https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Saturday, August 31, 2013

Kweinchili: Bila sisi wenyewe Handeni haitabadilika, chifunge bete mwe vigudi.


Na Adam Malinda Seif.
KWA mara ya kwanza naomba kutumia nafasi hii niliyoomba mwenyewe katika mtandao huu (Blog ya Handeni Kwetu) ili kuunganisha mawazo ya yangu kwa Watanzania wenzangu, hususan wale wilaya ya Handeni na kupeana mawazo muafaka kwa mustakabali wa Taifa.
Adam Malinda, mwandishi wa makala haya.
Hii itafanikiwa kwa kuleta usawa, kushauriana kwa njia ya amani kabisa kutoka kwa sisi wananchi na viongozi tunaowachagua. Lengo ni si kupata sifa za mtu mmoja mmoja, bali ni kutafuta jawabu la matatizo ya waliowengi na hatimae kuondokana na ufukara uliokithiri.
Mkuu wa Wilaya Handeni, Muhingo Rweyemamu, pichani.
Kwa nafasi hii lengo ni kuunganisha nguvu kila upande ili kuwa kitu kimoja ingawa nafahamu kutoka hali fulani kwenda nyingine kuna changamoto nyingi ikiwa ni baadhi ya watu kuona wanaingiliwa katika maslahi yao, bila wao kujali wangapi wanaathirika na mfumo huo ambao wao kwao ni neema.

Lakini mara zote linapokuwepo tatizo katika mifumo fulani ya maisha inakuwa imetengenezwa kwa madhumuni fulani, hivyo tunapaswa kuwa wawazi katika kubainisha haya tunayoyazungunza yana faida ipi kwa walio wengi, na kuwasadikisha kuwa yakifanyika haya yataweza kufika kule wanakotarajia wengi, hali itakayohamasisha maendeleo tunayokusudia.

Nilijisikia hivi juzi aibu kubwa na kunichoma moyo pale jamaa mmoja ambaye sasa ni mchungaji wa dhehebu moja tulipokutana katika ofisi ya chombo kimoja cha habari akisahau  kwa kuniuliza hivi wewe ni kutoka eneo gani la Tanzania?

Nikamwambia natoka Handeni. Jibu lililofuata akaniambia ni wilaya moja ya watu waliochelewa kimaendeleo. Nilichukia, lakini nikamwambia si kweli, huku nikiumia.

Baadae kidogo nilimkumbuka kuwa ni mtu ambaye siku hizi amekuwa akitoa kauli za upiganaji vita vya madawa ya kulevya kupitia kanisa lake. Tulikuwa kukikutana Mbeya katika ofisi yake ya kupigania uhalibifu wa mazingira miaka 12 iliyopita.

Huyu mchungaji hadi naandika makala hii bado ananisononesha, lakini kwa upande wangu  najiuliza wanahandeni tulikosea wapi. Tufanye nini, kwa kuwa kumnyooshea mtu fulani kidole itakuwa si haki. Tujilaumu sisi wenyewe tutafute jawabu la kweli, tuache majungu, fitna, tuwe wawazi kueleza uhalisia na njia za kupita, badala ya kutafuta mchawi.

Naomba kila mtu ajiulize anataka kuifanyia nini Handeni na Tanzania kwa ujumla? Kitu cha kufanya ili kuondokana na hali ya kudidimia kwa uchumi, kukosa mwelekeo kwa kizazi cha sasa na kijacho.

Vikwazo gani vinasababisha kuwepo kwa hali hiyo, lakini pia tujitathimini  michango yetu ianzie katika changamoto ipi. Tusishike kila jambo tutapoteza mwelekeo kwa kuwa shida ni nyingi kuliko uwezo wetu.

Kupitia makala haya, ni vema kuanzia sasa kutafute njia za kuunganisha wana Handeni kwa kuona tuanze kuchangishana, ama kubuni mradi upi utakao weza kuchangia fedha kidogo kwa ajili ya kutatua kero za wananchi.

Huo utakuwa mwanzo wa wananchi kukubali jitihada za jamii yote, ikiwa pia ni njia ya kuunga mkono na kuwa kitu kimoja katika kuleta maendeleo yao kwa ujumla.

Naamini kuna wasomi wengi waliotokea Handeni karibu kila eneo la nchi lakini mwitikio ama mrejesho wa elimu zao hazijaonekana katika jamii, hasa katika kuhamasisha wananchi kujiunga katika kuleta maendele bila kujali dini zao na itikadi za siasa.

Wanapaswa kukumbuka kila msomi hata wa kidato cha sita na zaidi ametumia kodi ya wana Handeni kupata elimu na uwezo aliokuwa nao, deni hilo ni kama halipo kimtazamo lakini kihalisia lipo, sababu Handeni ni sehemu ya serikali ya Tanzania ambayo imejenga shule tulizosoma sisi wote.

Handeni ni sehemu mojawapo katika Tanzania yenye neema ya maziwa na asali, matunda na nyama, ambavyo kwa afya ya binadamu tunapaswa kunona, kujivunia, na kuheshimika katika macho ya wengine.

Lakini imekuwa kinyume chake. Je sisi wazawa tunafurahia hali hii? Kama tunafurahia basi elimu tuliyonayo haina faida kwa wana Handeni. Kama tunachukizwa kwa dhati toka mioyoni mwetu wakati ni huu.

Neema ya dhahabu, ardhi isiyohitaji mbolea ya viwandani, mabonde yanayopitisha maji mengi nyakati za masika, miti inayoweza kutengenezea samani na matumizi mengine ya kibinadam tutumie fulsa hii kuona mrejesho wa rasilimali hizi kuinua uchumi wa Handeni.

Tuanze sasa kila mmoja wetu kusema ikiwa ni mchango wa kuleta maendeleo kuwa anafikiri tufanye nini kuondokana na hali hiyo?, miradi gani tunaweza kubuni kujikomboa na umasikini wa familia zetu, tukikutana pamoja kimawazo, naamini hatushindwi kujua la kufanya, kwa kuwa wasomi wapo, hatukosi kujua tuanze vipi yapatikane matrekta ya kilimo cha kisasa, hatutashindwa kutafuta wafadhili kwa ajili ya miradi ya maji vijijini, hatutashindwa kukopeshwa zana na nyenzo za mashine za ufyatuaji matofali kuboresha makazi yetu, zahanati na mashule.

Kila mtu anapaswa kuwa makini katika ufanyaji kazi wake, sanjari na kushirikiana na mwenzake kwa ajili ya kufanikisha maendeleo ya Handeni na Tanzania kwa ujumla.

Hatuwezi kubeza hatua zilizofikiwa hadi hapa tulipo, viongozi waliopo wamefanya yale yaliyo ndani ya uwezo wao, nasi wana Handeni tunapaswa kuwaunga mkono.

Waliochoka wapunzike nasi tupokee vijiti tukimbie mbali zaidi na kupata ushindi wa kimaendeleo. Hii ni kutokana na ukweli kuwa baadhi ya watu watapinga jitihada za kimaendeleo kwakuhofia vyovyote watakavyojua wenyewe.

Nawaomba wasiwe na moyo huo, uongozi ni kipaji toka kwa mwenyezi mungu, ikiwa wanalitambua hilo, kila kiongozi ana zama zake hawezi kuwa milele na lazima ujuwe kuwa kiongozi mwenye busara ni yule anayewapa wananchi wake fulsa ya kutoa maoni yao, ushauri, na kuwaongoza.

Nasema hivi kwa kuwa mjadala huu si wa kwanza kufanywa na wakazi wa Handeni, siku nyingi zilizo pita tukiwa wadogo wengine tukiwa shule wakuu zetu walianzisha mipango madhubuti, lakini ilihujumiwa na baadhi ya watu kwa maslahi ya kiutawala, hali iliyozidisha kuidumaza Handeni.

Jambo hili halikuwa jema, ni dhambi kubwa ambayo sasa tusikubali kuirejea upya kama kweli tunahitaji maendeleo ya wilaya hii ambayo kwa sasa inatajwa kuwa Mkoa.

Kuhujumu uratibu wa kimaendeleo ni hatari na sumu inayotafuna wanajamii waliopo na kizazi kijacho. Naomba nisiwachoshe, tuandae fikra mpya, zenye mashiko, zisizojenga chuki kati yetu na viongozi.

Tuwape wananchi fulsa ya kuona nia njema ili nao wachangie mawazo yao, waeleze dukuduku zao, waseme shida zipi ni kipaumbele kwa Handeni nasi tujue tuanze na lipi kwa misaada toka wapi yaani wafadhili.

Lakini kwa wale wenye kuonesha nia na kutaka msaada huku wakiwa wameshaanza kufanya vitu vinavyoonekana machoni kwa watu.


Tukutane tena Jumamosi ijayo kwa makala za kweinchili, ubala wa watu walongela kwenchili wakengila mo lwazo, hegu  mwenkondo wamanya houkukongela, ubala wa minde mwaawadole.
adam.seif70@yahoo.com
+255 716236171

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...