https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Saturday, August 31, 2013

DIAMOND PLATNUM: Kutoka Tandale hadi Serena Hotel kuweka historia mpya kimuziki


Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
KAMA kuna watu hawataki kuamini kuwa msanii Nassib Abdulmalick maarufu kama 'Diamond Platinum' ni mkali na mwenye ukwasi wa kutosha tu, huu ndio muda wao wa kuamini kinachosemwa.
Hapa Diamond akiwa nchini Uingereza kwenye safari zake za kimuziki.
Ni pale alipoweza kuwakusanya wasanii, wadau wake na waandishi wa habari katika hoteli ya Serena, iliyopo jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kuzindua video ya wimbo wake ujulikanao kama My Number 1.
Diamond alipokuwa anamkabidhi gari lake mzee Gurumo.
Watu wengi wanataka kusikia kinachotakwa kusemwa na msanii Nassib Abdulmalick ama Diamond Platinum kama anavyopenda kutambulika hivyo katika tasnia ya muziki wa kizazi kipya.
Msanii Diamond alipokuwa akizungumza wageni wake aliowaita katika Hoteli ya Serena, juzi jijini Dar es Salaam.
Wapo waliokuwa wakibashiri labda anataka kumtambulisha mpenzi mwingine kama ilivyokuwa kawaida yake. Hizi zilitokana na kauli ya msanii Diamond alipowakalibisha wadau walioalikwa katika tukio la kuonyesha video yake mpya ya ‘My Number 1’.

Hakika kulikuwa na maswali kadhaa yaliyoshangaza wengi. Kwanini Diamond? Huyu ni nani? Mbali na kutaka kuonyesha video yake mpya, kipi kingine anataka kusema?

Ikumbukwe huyu ni miongoni mwa wasanii waliozaliwa katika familia za kimasikini mno ndani ya ardhi ya Tanzania. Amekulia katika mitaa ya kifukara, Tandale jijini Dar es Salaam.

Mbali na kuzaliwa katika familia hiyo, Diamond wa leo anatajwa kuwa moja ya wasanii matajiri hapa Tanzania. Kwa kushihirisha hilo, Diamond amekuwa msanii wa kwanza wa kizazi kipya kuweza kuandaa tukio la aina yake katika hoteli ya nyota tano, yani Serena Hotel.

Amealika wadau kadhaa wa muziki akiwamo Mzee Muhdin Gurumo, bila kusahau waandishi wa habari. Miaka mine iliyopita, Diamond alikuwa na ndoto za kuhakikisha kuwa Tandale wanaishi kwa raha kwa kuwapatia huduma muhimu, ikiwamo misaada ya kujikinga na malaria.

Kwa kawaida hali ndani ya Hoteli ya Serena ilikuwa shwari na kilaa mmoja kuwa na mshawasha wa kuangalia kila kinachojiri kwenye pilika pilika hizo za Diamond wa Tandale hadi wa Serena.

“Maisha yangu yamekuwa yakichangiwa mno na kujituma kwangu, kufanya kazi kwa bidii bila kuchoka, ndio maana nimekuwa nikifikia katika mazingira kama haya,” alisema Diamond.

Wakati hayao yakijiri ndani ya viunga hivyo ambapo idadi kubwa ya watu ilikuwa imejitokeza kama vile Profesa Jay, Mwana FA, AY, Madee, Queen Doreen, Sheta bila kusahau nyota wa filamu Tanzania, wakiongozwa na Jacob Stephen, Vicent Kigosi Ray, Irene Uwoya na wengine wengi, watu walikuwa wakiendelea kujadili hili na lile, sanjari na kupata vinywaji kupoza makoo yao.

Msanii huyo anayeijua vyema kazi yake, aliweza kupanda jukwaani na kufanya shoo moja matata, ikiwa ni utambulisho wa mtindo mpya wa uchezaji katika video yake hiyo.

“Hii video yangu nimeifanya nchini Afrika Kusini ambapo iliweza kunigharimu Shilingi Milioni 50 za Kitanzania sanjari na kunifanya nionekane Diamond mpya kabisa.

“Ukifanya kazi nzuri ni sababu ya kukupandisha juu, japo katika kuandaa video hii nilichanganywa na vitu vingi, hasa mazingira mazima ya kuhakikisha nafanya kazi nzuri,” alisema.

Wakati hayo yakiendelea, msanii Diamond alishika tena kipaza sauti kwa ajili ya kuzungumza jambo jingine ambalo alikusudia kuwaambia Watanzania.

Ni pale alipotangaza kumnunua gari mwanamuziki mkongwe Muhdin Gurumo, aliyetangaza kustaafu muziki akiwa ndani ya bendi ya Msondo Ngoma.

Diamond anasema kuwa alishikwa na uchungu alipomsikia mzee Gurumo akilalamika kuachana na muziki huku akiwa hana chaa kujivunia, jambo ambalo kwake linamkera.

Aidha, hayo yote yametokea yakichaangiwa pia na Gurumo kuwaambia Watanzania kuwa anapenda kazi za Diamond, akiwa ni msanii anayefanya vyema katika tasnia hiyo.

“Jambo hili lilinifanya nipate furaha kupita kiasi nilipomsikia mzee Gurumo akisema kuwa anapenda kazi zangu, ukizingatia kuwa sisi wasanii wote tuliopo sasa tumetokana na kuangalia kazi za wakongwe wetu.

“Kwasababu hiyo basi, nimeamua kwa mapenzi yangu kwake kumnunua gari mzee Gurumo ili liweze kumsaidia katika mambo yake, ukiwa ni sehemu ndogo ya mchango wangu kwake,” alisema.

Hatua ya msanii huyo kumkabidhi ilizua gumzo ndani ya hoteli hiyo, kila mmoja akisema lake, hasa baada ya kuongozana hadi nje kulikopaki gari hilo aina ya Toyota Von Cargo FunCargo lenye thamani isiyopungua milioni saba.
 
Baada ya kupewa gari hilo, mzee Gurumo alishindwa kuzungumza kwa kirefu, akisema kuwa pumzi yake imegubikwa na furaha, hivyo sauti yake inashindwa kutoka kwa urahisi.

“Hili ni jambo kubwa linalonifanya nishindwe kuaamini mke wangu nyumbani atasema nini, hasa kwa kijana Diamond kuninunulia gari bila hata kutarajia.

“Namuombea kwa Mungu na hakika kila lenye kheri liwe ndani yake kwa kitendo chake cha kiungwana ambapo ameweza kunikomboa na kunifuta machozi,” alisema Gurumo.

Pamoja na yote hayo kutokea, wajuzi wa mambo wanaendelea kuwaza, kwanini msanii huyo ameamua kufanya mkutano wake katika hoteli ya Serena, yenye hadhi?

Jibu linalopatikana ni kutokana na mafanikio anayoendelea kuyapata siku hadi siku, ndio maana amekuwa mwepesi kubuni mambo ya kumtenganisha na nyota wengine.

Ni kama kuweka historia katika sanaa hiyo. Kwa wale wanaoendelea kupata msoto, lazima waamini kuwa kuna siku isiyokuwa na jina wanaweza kufikia walau robo ya mafanikio ya Diamond.

Kila kona anatajwa yeye. Akina dada ndio usiseme hadi Diamond kujipachika jina la Sukari ya warembo. Haya ni mafanikio ambayo yeye mwenyewe anasema yanatokea kwasababu ya kujituma kwake katika tasnia hiyo ya muziki wa kizazi kipya nchini.

Ukiacha wimbo huo wa My Number 1, Diamond pia anatamba na nyimbo zake za Kamwambie, Nataka Kulewa, Mbagala, Nimpende Nani, Kesho na nyinginezo lukuki.

Baada ya kuyaona hayo ya Diamond, swali linabaki vichwani mwa wadau wa muziki hapa nchini kuwa nani anaweza kufuata nyayo zake? Je, kwanini wadau wasiamini kuwa msanii huyo ana mafanikio makubwa kiasi cha kufikia kumnunulia gari mzee Gurumo?

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...