwamba wapinzani wao Zambia, walijiandaa zaidi kuliko wao, hivyo wametolewa kwa haki.

Katika mechi ya juzi iliyopigwa katika Uwanja wa Azam Complex, Twiga Stars, ilitoka sare ya bao 1-1 dhidi ya Zambia ‘Shipolopolo,’ hivyo kutolewa kwa bao 3-2 kufuatia matokeo ya mechi ya kwanza iliyochezwa nchini Zambia baada ya kupigwa bao 2-1.

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, Kaijage alisema kuwa maandalizi yao hayakuwa mazuri tofauti na wenzao, hivyo ujuzi wao ulishindwa kufanya vyema dhidi ya wapinzani wao.

Alisema ingawa walipania kuwatoa wapinzani wao, lakini kiwango chao na maandalizi yao hayakuwa mazuri kiasi cha kuwaaminisha kusonga mbele.

“Tumekuwa na matamanio ya kusonga mbele katika michuano ya Kimataifa, ila lazima tufahamu namna ya kuandaa wachezaji wetu.

“Tumevuna kile tulichokipanda dhidi ya timu ya Zambia, ambapo wametufunga bao 3-2, hivyo sisi kutoka katika michuano ya kuwania kufuzu Kombe la Mataifa ya Wanawake Afrika (AWC),” alisema.

Licha ya kuwa na wachezaji kadhaa wenye kutajwa kama hodari wa kucheza soka, timu ya Twiga Stars, imeondoshwa katika michuano hiyo, hivyo kushindwa kuwapa raha Watanzania.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...