https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Wednesday, August 21, 2013

MGODI UNAOTEMBEA: Hatuna mipango, hatuwezi kujikwamua kiuchumi



Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
BINADAMU anazidi kuandamwa na mabalaa mengi, yakiwamo mabaduliko ya tabia nchi yanayosababishwa na uchafuzi wa mazingira sehemu mbalimbali duniani.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete
Uzalishaji viwandani na ukataji wa miti usiozingatia utamaduni wa kutunza mazingira yanasababisha mkanganyiko mkubwa duniani.

Kama hivyo ndivyo, walau sasa kunahitaji maandalizi ya kutosha. Kinyume na hapo, Tanzania kama moja ya nchi zinazoathiriwa na suala hilo, itajiweka katika mazingira magumu.

Jamii ya Tanzania na Serikali kwa ujumla inahitaji kuliangalia hilo kwa mapana, ikiwa ni pamoja na kutunza mazingira ili iwe chanzo cha watu kuishi katika Dunia salama.

Bila kuzingatia hilo, hata wakulima wetu wa Tanzania hawawezi kuishi maisha bora ukizimngatia kuwa mazao yao mengi yanashindwa kustawi kutokana na ukosefu wa mvua au kunyesha bila mpango.

Tanzania inaamini kuwa uchimi wake ili ukuwe kunahitajika juhudi za wakulima wetu waliosambaa kwenye mikoa mbalimbali.

Je, Watanzania wangapi wanamasika katika kujishughulisha na kilimo? Je, ni vijana wangapi wanajiingiza kwenye sekta hiyo iliyopewa jina la uti wa mgongo?

Hayo yanasababisha watu wengi kuona hawawezi kuishi bila kufanya kazi za kuajiriwa, ikiwa ni tofauti na uzalishaji mali kwa kupitia sekta ya kilimo yenye changamoto mbalimbali.

Wanafanya hivyo bila kujua kuwa sekta ya kilimo ndio inayoweza kutoa nafasi nyingi za ajira, tofauti na fikra za waliokuwa wengi.

Mbali na kujiongezea kipato kwa kujiingiza kwenye kilimo, pia tunaweza kujiweka kando na baa la njaa kwa kuhakikisha kwamba tunakuwa na akiba ya kutosha, tofauti na sasa kila wakati kusikia habari mbaya zinazohusu njaa kwa vijiji na wilaya mbalimbali za Tanzania.

Njaa barani Afrika ni tatizo kubwa. Ndio maana  Nchi nane tajiri duniani, maarufu kama G-8, zimekuwa zikifanya mikutano ya kila wakati kujadili namna ya kupambana na hilo.

Katika mikutano hiyo, nchi ya Tanzania ni miongoni mwa zile zinazojadiliwa mara kwa mara kwa ajili ya kupewa misaada, ambapo hata hivyo sio jambo geni kutokana na viongozi wake kuona hilo ni jambo la maana kwao.

Pamoja na misaada hiyo inayotolewa mara kwa mara kutoka kwenye mashirika ya Kimataifa au serikali, ila ni vipi tunaweza kufanya kazi hiyo kwa unafanisi kwa ajili ya kuboresha maisha yetu?

Hii ni kwasababu baadhi ya viongozi wengi wa Tanzania ni wasemaji wasiozingatia vitendo katika harakati zao. Tunaishi kwa ahadi. Tutafanya hivi na kufanya lile, ila hakuna kitu. Ndio maana hata kwenye kujikita katika suala la kilimo bado hatuna jipya.

Mipango yetu mingi inaishia kwenye makaratasi. Kwa miaka 51 ya uhuru, kumekuwa na mipango mingi ingawa yote haina matunda. Hadi leo, bado hatuwezi hata kujiendesha wenyewe.

Serikali pia inashindwa kuwaongoza wakulima kama inavyotakiwa sambamba na kuwapatia pembejeo za kilimo, kuwa karibu nao kila wakati, hasa wakati wa majanga ya wadudu kushambulia mazao yao.

Suala hili ni kati ya changamoto nyingi zinazoongeza joto la ugumu wa maisha, maana wote wanakosa akiba ya chakula cha kujikimu wao na familia zao sambamba na kuuzwa nje.

Mwaka 2008, Serikali na wafanyabishara waliweza kukaa na kuliangalia hilo suala la kilimo. Lakini mpango wa kuendeleza kilimo, naweza kusema kwamba haukufanikiwa kwa vitendo.

Kitendo cha kukaa pamoja, ni kuonyesha kwamba wanatambua changamoto za kilimo, lakini ajabu ni maoni yao yanavyoishia kwenye karatasi.

Hii ni mbaya na ndio sababu ya nchi inakwenda ndivyo sivyo na hakuna mipango ya kuinusuru zaidi ya kusubiria hisani kutoka kwa wengine. Nchi sasa inaendeshwa kwa hisani ya watu fulani.
Tumekubali kuwa watu wa misaada kutoka kwa wanaojiweza. Tukiliangalia hili, kila mtu ataelekeza lawama zake kwa serikali, ambayo kwa bahati mbaya ipo chini ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Hapo tutasema na kujikuta kuamini kumbe tatizo ni serikali ya CCM inayoongozwa na Rais Jakaya Kikwete. Hawa wameshindwa kabisa kutuletea maisha bora kwa kila Mtanzania. Na wameshindwa walau kuwasimamia na kuwaendeleza wakulima ili kazi zao zikuze uchumi wa Taifa lao. Nao wanufaike ili waone kazi hiyo ni nzuri.

Wameshindwa hata kusimamia sera ya kilimo kwanza walioasisi kwa mbwembwe nyingi. Pamoja na yote hayo, je Watanzania nao wamekubali kukaa na kusubiria ahadi za serikali?

Watu wa aina hiyo wapo wengi katika jamii. Wanalalama sana. Hata hivyo, wale ambao pamoja na kukabiriwa na changamoto za aina hiyo lakini wanajihusisha na kilimo hoja wanayo.

Ni wakati wa kukaa chini na kuamua sasa tufanye kazi za kweli kwa ajili ya kuinua uchumi wa Taifa letu, ikiwamo changamoto zinazowasumbua wakulima wetu ziweze kufanyiwa kazi.

Kama serikali inashindwa kuwakopesha wakulima walau kiasi kidogo cha pesa, tunawezaje kuwaongezea morali wa kufanya kazi?

Hii vita ya tatu ya Dunia ambayo ni maji na chakula, hakika kwa sisi Watanzania, upo uwezekano wa kutuangamiza.

Maana wenyewe hatuna na mipango wala uelewa wa kujiingiza kwenye kilimo. Katika sekta hiyo kuna matatizo mengi mno.

Zipo sehemu zilizokumbwa na migogoro mikubwa ya wakulima wakubwa na wadogo. Hilo linapaswa kuangaliwa upya kwa ajili ya kuhakikisha tunainua uchumi wetu.

Bila hivyo vita ya umasikini ama maisha bora kwa kila Mtanzania ni ndoto. Hatuwezi kusonga mbele kama hatuna mipango endelevu ya utendaji kazi kwa vitendo na sio porojo na hadithi.

Tufanye kazi kwa nguvu zote ili tuweze kukwamua uchumi wetu kwa kupitia sera ya kilimo. Kilimo kinachoweza kufanywa na kila mmoja wetu na sio kukaa na kusubiri hisani ya Wamarekani kama tulivyozea.

Hapa sina lengo la kulaumu upande wowote, maana mambo hayo licha ya kushamiri sana, ila hayajaweza kutusaidia. Malalamiko ya wapinzani bado sio suluhu la kuwapatia maisha bora kwa Mtanzania kama wote hatuna uthubutu katika utendaji wa kazi.

Tunahitaji moyo wa uzalendo, ushirikiano kwa ujumla, maana ndio mbeleko ya kutuweka katika nafasi nzuri na kuacha kasumba zisizokuwa na mpango wowote ule.

Huo ndio ukweli wa mambo. Kuna mengi yametufanya tushindwe kusonga mbele, ikiwa ni pamoja na kutojua makosa yetu, hasa kuachia sekta muhimu kama kilimo kuendeshwa kienyeji.

Suala kama hilo tusipokuwa makini nalo basi hakuna tutakachoweza zaidi ya kusubiria hisani ya Wazungu. Na bado tujiandae kusubiria chakula kutoka kwao, wakati Tanzania ina ardhi kubwa yenye rutuba.

Hakuna tutakachopata zaidi ya aibu, maana licha ya kuzunguukwa na mapori kila mahali, kama vile Tanga, Rukwa, Morogoro, Mbeya, Iringa na mikoa mingine ila hatuwezi kuitumia ipasavyo.

Suala la kilimo linahitaji mkazo na watu wote bila kuangalia nafasi zao kwenye jamii ili tija kwao.

Kila Mkuu wa Wilaya na Mkuu wa Mkoa, lazima ahakikishe kwamba katika eneo lake, wananchi wake wanatembelewa na kusaidiwa katika kazi zao za kilimo.

Pale wakulima wanapovamiwa na wadudu hatarishi, Serikali iwasaidie kwa kuwanunulia dawa, pembejeo za kilimo na sio kuwaangalia tu, maana huo sio mtindo utakaonusuru sekta ya kilimo.

Tukiweza kufanya hivyo, sio tu tutakuwa na akiba ya chakula, bali pia tunaweza kuingiza fedha za kigeni kwa kuuza nje  na kukuza uchumi wa Taifa letu.

kambimbwana@yahoo.com
+255 712053949

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...