https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Thursday, August 01, 2013

Aibu hii ya Taifa Stars, Watanzania tuweke wapi sura zetu?


Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
MIMI ni miongoni mwa Watanzania waliofahamu matokeo ya kuondoshwa kwenye michuano ya kuwania kufuzu kwa Kombe la Mataifa Afrika kwa wachezaji wa ndani (CHAN), dhidi ya Uganda.
Juma Kaseja, kipa wa Taifa Stars
Ingawa nimeumizwa na matokeo hayo ya kupigwa bao 3-1 nchini humo katika mechi ya marudiano, ikiwa ni mfululizo wa ushindi baada ya kushinda pia bao 1-0 jijini Dar es Salaam, hivyo Uganda ‘The Cranes’ kushinda kwa mabao 4-1 na kuwaondosha Stars kwenye mbio hizo.



Kelvin Yonda, akiwa uwanjani
Wachezaji wetu walishafungwa kabla ya mechi kumalizika, hasa baada ya kukubali pia kufungwa katika mchezo wa kwanza uliochezwa katika Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam.



Pilikapilika uwanjani kati ya Stars na Uganda
Hii ni aibu ya aina yake na Watanzania wote, wakiwamo viongozi wa soka lazima wafahamu tunahitaji kuacha siasa na kufanya juhudi ya kunyanyua soka letu linalokwenda kwa kusua sua.

Nchi za wenzetu kama vile Kenya na Uganda wamekuwa wakisonga mbele siku hadi siku. Watanzania bado tupo pale pale. Kama hatuoni aibu hii.

Wakati mwingine tunashangilia matokeo ya kugongeana pasi tatu au nne kwa wachezaji wetu, ila bado haisaidii kupata dawa ya mwarobaini wa soka letu.

Ni aibu kubwa kwa timu kama Taifa Stars yenye wachezaji wenye majina makubwa kama vile Mrisho Ngassa, Juma Kaseja, John Bocco, Kelvin Yondan na wengine wanaotikisa katika ligi ya nyumbani.

Siku chache kabla ya kuelekea nchini Uganda, Kocha wa Stars, Kim Poulsen alijigamba mno juu ya mchezo huo wa marudiano, akiamini Stars itampa shangwe.

Alifahamu Stars ingetoka na ushindi wa bao 2-0, ukizingatia kuwa Uganda wao walishinda bao 1-0 wakiwa Tanzania.

Hajafahamu kuwa wenzetu Uganda wamefahamu mapungufu yetu yanayowafanya wao waibuke na ushindi katika kila mechi.

Kufundishwa na kocha anayeijua vizuri Tanzania na wachezaji wake kwa ujumla, Milutin Sredejovic Micho wa nchini Serbia, ambaye aliwahi kuinoa timu ya Yanga ya Dar es Salaam kwa miaka kadhaa, hivyo ushindi wa bao 4-1 wameupata kwa haki.

Ili tuweze kusonga mbele, ni pamoja kwa viongozi wetu pamoja na wanamichezo kwa ujumla kubaini makosa yao kwa ajili ya maendeleo yetu.

Ni ajabu licha ya mashabiki kuwa na kiu kubwa ya kimaendeleo, ila juhudi zetu hizo zinashindwa kufua dafu, jambo linalowakera wengi.

Stars hii inayopigwa bao 3-1 na Uganda, bado inaweza kushabikiwa na watu kujaza uwanja? Hata wawe na mapenzi ya kiasi gani, watachoka.

Lazima tujuwe mapungufu yetu na kuendeleza wachezaji wenye vipaji na kulitumikia Taifa.

Ukiangalia mechi zote mbili za Uganda na Stars, utabaini kuwa pengo la Mbwana Samatta na Thomas Ulimwengu limeonekana waziwazi.

Hawa wanacheza soka nchini Congo, katika klabu ya TP Mazembe, hivyo CHAN hawaruhusiwi.

Ukiacha Samatta na Ulimwengu, Stars iliwakosa wachezaji wawili wengine, Shomari Kapombe aliyekwenda nchini Uholanzi kufanyiwa majabirio ya kucheza soka la kulipwa, huku Mwinyi Kazimoto naye akiwa nchini Qatar.

Kama hivyo ndivyo, bado hatuwezi kukaa na kulaumu kwanini vijana hawa hawapo Stars, hasa kama tungekuwa na nyota wengine.

Lakini hatuna jipya. Tunaweza kuvuna tu bila kupanda, huku tukiwa wepesi kutoa majigambo wakati tunajua fika soka halichezwi mdomoni.

Tanzania ni nchi yenye wachezaji wengi wenye vipaji, ila ubaya wetu hatujui thamani hiyo. Wachache wanaonekana kwa juhudi zao.

Hata ligi zetu zinazoshirikisha vijana hazina mvuto, huku tukiwa wepesi kuweka udugu katika mambo yenye umuhimu mkubwa.

Wadau wakubwa wa michezo, Kampuni ya Coca-Cola, inaendesha mashindano ya Copa Coca-Cola, ila wanapotokomea hakujulikani.

Wazo la kuendesha mashindano haya ni zuri, ila tunatumia fursa vizuri ili kuondoa ukame wa kushiriki michuano mikubwa, kama vile Kombe la Mataifa na lile la Dunia?

Zaidi jukumu la kuendeleza soka la vijana linaachwa kwa wamiliki wa timu ya Azam FC. Hawa wanaandaa timu (B), kati ya zile zinazoshiriki ligi kuu.

Mtu huyo huyo mmoja ambaye timu yake naye inashiriki katika michuano hiyo, eti ndio mdhamini mkuu. Hili ni tatizo kubwa kwa soka letu.

Japo hakuna matatizo katika mashindano hayo, ila malalamiko hayawezi kwisha juu ya suala hilo, japo huo ni msaada mkubwa.

Shirikisho la Soka nchini (TFF), chini ya Rais wake, Leodgar Tenga, anapaswa kukaa chini na kuona kuwa anaondoka huku akiwa hana jipya alilofanya katika kipindi chote cha uongozi wake.

Taifa Stars haijaweza kushiriki michuano mikubwa zaidi ya kushuhudia malalamiko ya kila siku. Hatuna la kujivunia hata kwa wachezaji vijana, ambao ndio msingi wa soka letu.

Ndani ya utawala wake, tumeshuhudia vuta nikuvute ya Uchaguzi wa TFF ambapo hadi sasa hakuna kilichofanyika, huku tukitia aibu zaidi kuwaita wajumbe wa FIFA kuja kusimamia masuala ya uchaguzi wetu na kushangaza Dunia.

Ligi ya TFF katika mikoa yote hakuna ushindani wowote, maana timu hizi zinachangamoto kubwa, huku wasimamizi wa soka wenyewe TFF, wakiendelea kulala usingizi wa pono.

Ni jambo la kushangaza kuona viongozi wa soka wanaangalia zaidi mechi kubwa za Simba, Yanga pamoja na timu za Taifa hata kama itafungwa wakiamini mapato mengi yataingia.

Ndio maana nasema tuacheni ubabaishaji. Tushikwe na uchungu wa kweli juu ya soka letu. Tuwekeze kwenye soka la vijana, sanjari na kuendesha ligi za mikoani zinazoweza kuzalisha wachezaji wenye uwezo wa kucheza soka na kuitumikia pia timu ya Taifa inayotia aibu Barani Afrika.

Narudia tena, Tanzania ina wachezaji wengi wazuri kiasi cha kuweza kufanya lolote, isipokuwa hatujafahamu makosa yetu na kujikuta kila siku tukibaki pale pale wakati wenzetu wanachanja mbuga.
+255 712 053949

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...