https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Sunday, March 30, 2014

Mbio za urais zamkumbuka Mbunge wa Moshi Vijijini Dkt Cyril Chami

Mbunge  wa Moshi  Vijijini Dkt  Cyril Chami.

Na Mwandishi Wetu, Moshi 
Jinamizi la Urais linazidi kutikisa medani za siasa nchini, baada ya Mbunge wa Jimbo la Moshi Vijijini, Dk. Cyril Chami (CCM) kudai anaandamwa na mtandao wenye malengo ya Urais 2015.
 
Dk. Chami amedai kiini ni mbabe mmoja ambaye hakumtaja, mwenye uwezo wa fedha kukasirishwa naye, baada ya kukataa maagizo yake kwamba amsaidie swahiba wake anayewania Urais mwaka 2015.
“Niliikataa kazi hiyo kwa sababu haina maslahi kwa Taifa wala Moshi Vijijini…Mimi nitamuunga mkono mgombea Urais yeyote atakayechaguliwa na mkutano mkuu wa CCM,”alisema Dk. Chami.
Dk. Chami aliongeza kusema,”Haitanishangaza ikithibitishwa kuwa mbabe huyu ndiye anatoa fedha kuufadhili mtandao huu wa wahalifu, japo hii ni kazi ya Polisi na ni kazi inayoendelea,”
Mbunge huyo amedai mtandao huo, ndio ambao umefungua  akaunti yenye jina lake na picha katika mtandao mashuhuri wa kijamii wa Facebook na kumchonganisha na wapiga kura wake na CCM.
Katika taarifa yake Dk. Chami amedai akaunti hiyo inatumika kumchonganisha na chama chake pamoja na viongozi wakuu wa CCM ili asiteuliwe kugombea ubunge mwaka 2015.
“Kwa kujifanya wao ni mimi, wanapingana na misimamo yote ya CCM. Kwa mfano, wanadai kuwa kwenye mchakato unaoendelea wa Bunge la Katiba, mimi napendelea serikali tatu,”amelalamika.
Akitoa mfano wa hivi karibuni kabisa, Dk. Chami amedai Jumapili iliyopita, watu hao walitoa taarifa kuwa ana mashaka CCM itashindwa huko Kalenga kwa kuwa mara zote kinashinwa chaguzi ndogo.
 “Eti mimi napendelea kura ya siri katika Bunge la Katiba linaloendelea…. Naonyeshwa kuwa mtetezi wa CHADEMA na kutabiri ushindi wa Chadema huko Kalenga na Chalinze”amelalamika Dk. Chami.
Dk. Chami amesema akaunti hiyo ya Facebook sio yake na kwamba kama analo jambo anataka kuzungumza na wapiga kura wake, atawafuata jimboni na si kuzungumza nao kupitia Facebook.
Pia amesema tayari amewasiliana na viongozi wa CCM juu ya uwepo wa uhalifu huo ambao lengo ni kutaka kumuonyesha kuwa yeye ni msaliti ndani ya CCM jambo ambalo hata halifikirii kulifanya.
Dk. Chami amekilaumu kitengo kinachoshughulikia makosa ya mitandaoni (Cyber Crime Unit) kwa kushindwa kuifunga akaunti hiyo na kuwakamata walioifunga na wanaoendelea kuitumia.
“Tena akaniambia waliomba msaada TCRA (Mamlaka ya Udhibiti wa Mawasiliano Tanzania) ili akaunti hii ifungwe, nao TCRA wameshindwa”alilalamika Dk. Chami.
“Hadi leo akaunti inatumika naendelea kutengenezewa maadui ndani ya CCM na kwa viongozi wa juu wa nchi na wahalifu hawa wako huru wakiendelea kuchekelea maumivu wanayonisababishia”amedai.
Dk. Chami amesema japo ameshauri na Polisi kwamba naye aingie Facebook na kuwajibu wahalifu hao, kamwe hatafanya hivyo kwani anaweza kuchochea taarifa mbaya zaidi kuliko sasa.
“Nimekataa kwa sababu kama wahalifu wameweza kuniundia akaunti na Dola imeshindwa kunilinda, nikiunda akaunti yangu wataiingilia na hiyo na wataandika mabaya kuliko wanayoyaandika”alisema.
Dk. Chami alisema kama wahalifu hao wataweza kuingilia akaunti yake na kuandika mabaya zaidi kwenye akaunti yake halali, watasherehekea na kuhalalisha uovu wao huo.
Soma taarifa yake kamili hapa chini
Naitwa Dr Cyril August Chami,  Mbunge wa Moshi Vijijini Mkoa wa Kilimanjaro,  Tanzania.  Kwa miezi kadhaa sasa kuna mtu au kikundi cha watu ambaye/ambacho kimeunda akaunti feki kwenye Facebook kwa jina langu na kuitumia akaunti hiyo.

kunichonganisha na Chama cha Mapinduzi (CCM) na viongozi mbali mbali nchini Tanzania kwa lengo kuu moja: kunipaka matope na kuichafua taswira yangu mbele ya umma na ndani ya CCM. 

Wanachokilenga (na hapa natumia wingi kwa sababu ndivyo nimeelezwa na Cyber Crime Unit of the Police Force Tanzania) ni kupambana nami kupitia mitandao ili tu 2015 nisiteuliwe na CCM kuendelea kugombea ubunge Jimbo la Moshi Vijijini,  ateuliwe mwanachama mwingine wanayemtaka wao!
Kwa kujifanya wao ni mimi, wanapingana na misimamo yote ya CCM. Kwa mfano, wanadai kuwa kwenye mchakato unaoendelea wa Bunge la Katiba, mimi napendelea serikali tatu. Eti mimi napendelea kura ya siri katika Bunge la Katiba linaloendelea.

 Naonyeshwa kuwa mtetezi wa CHADEMA.  Hata katika uchaguzi uliofanyika March 16 Kalenga eti naonyeshwa "kutabiri" ushindi wa CHADEMA na pia eti "nimetabiri" ushindi wa CHADEMA Chalinze! 


Naonyeshwa nikijinasibu kuwa eti Chama changu CCM huwa kinashindwa chaguzi ndogo, kwa hiyo na hizi mbili CCM ijiandae kushindwa! Wahalifu hawa wanayatuma maoni haya yote kwa niaba yangu huku wakisahau kabisa kuwa ni hivi majuzi tu tarehe 9 Februari CCM ilivigalagaza vyama vya upinzani kwenye uchaguzi MDOGO wa madiwani kwa kushinda katika kata 23 kati ya kata 27. 

Ama kwa makusudi kabisa, ama kwa upungufu wao wenyewe wa kumbukumbu, au kwa ushabiki wao kwa upinzani, wanatabiri kwa  niaba yangu kuwa CCM ni dhaifu kwenye chaguzi ndogo, kitu ambacho ni kichekesho kwa sababu takwimu ziko wazi: 

CCM imewika uchaguzi mdogo wa madiwani, CCM imewika Kalenga, na kila mtu anayefahamu siasa angalau ya darasa la saba anajua kuwa CCM itawika Chalinze!

Kutokana na uhalifu huu, nimechukua hatua zifuatazo:
Kwanza nimeikana akaunti hiyo ya Facebook. Siyo yangu na situmii mitandao ya kijamii katika siasa kwa sababu kuu mbili. 

Sababu ya kwanza ni kwamba asilimia kubwa ya walioniajiri yaani wapigakura wa Moshi Vijijini hawatumii mitandao ya jamii. Kwa hiyo hata kama ningeandika mafanikio yote ya uongozi wangu kwenye Facebook ni asilimia ndogo sana ya wapiga kura wangu ingenisoma. Ni kweli kuwa Watanzania wanaoishi mijini au kwenye diaspora wangeelewa, lakini mwisho wa yote wengi wao hawatapanda ndege au magari ili tu kwenda Moshi Vijijini kunipigia kura.  

Nitoe mfano kuwa mwaka 2005 ilipigwa kura ya maoni kwenye mtandao mmoja wa jamii kuhusu nani angeshinda ubunge Moshi Vijijini. Mgombea wa CHADEMA "alishinda" kwa asilimia 80. Mimi "niliambulia" asilimia 20. Kwenye uchaguzi "halisi" nilipata kura 49,000 na mgombea wa CHADEMA akapata kura 18,000!
Pili, badala ya kuandika kwenye Facebook au mitandao mingine ya kijamii, nimegundua njia rahisi na yenye uhakika ya kuwaongoza wananchi walionichagua. Njia hiyo ni kuwafuata huko waliko. 

Katika miaka takriban tisa ya ubunge wangu nimewatembelea wapiga kura wangu walio katika vitongoji 322, vijiji 67 na kata 16 kuliko mbunge mwingine yeyote tangu Tanzania iwe huru. Kwa hakika, takwimu zinaonyesha kuwa jumla ya ziara zangu za miaka tisa inaizidi jumla ya ziara za watangulizi wangu wote kwa miaka 40. 
Hii haina maana kuwa sikutani na wapiga kura wangu wanaoishi nje ya jimbo. La hasha! Bado nakutana nao. Kwa mfano, tarehe 2 Februari mwaka huu nilikutana na wapiga kura wangu wanaotoka Kata ya Uru Mashariki (Kinyamvuo) waishio Dar es Salaam ukumbi wa Chuo cha Maji.

 Baada ya kuwaeleza hali ya kata yao na kuyajibu maswali yao, msemaji aliyesimama kunishukuru, Mheshimiwa DC mstaafu Clemence Orauya, alikiri kuwa katika hadhira ile ya watu karibu 300 hakuweko mtu anayeifahamu jiografia ya kata ile kama mimi, japokuwa mimi si mzaliwa wa kata hiyo. Aliungwa mkono na karibu kila aliyehudhuria. 
Kwa ufupi, Facebook haiwezi kumfikia mwananchi aliyeko kitongoji cha Uhondo au Saningo au Mandaleni au Msarikie ambako kote hakuna umeme achilia mbali mtandao; mbunge anaweza. Facebook haiwezi kusimamia ujenzi wa barabara za Kibosho na Uru kwa kiwango cha lami; mbunge anaweza.

Facebook haiwezi kuikumbusha Serikali  ianzishe ujenzi wa barabara ya lami ya Old Moshi kama ilivyoahidiwa; mbunge anaweza. Facebook haiwezi kusimamia sekta ya elimu Moshi Vijijini;  mbunge anaweza. Facebook haitatatua tatizo la maji katika Skimu ya Umwagiliaji Lower Moshi; mbunge anatatua kwa kuwashirikisha wadau mbalimbali.
Hatua ya pili niliyochukua ni kuwasiliana na uongozi wa CCM ngazi za wilaya, mkoa na taifa kuwaeleza juu ya uwepo wa uhalifu huu. Hivyo, picha inayotengenezwa kuwa mimi ni msaliti ndani ya CCM ni sawa na kumtupia tope mtu aliyejipaka mafuta! Tope zote zinadondoka bila kumchafua mlengwa.
Hatua ya tatu ni kutoa taarifa Makao Makuu ya Polisi Dar es Salaam Kitengo cha Makosa ya Uhalifu kwenye Mitandao (Cyber Crime Unit) ili wanisaidie kuifunga hiyo akaunti na kuwakamata wahalifu. Kwa masikitiko makubwa sana wameshindwa yote mawili. Hadi leo akaunti inatumika; hadi leo naendelea kutengenezewa maadui ndani ya CCM na kwa viongozi wa juu wa nchi; na hadi leo wahalifu hawa wako huru wakiendelea kuchekelea maumivu haya wanayonisababishia. 

Nina hakika watakaposoma ujumbe huu watakuwa hawana mbavu kwa vicheko huku wakijipongeza kwa kuyafanikisha malengo yao.
Kwa masikitiko makubwa zaidi, kiongozi wa Cyber Crime Unit ameniambia wameshindwa yote mawili!!!! Wameshindwa kuifunga akaunti hiyo;

na wameshindwa kuwatambua wahalifu hao, na kwa maana hiyo wameshindwa kuwakamata. Walichofanikiwa hadi sasa ni jambo moja tu, nalo ni kugundua kuwa uhalifu huu unafanywa na kikundi cha watu waliojipanga kiujanja kiasi kwamba wao (Cyber Crime Unit) wamewashindwa. Tena akaniambia waliomba msaada Mamlaka ya Udhibiti wa Mawasiliano Tanzania (Tanzania Communications Regulatory Authority-TCRA) ili akaunti hii ifungwe, nao TCRA wameshindwa!
Nayaandika haya yote kwa sababu mbili. Sababu ya kwanza ni ile inayotegemewa na msomaji yeyote, nayo ni ile ya haki yangu binafsi. Naamini ninayo haki ya kulindwa kutokana na uhalifu huu kama msomaji yeyote alivyo na haki hiyo. Binafsi natambua wahalifu hawa wanachokilenga ni kimoja tu: Dr Chami asiwe tena mbunge wa Moshi Vijijini kuanzia 2015.

 Wanajua hadi sasa hakuna mwana CCM mwenye ubavu wa kunishinda katika kura ya maoni mwakani. Hivyo njia pekee ni kunichonganisha na wakuu wangu wa CCM ili nitakaposhinda kura ya maoni, ngazi za juu za CCM ziache kuniteua ateuliwe mtu mwingine. Kwao haijalishi kama mgombea huyu mbadala atakipatia ushindi CCM.


 Kwao ni heri upinzani uchukue jimbo lile kuliko Dr Chami awe mbunge. Kwa ufupi, hawa sio wapenzi wa CHADEMA au CCM. Ni wababe wenye fedha wanaoamini wana uwezo wa kumuinua yeyote awe mbunge na kumshusha yeyote asiwe mbunge.


 Na kwa sababu walishanieleza nia yao hiyo na nimeyaeleza haya yote kwa Polisi, najisikia huru kuwaeleza wasomaji kiini cha tatizo lenyewe. Kiini ni kwamba mbabe mmoja mwenye fedha amekasirishwa nami kwa sababu nimekataa maagizo yake kuwa nimsaidie swahiba wake anayewania Urais 2015! 


Niliikataa kazi hiyo kwa sababu moja tu: Haina maslahi kwa Taifa wala Moshi Vijijini!!!!! Mimi nitamuunga mkono mgombea Urais yeyote atakayechaguliwa kwenye mkutano mkuu wa CCM, siye mgombea ninayelazimishwa nimuunge mkono nje ya mfumo halisi wa CCM na kinyume na dhamira yangu.
 
Haitanishangaza ikithibitishwa kuwa mbabe huyu ndiye anatoa fedha kuufadhili mtandao huu wa wahalifu, japo hii ni kazi ya Polisi na ni kazi inayoendelea. Kama mtandao huu utashinda au utashindwa ni jambo la "tusubiri tuone". 

Ninalothibitisha kwa wasomaji ni kuwa mimi nitaendelea kuwa mwaminifu kwa wapigakura wangu wa Moshi Vijijini na kwa Chama cha Mapinduzi (CCM). Wao wakiamua niendelee kuwawakilisha nitaendelea.  Wakinitaka nipumzike nitayaheshimu maamuzi hayo na nitafanya mambo mengine. Ikumbukwe kuwa kabla ya kuwa mbunge sikuwa barabarani.  Nilikuwa nafanya kazi na nitaendelea kufanya kazi.
 
Sababu ya pili iliyonifanya niandike ujumbe huu ni kuonyesha hofu yangu kwa nchi yetu ya Tanzania  kuwa uhalifu unaweza kufanywa NA VYOMBO HUSIKA VYA DOLA VIKAKIRI KUSHINDWA. The Cyber Crime Unit of the Police Force and the TCRA have both confirmed their helplessness on this matter! 
Hii ina maana gani?
Ina maana kuwa wakimalizana nami watafanya hivyo kwa yeyote wanayemchukia na vyombo vya dola vitakiri kuwa haviwawezi. Lakini mbaya zaidi, wataiingilia sekta ya fedha na kuwaibia wananchi bila huruma na vyombo vya dola vitakiri kuwa hawawawezi wahalifu hawa!
 
Nimeshauriwa na Cyber Crime Unit kuwa nami niingie Facebook kuwajibu wahalifu hawa. Nimekataa kwa sababu kama wahalifu wameweza kuniundia akaunti na dola imeshindwa kunilinda, nikiunda akaunti yangu wataiingilia na hiyo na wataandika mabaya kuliko wanayoyaandika kwenye akaunti waliyounda wao. 

 Hii ni kwa sababu kwenye akaunti waliyounda wanaogopa kufanya uharibifu mkubwa wakijua kuwa siku si nyingi watagunduliwa. Lakini wakiweza kuiingilia akaunti niliyoisajili mwenyewe watasherehekea kwa sababu wataweza kuandika mabaya zaidi kupitia akaunti yangu halali na kuyahalalisha kabisa haya ambayo wameshaandika. 


 Hapo hata wale wasomaji wanaoamini kuwa nahujumiwa wataniona msanii na CCM wataniita rasmi msaliti. Lengo la wahalifu litatimia na Cyber Crime Unit wataendelea kuniambia wameshindwa kuwapata "perpetrators" hao.
Wasalaam,
Dr Cyril Chami.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...