https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Thursday, March 27, 2014

TAZARA waomba kadi za uanachama Simba


Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
KLABU ya Simba, Makao Makuu, imeombwa kufanya haraka kuwapatia kadi za uanachama wapenzi wote wanaopatikana katika Tawi la Simba la Shirika la Reli la Zambia na Tanzania (TAZARA), ili kuwapatia nafasi ya kushiriki shughuli za kimaendeleo.
Wadau wakiwa katika picha ya pamoja baada ya uzinduzi wa tawi la TAZARA, lenye maskani yake jijini Dar es Salaam. Mwenye fulana ya mistari na kofia nyeusi ni Katibu Mwenezi wa tawi hilo, Alfredy Mdemu. Mwenye fulani nyekundi Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano ya Simba, Swed Mkwabi.

Akizungumza leo mchana jijini Dar es Salaam, Katibu Mwenezi wa tawi hilo, Alfredy Mdemu, alisema kuwa tawi lao lenye watu 176, ni wanachama 60 wenye kadi za klabu hiyo ya Simba SC.

Alisema hali hiyo inawapa wakati mgumu jinsi ya kuwabana katika kuiletea maendeleo, huku wakiamini kuwa wote wana mapenzi na klabu yao.

“Tumejitahidi kufungua tawi hili kwa ajili ya kuhakikisha kuwa wanachama wote wanafanikisha mambo ya kimaendeleo ya Simba, hivyo tunaomba kwa dhati kabisa klabu yetu iwape kadi wale walioomba,” alisema.

Naye Makamu Mwenyekiti wa tawi hilo, Amri Hussein, alisema kuwa wamefuata taratibu zote za kuwaombea uanachama watu wote wanaopatikana katika tawi lao la TAZARA.

“Endapo tutafanikiwa kuzipata kadi za wanachama wote wanaopatikana kwetu, hata sisi viongozi wao tunaweza kutafuta namna ya kuwabana kwa ajili ya kushiriki mambo ya kuiendeleza klabu yetu,” alisema.

Klabu ya Simba ni miongoni mwa klabu zenye wapenzi wengi, ikiwa ni kutokana na kuasisiwa kwake mwaka 1936, kama ilivyokuwa Yanga SC.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...