https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Saturday, August 10, 2013

Timu ya Mashorobaro wawatandika 4-2 mahasimu zao Men Stone katika mechi ya kusisimua kijiji cha Komsala, wilayani Handeni, mkoani Tanga



Na Sadiki Mbwana, Handeni
Timu ya soka Mashorobaro wamefanikiwa kuibuka na ushindi wa mabao 4-2 dhidi ya mahasimu zao Men Stone, zote za kijiji cha Komsala, wilayani Handeni, mkoani Tanga, katika mchezo wa kusisimua wa kirafiki wa sherehe za Idd El Fitri.

Mchezo huo ulikuwa na shangwe za aina yake kutokana na burudani ya aina yake dhidi ya vipai vya kucheza soka kwa vijana hao wanaowika pia katika mashindano mbalimbali yanayoanzishwa katika Kata ya Kwamatuku, wilayani Handeni mkoani Tanga.

Mabao ya Mashorobaro yaliwekwa kimiani na Julius Mwashiti, Malilo Gerevas, Juma Shaban na Joseph Goliama, wakati yale ya Men Stone yalifungwa na Hassan Kamota na Ally Hausi, likiwa ni pambano lililojaa ufundi wa kila aina.

Akizungumza mara baada ya mchezo huo, mmoja wa mashuhuda wa mchezo huo, Said Ling’ande, alisema kuwa mechi hiyo ilikuwa na msisimko wa aina yake, hivyo wanaamini watazamaji walipata burudani kamili.

“Kijiji hiki kimesheheni vipaji vya aina yake katika uchezaji wa soka, hivyo kunaposekana mechi za mashindano, wenyewe wanaingia uwanjani kwasababu kuna timu nyingi na zote zinacheza soka la uhakika.

“Tunashukuru Mungu kwa nguvu zake, hivyo hatuoni sababu ya kuendelea kukaa tu wakati watu wana vipaji vyao, ndio maana tunajaribu kujihusisha na michezo ikiwa ni kufanya mazoezi, ukizingatia kuwa michezo ni afya,” alisema Ling’ande.

Komsala ni kijiji cha kwanza kilichopo wilayani Handeni, mkoani Tanga, kinachopakana na wilaya ya Korogwe, huku kikiwa na vijana wengi wenye vipaji vya kucheza soka, licha ya eneo hilo kuadimika masuala ya kimichezo.


No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...