https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Tuesday, August 20, 2013

Ulaji wa Kapombe Ufaransa waitikia kiburi klabu ya Simba



Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
MCHEZAJI wa zamani wa Simba, Shomari Kapombe, amepata ulaji baada ya klabu yake ya Simba, kumuunganisha katika klabu ya AS Cannes ya nchini Ufaransa kwa makubaliano kuwa atakapouzwa Wekundu hao wa Msimbazi wapate mgao wao.
 
Shomari Kapombe mbele, akiwa kwenye heka heka za timu ya Taifa, Taifa Stars

Hayo yamebainika kwa kupitia Mwenyekiti wao Ismail Aden Rage, ambapo Simba imekubali mchezaji huyo achezee timu hiyo ya Ligi Daraja la nne nchini humo kwa makubaliano ya makubaliano ya kumtafutia timu ya kucheza ndani ya miaka miwili.

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, Ofisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga, alisema kuwa timu hiyo itamgharimia Kapombe kwa kila kitu wakati atakapokuwa nchini Ufaransa, ikiwa ni sambamba na kutafuta timu ya kuchezea soka la kulipwa.

Alisema endapo Kapombe atauzwa kwenda katika timu nyingine yoyote, Simba itapata gawio lake kupitia mauzo hayo na lengo la mchezaji huyo kubaki Ufaransa ni kumtengeneza ili awe kwenye kiwango bora zaidi.

“Katika makubaliano hayo, Simba haitapata chochote kwa sasa, isipokuwa pale atakapopata timu nyingine ya kuchezea, utaratibu ambao umekuwa nuru kubwa kwake sanjari na kumuwekea mazingira mazuri ya kukuza soka lake.

“Naamini mambo yatakwenda sawa kwa kuhakikisha kuwa Kapombe anafika mbali katika mpira wa miguu duniani, ambapo makocha wa Ulaya wamebaini kuwa Kapombe ni mchezaji mzuri anayehitaji kuboreshewa kwa baadhi ya vitu ili aje kuwa nyota duniani,” alisema.

Wakala wa Kapombe, Denis Kadito, alisema ingawa Kapombe ameonekana kuwa mchezaji mzuri, kutofahamika kwa jina la Tanzania kumekuwa kikwazo kikubwa kwa kupata kwake nafasi ya moja kwa moja na ndiyo maana imebidi aanzie kwenye hatua ya chini.

Kutokana na mkataba huo wa Kapombe na Cannes, Simba sasa imeongeza mkataba wake na mchezaji huyo kwa muda wa miaka mitatu zaidi, kwa vile mkataba wake wa sasa unamalizika Aprili mwakani, huku akirejea katika klabu yake endapo hatapata timu ndani ya miaka miwili.



No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...